Familia Ya Mume Wanashiriki Majini, Kumtahiri Mtoto Kaambiwa Lazima Ruhusa Ya Majini Wao

 

Familia Ya Mume Wanashiriki Majini, Kumtahiri

Mtoto Kaambiwa Lazima Ruhusa Ya Majini Wao

 

Alhidaaya.com

 

SWALI:

 

Assalamu aleykum warahmatullahi wabarakatu, dadangu alalamika sana kuwa katika family aliyo olewa wanayapendekeza sana mambo ya Ushirikina mwisho wakwisha anaeumwa nakitwa kidogo husema amerogwa, sasa mwezi uliopita alhamdulillahi alijifunguwa mtoto wa kiume alipokuwa ataka kumtahiri akaambiwa asende kumtahiri mpaka apawe ruhusa na majini wa kina mumewe tulipopawa habari hizi tulishtuka sana kwa sababu hivi sivoilivo kidini yetu ya kiislamu haijatufundisha mambo hayo tena dini yetu tukufu yameyapiga vita vikali mambo yakumshirikisha Allaah Subhaanahu wa Ta'aalaa, sasa dadangu na mimi pia twaomba mututolee namna yakueza kuepukana na mtihani huu uliompata dadangu ni mpendae, jee tufanyeje maana haya simadogo? Wanaudhu Billahi Minal Mushrikin!! Shukran wajazakaallah kher wa ramadhan kareem.

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Hakika tatizo hili ambalo limewakumba si dogo katika Dini, bali ni kuivunja Dini yenyewe na kujitoa katika Uislamu. Kuhusu hili Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ametuweka wazi kabisa kuwa ushirikina ni dhambi ambayo haisamehewi kabisa na inaharibu ‘amali zote ikiwa mtu atakufa bila kutubia.

 

Hata hivyo, kosa linatoka kwenu zaidi kuliko kwa upande wa mume kwani nyinyi ndio mlimkubali huyo mume na mkaacha maagizo ya Dini yetu. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametuusia sana tuwe makini katika kuchagua mume. Na miongoni mwa sifa anazofaa aangalie mke mtarajiwa kwa mume ni Dini na maadili mema. Inaonyesha kuwa hayo hamkuyatazama na ndio mnakumbana na haya matatizo kwani kama mngechunguza mngeyaona hayo na hivyo kukataa posa hiyo.

 

Kwa hayo ambayo mnayokumbana nayo inatakiwa mfanye yafuatayo:

 

1.  Mwanzo una wajibu wa kumtoa mumeo katika ushirikina ambalo ni dhambi kubwa la mwanzo na ni kinyume na Tawhiyd ya kumpwekesha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa). Kwa hiyo, jaribu kuzungumza na mumeo kwa njia nzuri umueleze uovu wa suala hilo. Na ikiwa utapata vitabu kuhusu hilo, kaseti au chochote ambacho kinaweza kumsaidia.

2.  Ikiwa bado ameshikilia lake inabidi utafute Shaykh ambaye anamsikiliza ili amwelezee kuhusu hilo.

3.    Ni kumchukua mtoto mwenyewe ukaondoa ushirikina kwa kwenda kumtahiri.

4.  Ikiwa hukufanikiwa katika kumrekebisha katika ushirikina wake huo itabidi uende kwa Qaadhi ili umshitakie mumeo kuhusu hayo. Na katika hilo ni kutaka talaka ikiwa bado ataendelea na ushirikina wake kwani haifai kwako Muislamu mzuri kukaa na mume kama huyo.

5.   Juhudi yako yote hiyo utapata thawabu kutoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) hata kama hukufanikiwa.

 

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Akusaidie katika hilo na Akufanikishie hilo.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share