19-Adabu Za Ndoa Katika Sunnah Iliyotakasika: Wakati Gani Unaruhusiwa Kurudia Jimai Baada Ya Hedhi?

Atakapokuwa ametwaharika kutokana na damu ya hedhi yote na kutoka kwake kumesimama kabisa, hapo anaruhusiwa kurudia kitendo cha jimai baada ya kuosha sehemu inayotoka damu, akafanya wudhuu au akakoga josho kamili (Ghuslu). Vyovyote kati ya haya matatu atakavyofanya itaruhusiwa kwao kurudia kitendo cha jimai kutokana na kauli ya Allaah سبحانه وتعالى katika Qur-aan:

  

َ ((فَإِذَا تَطَهَّرْنَ فَأْتُوهُنَّ مِنْ حَيْثُ أَمَرَكُمُ اللّهُ إِنَّ اللّهَ يُحِبُّ التَّوَّابِينَ وَيُحِبُّ الْمُتَطَهِّرِينَ))

 
((Wakishatoharika basi waendeeni Alivyokuamrisheni Allaah. Hakika Allaah Huwapenda wanaotubu na Huwapenda wanaojitakasa))

(Al-Baqarah 2:222)
 

Huu ni msimamo wa Ibn Hazm, 'Atwaa, Qataadah, Al-Awzaa'iy na Daawuud Adh-Dhwaahiriy na Mujaahid kama alivyosema Ibn Hazm, "Zote tatu hizi ni Twahara, kwa hiyo yoyote mojawapo atakayefanya baada ya kusimama hedhi yake, basi atakuwa ni halali kwa mumewe."

Kauli hiyo hiyo inatumika kumaanisha kuwa ni kuosha sehemu ya siri katika Aayah iliyoteremshwa kuhusu watu wa Qubaa:

 

((فِيهِ رِجَالٌ يُحِبُّونَ أَن يَتَطَهَّرُواْ وَاللّهُ يُحِبُّ الْمُطَّهِّرِينَ))

  

"…Humo wamo watu wanaopenda kujitakasa. Na Allaah Anawapenda wanaojitakasa" (At-Tawbah 9:108)

Hata hivyo, hakuna dalili yoyote katika Aayah au Sunnah inayoshurutisha Aayah "…Wakishatoharika basi waendeeni Alivyokuamrisheni Allaah…" (Al-Baqarah: 222) inayohusika katika maana tatu hizo, na kufanya hivyo kunahitaji dalili. (huu ni msimamo wa Ibn Hazm)

 

 

Share