Skip navigation.
Home kabah

Kuchukua Mkopo Katika Benki Za Riba Ikiwa Hakuna Benki Za Kiislamu Inafaa?

SWALI LA KWANZA:

 

MIMI NAISHI SKANDINAVIA NINA SWALI. KUHUSU RIBA NI HIVI HUKU SKANDINAVI BENKI ZA HUKU HUKOPA WATU PESA KAMA 3000 ALAFU WANATAKA URUDISHE 3300 SASA. HII PIA UKIKOPA NI RIBA HATA KAMA UNAMATATIZO. HUNA ELA HAKUNA MTU WA KUKUKOPA. UKIKOPA HAPO BENKI NI HARAM.

 

 

 

SWALI LA PILI:

 

Asalam aleykum mi nauliza kama nimekopa gari bank na nalipa pamoja na riba je inafaa kwa mwislam kukopa bank? Je na kama hakuna taasisi ya kukopa bila riba tufanyeje naomba msaada kwa hilo


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu kuchukua mkopo wa riba. Mkopo wowote unaokopa na kulipa juu yake ziada ni riba kisheria na haifai kwa Muislamu kuchukua mkopo aina hiyo. Nchi za Scandinavia zinajulikana kuwa na Waislamu wengi kwa wakati huu wa sasa. Unalohitajia kufanya kwa sasa ni kujaribu kutafuta markaz (centre) na uwe na ndugu zako kwa hali na mali katika kufanya mambo ya Kiislamu.

 

Hata hivyo, sheria ya Kiislamu inamuangalia kila mmoja na tatizo alilo nalo. Ikiwa hali yenyewe ya hilo tatizo ni mas-ala ya uhai na kifo basi unaruhusiwa kuchukua mkopo wa riba kutoka kwa benki baada ya kufanya juhudi ya kutafuta mkopo usiokuwa na riba. Ikiwa juhudi zako zimeruka patupu hapo utaruhusiwa kwa ajili ya kuokoa maisha na huku unachukukia sana. Suala hilo ni kama mfano wako kuwa katika sehemu ambayo hakuna chakula kabisa nawe uko katika hali ya kushurutishwa kula nguruwe kwani hakuna chakula kingine isipokuwa nguruwe. Wakati huo utakula nguruwe kwa kiasi cha kuokoa maisha yako.

 

Lakini haya matatizo tuliyo nayo kama kutaka kununua nyumba, gari au vitu vingine ambazo kuzikosa hazitakupelekea wewe kuwa katika hali ya kukaribia kifo Uislamu umekataa kabisa mkopo wa aina hiyo.

 

Wengi wanaochukua mkopo wa benki si wenye kuwa na shida ya uhai na kifo, huchukua kwa mahitaji yao ya ziada ya kilimwengu kama tulivyoona hapo kuhusu kuchukua gari kwa mkopo na kulipa riba, au kuchukua nyumba za za mkopo kwa kulipa kidogo kidogo kwa miaka mingi ambazo ni mogeji (mortgage) na mahitaji mengineyo ya zaida ya kidunia.

 

Kwa hiyo, mikopo yoyote ya aina hiyo haifai kabisa kisheria. Na tumuogope sana Allaah kwa kuingia kwenye ribaa ambayo madhambi yake ni makubwa na adhabu zake ni kali mno.

 

Hakika ni kuwa Allaah Aliyetukuka Ametangaza vita na yeyote anayechukua riba pale Aliposema:

Enyi mlioamini! Mcheni Allaah, na acheni riba zilizobakia, ikiwa nyinyi ni Waumini. Basi mkitofanya jitangazieni vita na Allaah na Mtume wake. Na mkitubu, basi haki yenu ni rasilmali zenu. Msidhulumu wala msidhulumiwe” (Al-Baqarah: 278-279).

 

 

Na Allaah Anajua zaidi