Mume Amechukua Pesa Zangu Hataki Kunilipa Naye Hana Shida, Nimezidi Kuchukiwa Naye, Nadai Talaka Je Nina Haki?

SWALI: 

 

Mume wangu alinichukulia pesa zangu katika account yangu ambazo nilikua nazihifadhi kwa muda mrefu kidogo kidogo.Anajua pin yangu na kachukua card yangu amezitoa zote. Zaidi ya Milioni sita za Tsh lakini ni pesa za kigeni, tunaishi huku ulaya. Nilipokwenda kuangalia sikuona kitu nilipomuuliza alisema amezichukua alikua na shida. Nilipokua namdai anasema, umepata wapi kuona mke anamdai mumewe. Jambo hili pia limenichukiza sana na kila nikikumbuka linaniumiza roho yangu. Kwasababu nilitaka kufanyia shughuli zangu za familia yangu,jee nami sina haki kusaidia familia yangu.nimekua ninahifadhi pesa zangu tena hivi karibuni amezichukua pesa nyenginge nyingi zaidi kuliko zile za mwanzo. pia anasema alikua ana shida. yeye anafanya kazi anapata kila anachokitaka sijui shida gani, hakuwahi kunielezea.nimemshataki kwawazee anasema atanipa sijui lini.jee mume kama huyu anakubalika katika uislam.na mambo mengi ndio yamezidi kuchangia nidai talaka yangu.au sina haki hii


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalah Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Hakuna kosa wala katazo kwa mume kuchukua mali yako ikiwa kwa ridhaa yako, kwani katika Uislamu mke ana haki ya kumiliki mali yake na ana haki ya kumpa amtakae na ana haki ya kumsamehe amtakae ikiwa anamdai na mume hana haki ya kumuingilia mkewe katika maamuzi yake haya au kumkatalia.

Hata hivyo, kama mke atamruhusu mumewe kutumia mali yake basi hakuna tatizo, ila ni vyema ieleweke kuwa haijuzu kwa mume kumfanyia maudhi na kumdhuru mkewe kwa sababu ya kutotoa mali yake mke.

Mume kujua pin number yako ni ishara kuwa uliwahi kumpatia kwa mapenzi yenu na kumpa card yako ili atoe fedha katika account yako na huenda sasa hakuna masikilizano kwa sabau moja au nyengine; hivyo basi ikiwa hakuna masikilizano wala mapenzi baina yenu basi ni vyema huyo mume akuache kwani nyumba isiyokuwa na mapenzi wala rehma huwa si nyumba; kama hataki kukuacha ushauri ni kufikisha kadhia yako mbele ya Qaadhi na yeye atakupa haki yako ya talaka.

Ama ikiwa sababu ni kuwa anakuchukulia mali yako na uliwahi mwenyewe siku za nyuma kumtunukia mali au pin number na zaidi ya hayo kwa penzi lako kwake na sasa haliko kwa sababu moja au nyengine, basi utahitaji kuthibitisha madai yako na utahitaji kuwasilisha kadhia yako mbele ya wahusika, kama inavyoshauri Qur-aan:

“Na mkichelea kutakuwapo mfarakano baina ya mke na mume basi pelekeni muamuzi kutokana na jamaa za mume, na muamuzi kutokana na jamaa za mke. Wakitaka mapatano Allaah Atawawezesha. Hakika Allaah ni Mjuzi Mwenye khabari” An-Nisaa: 35.

Kusema kwake, Umepata wapi kuona mke kumdai mumewe, ni kwa kuwa ulimpa kwa mapenzi na ulimtunuku kwa sababu uzijuazo wewe mwenyewe.

“….wakikutunukieni kitu katika mahari, kwa radhi yao, basi kileni kiwashuke kwa raha” An-Nisaa: 4.

Hii ni kuwa umemtunuku na kama ulimpa kwa makubaliano yenye uthibitisho kuwa ni deni basi ni haki yako kumdai na ni juu yake kulilipa deni hilo kwani ni haki yako kama unaweza kuthibitisha madai yako.

Ushauri ni kuwa kama huna mapenzi na huyo mumeo basi ni vyema muachane kwa ihsaan na kwa wema kwani sababu nyengine za kuwa kakuchukulia fedha zako huwa hazina msingi kama hutoweza kuthibitisha madai yako ama kuwa huna mapenzi naye ni jambo la kawaida kuwa mshachokana na umeonelea kutafuta mwengine na kila mmoja atapata mwengine hakuna haja ya ugomvi wala kuvutana.

Mume kama huyo anakubalika Kiislam, kwani Waislamu ni watu wenye kutegemewa na kutarajiwa kufanya makosa na kurudi kwa Mola, wanatarajiwa kufikwa na mitihani kama hiyo au zaidi ya hiyo ya ndani ya nyumba zao na ahli zao na kuwepo wa kuwapatanisha na kuwasuluhisha; na kama wewe humtaki basi watakuwepo wengi wenye hamu na tamaa ya kuolewa na yeye kama watakavyokuwepo wengi na wenye tamaa ya kukuoa wewe kama mkiachana lakini muachane kwa wema na ihsaan sio kwa ugomvi na malumbano yasiyo kuwa na faida wala maana katika dini na dunia yenu.

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share