Kumbikumbi Wanafaa Kuliwa?

 

 

Kumbikumbi Wanafaa Kuliwa?

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

assalam alaykum warahmatullah wabarakatuh, amma baada. kuna itilafu nyingi zijadiliwazo kuhusu ulaji wa Kumbikumbi je, inaswihi kula kumbikumbi kisheria?

 

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Kumbikumbi ni jamii ya wadudu warukao ambao hupatikana katika baadhi ya maeneo na katika baadhi ya misimu, na hujulikana kwa majina tofauti baina ya eneo na eneo.

 

Kwa kuwa jina la Kumbikumbi halipatikani katika lugha ya kiarabu imekuwa vigumu kueleweka hukmu ya kuliwa kwa mdudu huyo, na kwa msingi huo watu wamegawanyika katika makundi mawili wanaohalalisha na wanaoharamisha; wanaohalalisha kuliwa wanategemea vigezo vifuatavyo:

 

 

1-Kwamba kumbikumbi ni jamii ya nzige, kwa kuwa nzige amehalalishwa kuliwa, basi na kumbikumbi naye ni halaal kuliwa na wakatoa dalili kuwa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  katika hadiyth iliyopokewa na Ibn 'Umar Amesema:

 

“Tumehalalishiwa maiti mbili, na damu mbili, Samaki na nzige, na ini na bandama” [An-Nawawiy]

 

 

 

2-Hoja nyingine ni Hadiyth:

 

عَنِ ابْنِ عَبَّاسٍ، قَالَ كَانَ أَهْلُ الْجَاهِلِيَّةِ يَأْكُلُونَ أَشْيَاءَ وَيَتْرُكُونَ أَشْيَاءَ تَقَذُّرًا فَبَعَثَ اللَّهُ تَعَالَى نَبِيَّهُ وَأَنْزَلَ كِتَابَهُ وَأَحَلَّ حَلاَلَهُ وَحَرَّمَ حَرَامَهُ فَمَا أَحَلَّ فَهُوَ حَلاَلٌ وَمَا حَرَّمَ فَهُوَ حَرَامٌ وَمَا سَكَتَ عَنْهُ فَهُوَ عَفْوٌ وَتَلاَ: (( ‏قُلْ لاَ أَجِدُ فِيمَا أُوحِيَ إِلَىَّ مُحَرَّمًا )) إِلَى آخِرِ الآيَةِ ‏

“Walikuwa watu wa Jaahilyyah wanakula baadhi ya vitu na kuacha baadhi ya vitu kwa kuona kinyaa, Allaah Akamtuma Rasuli Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  na Akateremsha Kitabu chake, Akahalalisha vya halaal na kuharamisha vya haraam  Alivyohalalisha ndio halaal, na Alivyoharamisha ndio haraam, na Alivyo vinyamazia ndio vilivyosamehewa ” Kisha akasoma maneno ya Allaah:

 

 

قُل لَّا أَجِدُ فِي مَا أُوحِيَ إِلَيَّ مُحَرَّمًا عَلَىٰ طَاعِمٍ يَطْعَمُهُ إِلَّا أَن يَكُونَ مَيْتَةً أَوْ دَمًا مَّسْفُوحًا أَوْ لَحْمَ خِنزِيرٍ فَإِنَّهُ رِجْسٌ أَوْ فِسْقًا أُهِلَّ لِغَيْرِ اللَّـهِ بِهِ ۚ فَمَنِ اضْطُرَّ غَيْرَ بَاغٍ وَلَا عَادٍ فَإِنَّ رَبَّكَ غَفُورٌ رَّحِيمٌ ﴿١٤٥﴾

Sema: Sipati katika yale niliyofunuliwa Wahyi kwangu kilichoharamishwa kwa mlaji kukila isipokuwa kiwe ni nyamafu au damu inayomwagika au nyama ya nguruwe; kwani hiyo ni najisi au ufasiki; kimetajiwa asiyekuwa Allaah (katika kuchinjwa). Lakini atakayefikwa na dharura bila ya kutamani wala kuvuka mipaka, basi hakika Rabb wako ni Mwingi wa kughufuria, Mwenye kurehemu. [Al-An’aam: 145] [Hadiyth katika Sunan Abiy Daawuwd na Musnad Ahamd ameisahihisha Al-Albaaniy (5/13)]

 

 

Kwa hoja hizo mbili kundi hili linaona kula kumbikumbi ni halaal, kwani ni jamii ya nzige ambao ni halaal kuliwa kwa mujibu wa kauli ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  na maelezo ya Ibn 'Abbaas kuwa kilichonyamaziwa na Allaah ni ruhusa kuliwa.

 

Ama wale wanaoharamisha kuliwa kwa kumbikumbi wao wanasema:

 

Uislamu una Shariy’ah yake katika mas-ala ya chakula. Chakula cha Muislamu kina masharti na hawezi mmoja wetu kula anachotaka bila kurudi katika maandiko.

 

 

Uislamu umekataza kuliwa nyamafu, hata hivyo ukaruhusu kuliwa kwa samaki na nzige hata wakiwa wamepatikana wakiwa tayari wamekufa. Hayo yanaeleweka na kila mmoja wetu, hata yule Muislamu wa kawaida.

 

 

Shaykh Al-Amiyn bin 'Aliy, katika kitabu chake Majina ya Nyama kwa Kiswahili na Kiarabu, ametupatia faida kwa nyama zilizo halaal na haraam na akatupatia baadhi ya faida. Miongoni mwa faida ni yafuatayo:

"Nyama waliwawo hawawi halaal ila baada ya kutindwa tindo (kuchinjwa chinjo) la Shariy’ah, ila nzige na waishio baharini, kama samaki, papa na wengineo, hawa hawaihitajii kutindwa (kuchinjwa)". 

 

 

Hitimisho 

 

Ni vema kwa Muislamu akajiepusha na mambo yasiokuwa na ushahidi ndani yake, au yenye shaka ili kubakia salama. Kula kumbikumbi ni jambo ambalo halina kishiko ndani ya Shariy’ah za Kiislamu, ni vema kwa Muislamu kujiepusha na kuwala wadudu hao, hususan watu huwala kwa matamanio tu  na siyo kama chakula cha msingi. Na kujiepusha na mambo yaliyo na shaka ndivyo tulivyoamrishwa na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa alihi wa sallam): Kutoka kwa  Abuu 'Abdillaah An-Nu’umaan bin Bashiyr (Radhwiya Allaahu ‘anhu)  ambaye alisema: Nilimsikia Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa alihi wa sallam)  akisema:  ((Halaal iko wazi na haraam iko wazi, baina yao ni vitu vyenye shaka ambavyo watu wengi hawajui.  Kwa hivyo, yule anayeepuka vyenye shaka  anajisafisha nafsi yake kwenye dini yake na heshima yake, lakini yule anayetumbukia katika mambo yenye shaka, huanguka katika haraam, kama mchunga anayechunga pembezoni mwa mpaka, mara  huingia ndani (ya shamba la mtu).  Hakika kila mfalme ana mipaka yake, na mipaka ya Allaah ni makatazo Yake…)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Kwa kumalizia, tukija katika suala hili la kumbikumbi tutakuta kuwa haikutajwa katika Qur-aan wala Sunnah kuwa ni halaal. Kwa kutotajwa kuwa ni hivyo, wadudu hao wanakuwa ni haraam kwa kanuni tulizozitaja hapo juu. Na hasa kuwa mnyama mpaka achinjwe ndio awe halaal isipokuwa waliotajwa kama samaki na nzige, na kumbikumbi hawamo katika hao. Hivyo, wanakuwa ni haraam kwetu kuwala. 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share