Asiye Muislam Anataka Kusilimu Kwa Kunioa, Nikikataa Itahesabikaje?

 

SWALI:

Ningependa kuuliza suala kama ifuatavyo

mimi ni msichana mwenye umri wa karibia miaka 25, ninaesoma nje ya nchi . huko ninakaa peke yangu. nimejitahidi kufuata dini kwa kadri ninavyoweza kwa kipindi chote nilichokuwepo huku masomoni kwa bahati mbaya au nzuri, ametokea mtu ambae si muislam kunipenda na kutaka kuniona (hatujawahi kufanya kitendo kibaya chochote), jee nini uhalali wa ndoa pamoja na yeye ikiwa atasilimu? Na ikiwa nitakataa kuolewa naye, nitahesabika kuwa nimemumzuilia mtu nafasi ya kuingia kwenye usilam?

naomba majibu yenu

 


JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani za dhati kwa dada yetu aliyeuliza swali kuhusu jambo muhimu katika maisha yetu hapa ulimwenguni. Hasa ikiwa suala hilo likiwa ni mahusiano ya kijamii baina ya Muislamu na asiyekuwa Muislamu.

Mwanzo kabisa tunakupatia hongera zetu kwa kushikilia Dini yako katika nchi ya ugeni ambapo wengi wanapotea kwa kutoweza kushikilia jambo hilo. Hiyo inatokana ima na kutopata malezi mazuri kutoka kwa wazazi, au kuwa na marafiki wabaya na pengine wasiokuwa Waislamu, kujiona kujitambulisha kwako na Uislamu ni kujitweza au kuona kuwa ugenini unaweza kufanya lolote kulingana na msemo 'When in Rome do as the Romans do' - "Don't set your own rules when you are someone's guest” - (Ukiwa Roma fanya kama Warumi). Huu ni msemo ambayo unakwenda kinyume kabisa na maadili ya Kiislamu. Na ni msemo ambao asili yake ni wa mmoja wa wakuu wa kikrsto aitwaye Saint Ambrose (340-397), ambaye alimshauri Saint Augustine kwa kumwambia: Si fueris Romae, Romano vivito more; si fueris alibi, vivito sicut ibi ('When you are in Rome live in the Roman style; when you are elsewhere live as they live elsewhere') – Ukiwa Roma ishi kwa mtindo wa maisha ya ki-Roma, na ukiwa pengine, ishi kama wanavyoishi huko”

Ni msemo unaotumiwa na Waislam wengi kwa kuiga na wengine huufan yia kazi kabisa kimaisha, na hali ni msemo unaopingana kabisa na Dini yetu na unaogongana na Uislam kama ndio sehemu ya maisha yetu katika kila Nyanja na katika kila sehemu na kila wakati. Utakapoufuata msemo huo kama ambavyo tunaona kwa wengi wanaoishi Ulaya baada ya kutoka na maadili yao mazuri kutoka Tanzania, Zanzibar, Kenya na kwengineko kwa kufuata utamaduni wa ki-Magharibi wa kuwa na ‘boy friends’ na ‘girl friends’ n.k, basi utakuwa umejivua na sifa za Uislam na kuelekea kwenye hizo sifa za nasaha za kina Saint Ambrose na mwisho wake utakuwa ni mtu aliyebakiwa na jina la Kiislam lakini matendo ya kikafiri.

Nasaha yetu ya kwanza kwa dada yetu ni kuwa upate marafiki wa kike wa Kiislamu walio wema ili upate kukabiliana na changamoto za huko. Ikiwa unaishi karibu na Msikiti na ipo sehemu ya wanawake ya masomo ya Dini ujiunge nao. Ikiwa hakuna Msikiti lakini zipo sehemu ambazo Waumini wanakutana ima siku za wikiendi utafute njia ya kuweza kuwa nao. Hii ni kuwa, kusikiliza mawaidha kunamsaidia Muislamu kuweza kukabiliana na mitihani kama hiyo yako kwani utakuwa na wenzi wako watakaokusaidia kwa nasaha, fikra na mengineyo.

Ile hali ya kuwa mpaka sasa hamjafanya chochote kibaya ni dalili ya kuwa unaweza kukumbana na vishawishi katika maisha. Baada ya kusema hayo inahitajia uwe mkakamavu zaidi kwani mara nyingi wasichana kwa ujumla wao wanakuwa rahisi kudanganywa na kushawishiwa kuingia katika tendo la mapenzi kabla hata ya kuolewa.

Pindi atakaposilimu ndoa yenu ikiwa itatimiza masharti mengine itakuwa halali. Lakini swali la kujiuliza ni: Je, huyu mvulana anataka kuingia katika Uislamu kwa sababu ya kunipata mimi au kwa kuipenda Dini yenyewe? Hivyo, hapana budi kumfanyia mtihani na kujua uhakika wake. Jambo kama hili liliwahi kutokea katika wakati wa Shaykh Muhammad Qaasim Mazrui akiwa Qaadhi mkuu wa Kenya. Alitakwa shauri na mzazi ambaye binti yake aliposwa na Mzungu aliyekuwa tayari kusilimu. Shaykh Muhammad Qaasim alimwambia bwana huyo kuwa wazazi wa binti wameghairi katika suala hilo la ndoa lakini yeye anaweza kuendelea kusilimu. Aliposikia hayo bwana huyo alimaka kwa kusema ikiwa ni hivyo basi hana haja ya kusilimu tena.

Ni juu yako kama Muislamu mwanzo kabisa kumchunguza kuhusu ukweli wake au ni kuwa anakutaka wewe na kusilimu ni chambo tu. Katika mas-ala ya mtu kusilimu isiwe tunafanya haraka kumuozesha kabla ya kupata tamkini na uhakika wa kusilimu kwake. Yapo matatizo mengi yanayotokea kwa mtu kusilimu na kisha kuoa bila ya kupatiwa mafunzo ya aina yoyote. Mara nyingi ndoa hizo hazidumu kwani mkikosana kidogo tu huyo mume atarudi katika dini yake ya awali na huenda ikiwa mmeshazaa naye na hivyo kuna hatari hata ya kuja kukimbia na mtoto. Vilevile udhaifu wa binti kwa kiasi fulani huwafanya na wao pia wakaritadi jambo ambalo ni hasara kubwa kwa Waislamu.

Ikiwa umeona ya kwamba huna budi kuoana naye basi itabidi umwambie wazi kuwa ndoa haiwezi kuwa moja kwa moja baada ya kusilimu kwake. Ni juu yake mwanzo ajifunze Dini ya Uislamu kwa muda usiopungua miezi sita. Katika kipindi hicho unaweza kutathmini uhakika wake wa kuingia katika Dini. Katika hilo ikiwa utakuwa na ndugu wa Kiislamu wakupatie ushauri baada ya hayo na hasa mwalimu wake anayemfundisha. Huna budi pia kuwajulisha wazazi wako kwa hatua hiyo ambayo umeiona kuwa inakufaa katika maisha yako na Imani yako. Ikiwa wazazi hawana pingamizi basi ni juu yako kuswali Swalah ya kumtaka ushauri Allaah Aliyetukuka (Swalatul-Istikhaarah Swalah ya Istikhaarah ) ambayo ni rakaa mbili naye Allaah Atakuongoza kwa lililo la kheri nawe katika Dini yako, maisha na hatima yako atakufanyia sahali.

 

Ikiwa wazazi wameridhia hasa baba ambaye ni walii wako basi ndoa itakuwa halali kwani Mtume Muhammad (Swalla Alaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema kuwa hapana ndoa bila walii. Hii ina maana hata ikiwa umekubaliana na huyo bwana huwezi kujiozesha mpaka upate  idhini ya walii wako.

Kipengele cha mwisho katika swali lako ni kuwa kukataa kwako kuolewa na huyo bwana hata baada ya kuwa amesilimu na akawa ni Muislamu mzuri hutakuwa na makosa wala dhambi aina yoyote. Ikiwa yeye amesilimu kwa sababu ya Dini yenyewe au anataka kusilimu kwa sababu hiyo hatatishwa kukataa kwako kwani lengo lake si wewe bali kufika katika njia nyoofu. Hata pindi unapokataa kuolewa naye, naye akakataa kusilimu au akaritadi basi wewe hutakuwa na dhima yoyote wala dhambi. Kosa litakuwa kwake kwani atakuwa tayari amejua ukweli wa Uislamu. Wewe hutakuwa umemzuia kuingia katika Uislamu bali amejizuia mwenyewe. Mtu huyo anaingia katika ile Hadiyth ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliposema:

“…na ambaye kuhama kwake ni kwa ajili ya kuupata ulimwengu au mwanamke wa kumuoa, basi kuhama kwake ni kwa lile alilohamia

(Ahmad, al-Bukhaariy, Muslim, Abu Daawuud, at-Tirmidhiy, an-Nasaaiy na Ibn Maajah). Usibabaike kwa hilo bali mtegemee Allaah Aliyetukuka naye Atakuongoza katika njia iliyonyooka.

Tunamuomba Allaah Aliyetukuka Akupatie subra, utulivu, umakini, usighurike kwa chochote wala lolote na Akupe lililo na kheri nawe hapa duniani na Kesho Akhera pamoja na kukuweka katika Imani thabiti.

Na Allaah Anajua zaidi   

Share