032-Sifa Ya Swalah Ya Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi Wa Aalihi Wa Sallam): Kurukuu, Sifa Na Ulazima Wa Kutulia Katika Rukuu

 

KURUKUU

 

Baada ya kumaliza kisomo chake   (صلى الله عليه وآله وسلم), alikuwa akinyamaza kinyamazo kidogo([1]

), kisha huinua mikono yake(

[2]

) kwa namna zilizotangulia kuelezwa katika 'Takbiyr Ya Kufungulia, akaleta Takbiyr(

[3]

) na akarukuu.(

[4]

).

 

Na pia alimuamrisha mambo mawili hayo aliyeswali vibaya kwa kumwambia: ((Hakika Swalah ya mmoja wenu haitotimia mpaka akamilishe wudhuu vizuri kama Allaah Alivyoamrisha… kisha alete Takbiyr, amsifu na kumtukuza Yeye, na asome kiasi kinachosahilika tu kwake katika Qur-aan miongoni mwa Aliyofunzwa na Allaah (kwa kiasi cha wepesi) na uwezo wake, kisha alete Takbiyr na arukuu [na aweke mikono yake miwili juu ya magoti yake mawili] mpaka viungo vyake vitulie na vipumzike…))(

[5]

).

 

 

 

SIFA YA RUKUU

 

Alikuwa  (صلى الله عليه وآله وسلم)akiweka viganja vyake juu ya magoti yake(

[6]

) na alikuwa akiwaamrisha kufanya hivyo(

[7]

) kama alivyomuamrisha mtu aliyeswali vibaya, kama ilivyoelezwa nyuma.

 

Alikuwa (صلى الله عليه وآله وسلم) akiimakinisha mikono yake barabara na magoti yake (kama kwamba akiyashikilia](

[8]

), na alikuwa akivichanua vidole vyake(

[9]

), na alimuamrisha aliyeswali vibaya kama hivyo, kwa kumwambia: ((Utakaporukuu, weka viganja vya mikono yako juu ya magoti yako, na kisha vichanue vidole vyako, kisha bakia (hivyo) hadi kila kiungo kitue  mahali pake))(

[10]

).

 

Alikuwa akijitawanya (sio kujigandamiza mkao mmoja) na akitenganisha viwiko vya mikono na ubavu wake.(

[11]

)

 

Alikuwa (صلى الله عليه وآله وسلم) anaporukuu, hutandaza mgongo wake na kuusawazisha(

[12]

) kiasi kwamba kama ungelimwagiwa maji, basi yangelitua (

[13]

). Na pia alimwambia aliyeswali vibaya: ((Utakaporukuu, weka viwiko vyako juu ya magoti yako, na tawanya mgongo wako na makinisha madhubuti rukuu yako)).(

[14]

)

 

Alikuwa (صلى الله عليه وآله وسلم) hainamishi kichwa chake wala hakinyanyui (zaidi ya mgongo wake),(

[15]

) bali kilikuwa baina yake.(

[16]

)

 

 

ULAZIMA WA KUTULIA KATIKA RUKUU

 

Alikuwa (صلى الله عليه وآله وسلم) akitulia kwenye rukuu yake, na alimuamrisha awe hivyo aliyeswali vibaya, kama ilivyotajwa katika mlango wa rukuu.

 

Alikuwa (صلى الله عليه وآله وسلم) akisema: ((Kamilisheni rukuu na sujudu, kwani naapa kwa Yule Ambaye nafsi yangu imo Mikononi Mwake, hakika mimi nakuoneni nyuma yangu(

[17]

) mnaporukuu na mnaposujudu)).(

[18]

)

 

Alimuona mtu anaswali bila ya kukamilisha rukuu yake sawa sawa, akidonoa katika sujuud yake, akasema (صلى الله عليه وآله وسلم): ((Lau atakufa mtu huyu katika hali yake hii, basi atakuwa amekufa katika Mila isiyokuwa ya Muhammad, [anadonoa katika Swalah yake kama adonoavyo kunguru damu]. Mfano wa yule asiyekamilisha rukuu yake na akadonoa katika sujudu yake, ni kama mfano wa mwenye njaa anayekula tende moja au tende mbili, ambazo hazitomfaidisha kitu chochote))(

[19]

)

 

Abu Hurayrah (رضي الله عنه) alisema: "Rafiki yangu mpenzi  (صلى الله عليه وآله وسلم) amenikataza kudonoa katika Swalah yangu mdonowo wa  jogoo na kugeuka geuka kama ageukavyo mbweha, na kuchuchumaa kama achuchumaavyo tumbili"(

[20]

).

 

Mjumbe wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) alikuwa akisema: ((Mwizi muovu kabisa miongoni mwa wevi ni yule anayeiba katika Swalah yake)). Wakasema: "Ewe Mjumbe wa Allaah! Vipi anaiba katika Swalah yake"? Akasema: ((Hatimizi rukuu yake na sujuud yake))(

[21]

)

 

Mara moja, alikuwa (صلى الله عليه وآله وسلم) akiswali, na alitupa jicho kwa mtu ambaye hakusawazisha uti wa mgongo wake katika rukuu na sujuud. Alipomaliza alisema: ((Enyi Waislamu! Hakika hakuna Swalah kwa yule asiyesawazisha uti wake wa mgongo katika rukuu na sujuud)).(

[22]

)

 

Akasema katika Hadiyth nyingine: ((Swalah ya mtu haihesabiwi hadi asawazishe mgongo wake katika rukuu na sujuud)).(

[23]

)

 



[1]

Abu Daawuud na Al-Haakim ambaye amesema kuwa ni Swahiyh na Adh-Dhahabiy amekubaliana naye.

[2]

Al-Bukhaariy na Muslim. Huku kuinua mikono ni jambo lililothibiti kutoka kwake (صلى الله عليه وآله وسلم) kwa njia ya mutawaatir (Iliyopokelewa na idadi kubwa -ya watu- yenye kuwa muhali katika kawaida kukubaliana kusema uongo) kutoka kwa Mtume (صلى الله عليه وآله وسلم). Na vile vile imethibiti kutoka kwake (صلى الله عليه وآله وسلم) kwa njia hiyo hiyo ya mutawaatir, kuinua mikono wakati wa kunyanyuka -wakati wa kuitadili - kutoka kwenye rukuu mpaka alingane sawa hali ya kusimama. Na hivi ndivyo walivyokwenda Maimaamu watatu; Maalik, Ash-Shaafi'iy na Ahmad, na wengineo katika kundi kubwa la Maulamaa wa Hadiyth na Maulamaa wa Fiqh. Na ndio mwenendo alioshikamana nao Imaam Maalik (رحمه الله) hadi kufa kwake kama ilivyoripotiwa na Ibn 'Asaakir (15/78/2). Baadhi ya Mahanafi wamechagua kufanya hivyo. Miongoni mwao ni 'Iyswaam bin Yuusuf Abu 'Aswmah Al-Balkhiy (aliyefariki 210) ambaye ni mwanafunzi wa Imaam Abu Yuusuf (رحمه الله), kama ilivyoelezewa katika utangulizi. 'Abdullaah bin Ahmad ameripoti kutoka kwa baba yake katika Masaail yake (Uk. 60).

"Imesimuliwa kutoka kwa 'Uqbah bin 'Aamir kwamba amesema kuhusiana na kunyanyua mikono miwili katika Swalah: "Anapata mema kumi kwa kila anapoinyanyua". Nikasema: Yana ushahidi - maneno ya ‘Uqbah - wenye nguvu kutokana na Hadiythul-Qudisy isemayo: ((…mwenye kutia nia ya kitendo chema na akakitekeleza, Allaah Atamuandikia mema kumi hadi mia saba)). Imesimuliwa na Ash-Shaykhaayn. Taz. Swahiyh At-Targhiyb Namba 16.

[3]

Kifungu kile kile kilichotajwa hapo mbeleni.

[4]

Kifungu kile kile kilichotajwa hapo mbeleni.   

[5]

Abu Daawuud na An-Nasaaiy. Al-Haakim amesema ni Swahiyh na Adh-Dhahabiy amekubaliana naye.

[6]

Al-Bukhaariy na Abu Daawuud.

[7]

Al-Bukhaariy na Muslim.

[8]

Al-Bukhaariy na Abu Daawuud.

[9]

Al-Haakim ambaye amesema ni Swahiyh. Adh-Dhahabiy na Atw-Twayaalisy wamekubaliana naye. Imetolewa katika Swahiyh Abu Daawuud (809).

[10]

Ibn Khuzaymah na Ibn Hibbaan katika Swahiyh zao.

[11]

At-Tirmidhiy ambaye amesema ni Swahiyh, na Ibn Khuzaymah.

[12]

Al-Bukhaariy na Al-Bayhaqiy kwa isnaad Swahiyh.

[13]

Atw -Twabaraaniy katika Mu'jam Al-Kabiyr na Mu'jam As-Swaghiyr, 'Abdullaah bin Ahmad katika Zawaaid Al-Musnad na Ibn Maajah.

[14]

Ahmad na Abu Daawuud kwa isnaad Swahiyh.

[15]

Abu Daawuud na Al-Bukhaariy katika Juzuu Al-Qaari'ah kwa isnaad Swahiyh.  Na maana ya hakinyanyui, ni kuwa hakinyanyui kichwa chake mpaka kikawa juu zaidi ya mgongo wake, bali kinakuwa usawa wa mgongo.

[16]

Muslim na Abu 'Awaanah.

[17]

Nasema na kuona huku ni kuona kwa uhakika wake kimaumbile, na ni miongoni mwa miujiza yake (صلى الله عليه وآله وسلم), nako ni katika Swalah basi. Na hakuna dalili ya kuona kwa ujumla.

[18]

Al-Bukhaariy na Muslim.

[19]

Abu Ya'alaa katika Musnad yake (340/3491/1), Al-Aajuriy katika Al-Arba'iyn, Al-Bayhaqiy, Atw-Twabaraaniy (1/192/1), Adhw-Dhwiyaa katika Al-Muntaqaa (276/1), Ibn 'Asaakir (2/226/2, 414/1, 8/14/1, 76/2) kwa isnaad nzuri. Na Ibn Khuzaymah amesema ni Swahiyh (1/82/1). Ibn Batwtwah katika Al-Ibaanah (5/43/1) anao usimulizi Mursal -Hadiyth mwisho wa isnad yake ameangushwa Swahaba- unaounga mkono sehemu ya mwanzo ya Hadiyth ukitoa ziada katika Al-Ibaanah (5/43/1).

[20]

Atw-Twayaalisy, Ahmad na Ibn Abi Shaybah. Ni Hadiyth Hasan, kama nilivyoielezea katika tanbihi zangu kwenye Al-Ahkaam (1348) ya 'Abdul-Haqq Ishbiyliy (1348). 

[21]

Ibn Abi Shaybah (1/89/2), Atw-Twabaraaniy na Al-Haakim ambaye amesema ni Swahiyh, na Adh-Dhahabiy amekubaliana naye.

[22]

Ibn Abi Shaybah (1/89/1), Ibn Maajah na Ahmad kwa isnaad Swahiyh.

[23]

Abu 'Awaanah, Abu Daawuud na As-Sahmiy (61). Ad-Daaraqutwniy amesema ni Swahiyh.

Share