008-Hakimu Wa Kiislamu: Sura Ya Pili

 

SURA YA PILI

 

UFUNGUZI WA KESI

 

 

Nani Anayeweza Kudai?

 

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anatueleza kuwa mtoto kabla kubaleghe, mtu aliye kwenye usingizi na mwenda wazimu hawaandikiwi dhambi. Hivyo hawawezi kwa nafsi zao kuingia kwenye masuala ya mikataba au ufunguzi wa kesi au kudaiwa.

Mtoto mdogo na yule asiyekuwa na akili, hawawezi kufungua kesi bila ya kusimamiwa na mlezi au msimamizi. Mada hii imeelezwa vyema na wanachuoni tofauti.

 

Dai linaweza tu kufunguliwa na mtu mwenye akili timamu. Hivyo, dai la mtoto au mwendawazimu halitosikilizwa isipokuwa kupitia kwa mlezi, wala shauri halitosikilizwa dhidi yake bila ya kuwa na mwakilishi.

 

Sheria inaruhusu kuwepo msimamizi wa mtoto na mwenda wazimu. Kesi yoyote ya mtoto mdogo itafunguliwa kwa jina lake lakini itasimamiwa na mlezi wake.[1] Mahkama itakaporidhika kwamba mdaiwa ni mtoto mdogo au mwenda wazimu, wala hana mtu wa kuisimamia kesi yake, itateuwa mtu anayefaa kuwa ni wakala wake.[2] Hata hivyo, msimamizi huyo ni lazima awe ni mwenye umri wa mtu mzima na wala asiwe na nia mbaya juu ya usimamizi wake.[3]

 

 

Uteuzi Wa Mahkama Inayofaa

 

Mtu ambaye anataka dai lake lisikilizwe, kwanza kabisa ateue Mahkama inayofaa, ile ambayo ina nguvu ya Kisheria kusikiliza lalamiko hilo. Uteuzi wa Mahkama inayofaa ni jambo jepesi chini ya mfumo wa Kiislamu.

 

Isipokuwa kwa sasa, nguvu za Kisheria za Hakimu fulani zitakuwa zimebanwa kulingana na amri ya uteuzi wake ambapo amepatiwa aina fulani tu za kesi anazozitolea hukumu. Mdai anawajibika kupeleka maombi yake kwenye Mahkama ambayo mipaka yake ya kisheria anaishi yeye na mdaiwa wake. Na haitoleta tofauti yoyote kwenye sehemu hii kuhusu kiini kikuu cha madai.

 

Kwa mfano, ardhi ipo sehemu nyengine au mtu ambaye amedaiwa anaishi kwenye nguvu za Kisheria za Hakimu mwengine. Zote kwa pamoja, zitakuwa na nguvu sawa sawa mbele ya Mahkama. Kitakachotofautiana ni thamani ya ardhi hiyo.

 

Kesi yoyote kwa mujibu wa Sheria itafunguliwa kwenye Mahkama yenye mamlaka ya kuisikiliza. Madai hayo ni lazima yawe ndani ya mipaka ya Mahkama hiyo.[4] Pale ambapo dai ni la thamani ya kitu kisichohamishika kama vile ardhi iliyopo kwenye mamlaka ya Mahkama nyengine, inaruhusika kufungua kesi hiyo kwenye Mahkama yoyote yenye mamlaka ya kusikiliza madai ya ardhi kama hiyo.[5] Inapotokezea hitilafu ya eneo la ardhi iwapo lipo ndani ya mamlaka ya Mahkama Y au Mahkama X. Moja kati ya Mahkama hizo, itaweka kumbukumbu ya maelezo hayo na kuisikiliza kesi hiyo kama vile imo ndani ya mamlaka yake. Pingamizi ya kwamba Mahkama haikuweka kumbukumbu hiyo itatupiliwa mbali na Mahkama ya juu pale itakapokatiwa rufaa ikiwa tu Mahkama hiyo iliendelea kusikiliza kesi hiyo kwa lengo la kutenda haki na uadilifu. [6]

 

 

 

Dai Lazima Litimize Kanuni Zake

 

Al-Mawardi anajishughulisha na mada hiyo kwenye kitabu maalum chenye jina la Sayr ad-Dalawa-Safari - Kuhusu Mwenendo Wa Kesi. Kwa mujibu wa al-Mawardi na Ibn Qudaamah, madai ni lazima yawe kwa maandishi[7].

 

Wakati wa kipindi cha Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Makhalifa waongofu, madai mengi yakitolewa hukumu kwa njia ya mdomo na amri kupitishwa bila ya shaka kwa mdomo. Siku zilivyoenda mbele na kufanya maandiko kuwa rahisi, wanachuoni wakapendekeza kwamba madai na hukumu zake ziwe kwa maandishi.

 

Hata hivyo, ni vizuri kufafanua kwamba Qur-aan tukufu inatilia mkazo zaidi kufanya shughuli zenye mnasaba wa amana kama vile mikataba (na madai) kwa njia ya maandishi, Qur-aan inasema:

 

{{Enyi mlioamini! Mnapokopeshana deni kwa muda uliowekwa, basi iandikeni…}} [2: 282]

 

Kwa kutumia Aayah hiyo, ni usalama zaidi kufanya madai hata katika kuitoa hukumu kwa maandishi.

 

Kuna kanuni nyengine kadhaa ambazo dai ni lazima litimize. Kwa mfano, mtu mmoja au walio wengi dhidi ya yule anayependekezwa au wanaopendekezwa (kudaiwa) a/watambulike. Kitu hicho au hali inayodaiwa ni lazima pia iwekwe wazi na sifa zake zilizokuwa wazi. Kwa mfano, kama ni ardhi, aeleze namna alivyoipata, mipaka yake ni lazima iwekwe wazi ijapokuwa thamani yake haina haja ya kutajwa. Kama dai linahusika na deni, ni lazima aeleze namna lilivyopatikana deni hilo, aeleze kama ni aina ya pesa iliyoazimwa, pesa iliyonunuliwa au mshahara, na nyenginezo na pia thamani yake iwekwe wazi.

 

Kinachodaiwa kiwe kinawezekana kudaiwa, ili kwamba ikiwa haiwezekani kwa mujibu wa uzoefu na hukumu zetu, dai hilo litupwe. Kwa mfano, X anaonesha kuwa na umri wa miaka 35, lakini anadai kuwa ni mkubwa kuliko Y ambaye ni mzee anayefika miaka 60. Au B anayedai C kuwa ni mwanawe, ilhali yatambulika kwa uwazi kuwa C ni mtoto wa A.

 

Maelezo ya madai kama si ya ulinganifu (kigeugeu) na hayana muelekeo wa kutendeka haki yatakataliwa. Kwa mfano, X amekwenda dukani kununua bidhaa, kabla ya kuinunua anadai ni ya kwake. Hapa X atakuwa hana haki ya kudai kutouziwa bidhaa hiyo, kwani hajaenda kununua ila amedai bidhaa isiyo na uhakika wa milki ya X. Lakini, hata hivyo, kama madai ya mdai yatarekebishwa na kueleweka, madai yake yatahitaji kusikilizwa na pingamizi ya kukosekana muelekeo wa kesi haitakuwa na mashiko kwasababu madai yameshafanyiwa marekebisho.

 

Madai yaweza kuwa kwa matamshi au kwa maandishi. Kama ni matamshi, Mahkama itawajibika kuyawekea kumbukumbu.

 

Madai pia ni lazima yaweke wazi vizuri kiini cha madai dhidi ya yule mtu anayedaiwa, inaweza kujaribiwa kwa aidha, kama mtu huyo atakubali tuhuma za madai, ambapo maamuzi yatatolewa dhidi yake. Kama mdaiwa atakana madai hayo, kesi itaendelea dhidi yake kama ni mshindani (khaswm) wa mdai, na mdaiwa ataitwa kuja kujibu hoja. Jaalia, mdai anatamka kwamba wakala wa mdaiwa amenunua bidhaa fulani kutoka kwake, na anadai malipo, lakini mdaiwa anakana dai hilo, mdaiwa atatambulika kuwa ni mshindani na kesi itaendelea dhidi yake. Kwa upande mwengine, kama mdai kiurahisi tu atatuhumu kwamba wakala wa mdaiwa hakulipa malipo na mdaiwa akakataa dai, kesi haitosimama na wala haitasikilizwa kama yalivyo madai ya mdai kwani hayajaweka wazi kiini cha madai dhidi ya mdaiwa. Kwa mfano, mdai ameshindwa kuonesha namna na sababu gani anayostahiki kulipwa malipo kutoka kwa mdaiwa.

 

Hivyo, ni lazima madai yawe na maelezo yote muhimu kuhusiana na kinachodaiwa kwenye kesi pamoja na sababu ya kudai hicho kinachodaiwa na maombi ambayo Mahkama itatakiwa itolee hukumu.

 

Mwandishi wa kitabu cha al-Hidayah anashauri kwamba: pale inapotokezea kwamba kitu kinachodaiwa hakipo na wala hakijulikani, basi madai yatawajibika kutupwa, kwani hayana maelezo ya kinachodaiwa[8].

 

Ibn Farhuun anaweka vipengele vitano vya madai:

 

1)    Kinachodaiwa kijulikane.

2)    Kama mdaiwa atakubali ukweli wa madai, kitulizo (relief) kitolewe.

3)    Madai yasiwe ya uchokozi (madai ya uongo).

4)    Madai yaletwe yakiwa na sababu maalum.

5)    Madai yawe na sababu nzuri ambayo hayatokataa ukweli wake[9].

 

Mwandishi wa al-Hidayah anaendelea kueleza kwamba ikiwa ni kesi ya kitu kinachoweza kuhamishika, basi ni lazima kiletwe Mahkamani (kama inawezekana), ili kiwekwe wazi na kutambuliwa. Kama hakiwezekani kielezwe ukubwa wake, thamani, jinsia, aina na sifa yake zote zielezwe.

 

Kwa kitu kisichohamishika, maelezo ya kina ya mipaka pamoja na watu, unganisha na maelezo ya wanafamilia, namna ya mipaka na walio jirani watajwe. Inatosha kama ni mipaka mitatu tu ya kesi ya ardhi itatajwa, kwa mujibu wa wanachuoni wengi wa wafuasi wa Abu Haniyfah[10]. Wanachuoni wengine kama Ibn Qudaamah na al-Mawardi, wana mtazamo kwamba mipaka yote minne itajwe[11].

 

Sheria kwa upande wake inaeleza kuwa dai ni lazima lipelekwe Mahkamani ama kwa mdomo au maandishi likiwa na maelezo yaliyo wazi ya dai hilo.[12] Madai hayo yawe na kiini chake.[13] Pale mdai anapoegemeza madai yake kwa hoja ya kutenzwa nguvu, makosa ya makusudi, uongo n.k. itamwajibikia kuyaeleza ndani ya madai (pamoja na tarehe kama inahitajika).[14] Baada ya kufunguliwa kesi na kuanza kusikilizwa, madai hayataruhusika kuibua hoja mpya ya dai au kuingiza madai mengine yasiyoendana pamoja na madai yaliyofunguliwa hapo mwanzo.[15] Hata hivyo, Hakimu ana uwezo wa kuamrisha kuondoshwa baadhi ya vifungu vilivyomo ndani ya madai ikiwa anaamini kuwa kubakia kwake vitaifanya Mahkama kutotenda haki na uadilifu au kupelekea kwenye sakata lisilo na msingi.[16]

 

Vifungu vifuatavyo ni lazima vitimizwe ndani ya madai:

 

(a)             jina la Mahkama ambayo dai linapelekwa,

(b)             jina na anwani ya mdai,

(c)             jina na anwani ya mdaiwa,

(d)             kama mdaiwa ni mtoto au mwenda wazimu, ielezwe,

(e)             hoja za kufungua kesi na lini liliibuka,

(f)               hoja za kuonesha kwamba Mahkama inayo mamlaka,

(g)             kitulizo anachodai mdai,

(h)             kama mdai amesamehe kiwango cha dai, ielezwe,

(i)                thamani ya kinachodaiwa kwa mnasaba wa mamlaka na malipo ya Mahkama, yaelezwe.[17]

 

Pale dai linapohusu malipo ya fedha taslim, ni lazima dai lieleze idadi halisi ya fedha inayodaiwa.[18] Na kama ikiwa ni fedha iliyokopeshwa, dai pia liweke wazi maelezo yote yanayohusiana na mkopo huo. Kwa mfano, tarehe ya mkataba, tarehe iliyotakiwa kulipwa, fedha iliyolipwa na iliyokuwa bado (kama ipo).[19] Ama ikiwa ni dai la kitu kisichohamishika kama vile ardhi, dai ni lazima lieleze mipaka ya ardhi hiyo pamoja na nambari za kumbukumbu ya upimaji.[20]

 

 

Kuunganisha Kwa Pande Za Watu

 

Inaweza kutokea kwamba watu wawili au zaidi wamehusika kwenye kuvunja Shari'ah, au wana faida fulani katika kukataa haki ya mdai, wengine ni wengi zaidi kuliko wengine au wote kwa nguvu moja, au zaidi ya mtu mmoja ana faida katika kuanzisha dai. Hapo, suala muhimu linakuja katika uteuzi wa watu na Shari'ah inaweka wazi kanuni kwa lengo la uteuzi huo. Kwa mfano, pale dai linapofanywa kwa madhumuni ya bidhaa mahsusi, yule mtu ambaye anayo milki nayo afanywe kuwa mdaiwa peke yake.

 

Hivyo, kama A amechukua milki ya farasi visivyo halali anayemilikiwa kihalali na B na kumuuza kwa C na B anamtaka farasi wake, B anaweza kumfungulia kesi A na C kwa pamoja, ingawa A ndiye aliyechukua lakini kwa sasa C ndie mwenye milki ya mnyama. Yule mtu ambaye anayo milki, atalazimika kumfungulia kesi mchuuzi wake kwa kurudishiwa thamani aliolipa. Mifano  mengine ni mdhaminiwa aliyeajiriwa, mtu aliyekuwa na nguvu ya kutumia kifaa, na mpangaji, pale mali iliyokuwa kwenye mamlaka yao imechukuliwa visivyo halali na mwengine, wanaweza kumfungulia kesi aliyefanya kosa kwa kurudisha kifaa bila ya kumfanya mmiliki (mfano mdhamini au mpangishaj) kuwa ni upande wa kesi.

 

Kwenye masuala ya mali ya aliyefariki, kanuni ya jumla ni kwamba, mmoja kati ya warithi anaweza kuwa ni mdai au mdaiwa kwa mnasaba wa madai ambayo yanaweza kufanywa kwa niaba au dhidi ya aliyefariki. Isipokuwa pale ambapo dai hilo ni kurudishwa kwa mali maalum kutoka kwa milki ya aliyefariki, ambapo mdaiwa anayefaa ni mtu mwenye kuwa nayo hiyo mali na mrithi asiyekuwa nayo hiyo mali hawezi kufanywa kuwa ni mdaiwa.

 

Ni hivyo hivyo kwa kesi ya kukubali kuwa mrithi, au kuhodhi mali ya aliyefariki, au kuwazuia warithi wengine. Mmoja kati ya warithi atakuwa na nguvu ya kufungua kesi kwa niaba yaaliyefariki kwa kitu ambacho kilikuwa ni haki yake aliyefariki kutoka kwa mdaiwa, kwa muundo wa deni au mfano wa hiyo haki au wajibu kwa aliyefariki kutoka kwa mdaiwa. Kama dai litatimizwa, maamuzi yatatolewa kwa mali anayostahiki kwa faida ya warithi wote. Mdai yeye mwenyewe, hata hivyo, ataruhusika kuitambua sehemu yake ya urithi.

 

Mfano: Kama X ana dai la pesa dhidi ya mali iliyoachwa na aliyefariki Y, anaweza kuthibitisha dai lake mbele ya warithi A, B au C (mmoja tu kati ya warithi). Ikiwa kama X amehodhi (ameitia mkononi) au hahodhi (hajaitia mkononi) sehemu yoyote ya mali ya aliyefariki Y. Ingawa kukubali kwa mmoja kati ya hao warithi kwamba X anahodhi au hahodhi mali ya aliyefariki Y, hakutowafunga warithi wengine wasidaiwe na X. Kama mmoja kati ya A, B au C hatokubali dai, na X atathibitisha dai lake mbele ya A, B au C, maamuzi yatapitishwa dhidi ya warithi wote na warithi wengine hawatolazimika kumtaka X kuthibitisha dai lake dhidi yao kwa mnasaba wa sehemu ya urithi wao. Hata hivyo, wapo wazi (A, B au C) kukubaliana na maamuzi hayo kwa maombi ya kujitoa kwenye madai (ili wawe na kesi tofauti).

 

Wenye hisa wanapokuwa wengi katika mali mahsusi lakini sio kwa haki ya kurithi, mmoja kati ya wenye hisa hawezi kuwakilisha wengine kama ni mdaiwa katika kesi kwa mnasaba wa mali hiyo, lakini kama atalalamikiwa na kufunguliwa kesi peke yake, maamuzi yaweza kutolewa dhidi yake kwa kiwango cha hisa zake.

 

Mwananchi wa eneo anaweza kufungua kesi kwa mali au suala lenye manufaa ya jamii nzima kama vile bughudha za walevi zinazotokana na klabu inayopigisha miziki usiku kucha (public nuisance); na maamuzi kumpendelea yeye yatatolewa kwa manufaa ya wananchi wote wa eneo hilo. Kwenye kesi kuhusiana na kitu chenye manufaa ya jamii ambacho kinatumiwa na watu wa vijiji viwili, kama vile mkondo au kisima, inatosha kwa baadhi ya watu wa kila kijiji kuwa ni wahusika, isipokuwa pale Mahkama itakapoweka idadi maalum ya watu. Idadi inapozidi mia moja, inatambulika ya kwamba hakuna kizuizi.[21]

 

Sheria inaeleza kwamba kuunganishwa kwa pande za wadai tofauti inawezekana ndani ya kesi moja. Kesi ambayo haki au fidia kwa mnasaba wa tendo au makubaliano yamefanywa, ikiwa kwa pamoja, au mmoja mmoja.[22]

 

Masharti muhimu ambayo yameeleza kwamba ni lazima yathibiti yamo ndani ya kesi ya Stroud dhidi ya Lawson[23], ambayo Mahkama iliamuru:

 

"Inatosha kwamba masharti haya yatimizwe, ni kusema kwamba, haki ya kitulizo (relief) inayodaiwa kuwepo kwa kila mdai iwe kwa mnasaba kwamba imetokana na mauziano hayo hayo, na pia kwamba kuwe na hoja moja ya msingi, ili kwamba kesi iwe ndani ya kanuni hiyo hiyo."

 

Mdai anaweza kuunganisha wadaiwa kwa kufuata masharti maalum yaliyoelezwa hapo juu.[24] Hata hivyo Hakimu anayo nguvu ya kumtoa mdai au mdaiwa yeyote iwapo ni kwamba huenda kuunganishwa huko kutaishushia heshima pande nyengine.[25]

 

 

Utaratibu Pale Mdaiwa Anapoishi Nje Ya Mpaka

 

Kwa mujibu wa hukumu za jumla katika Shari’ah zinazopatikana kwa kufananisha (al-Qiyaas), maamuzi ya Hakimu yanamfunga mdaiwa ambaye anaishi ndani ya mipaka yake. Lakini kwa mujibu wa hiari ya wanachuoni ambao wanakubaliana na Maswahaba na warithi wao na inaegemezwa kwenye dharura, kama mdaiwa yupo ndani ya mipaka ya Hakimu mwengine, mdai anaweza kufungua kesi yake katika Mahkama ndani ya mipaka hiyo anayoishi na mashahidi wake wanapatikana.[26] Hakimu ambaye kesi imefunguliwa katika Mahkama yake, anaweza kuweka kumbukumbu ya ushahidi na halikadhalika kutoa amri yake ikiangaliwa kwamba mdaiwa aliyeshindwa kufika aidha ameteua wakala kumwakilisha yeye au Mahkama yenyewe imeteua mtu kuangalia faida yake.

 

Lakini usahihi wa uteuzi wa Mahkama wa wakala, kwa ajili ya mdaiwa kwa kesi kama hiyo haionekani kuwa haina mashaka. Kama ushahidi uliotolewa na mdai huthibitisha kesi yake, Mahkama inaweza kuweka kumbukumbu kwa yale iliyoyaona na kutoa hukumu na baada ya mali kuizuia na kudhibiti kumbukumbu mbele ya mashahidi wawili kwa Hakimu ambaye ndani ya mipaka yake, mdaiwa anaweza kupatikana. Kama mdaiwa asiyehudhuria hajawakilishwa na wakala wake, Mahkama ambayo imefunguliwa kesi, inaweza kama ikichagua kufanya hivyo, kuweka kumbukumbu wa ushahidi na kuupeleka kwa Hakimu wa sehemu ambayo mdaiwa anaishi, kwa minajili ya Hakimu huyo kupitisha amri hiyo mbele ya mdaiwa.

 

Mienendo hii inaruhusiwa kwa kesi tu zinazohusiana na kutoa haki binafsi, kama vile kurudisha deni, kuthibitisha ndoa au uzazi (mfano mtoto A ni wa mzazi B), kurudisha mali isiyohaulishika (non transferable) na mfano wa hayo na sio kwenye masuala ya hadd (jinai) na kulipiza kisasi.

 

Ama kwa upande wa Sheria inaeleza kwamba hati ya madai inaweza kupelekwa kwa mdaiwa ikiwa yupo au hayupo ndani ya mipaka ya Mahkama iliyoitoa hiyo hati. Hati hivyo itapelekwa kwenye mipaka ya Mahkama ambayo mdaiwa anaishi na Mahkama hiyo itaifanyia kazi kama vile imeitoa binafsi. Baadaye itaweka kumbukumbu pamoja na mwenendo wowote uliotumia na kuirudisha Mahkama iliyoitoa.[27]

 

 

[1] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XXXVI, r. 1.

[2] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XXXVI, r. 3 (1).

[3] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. XXXVI, r. 4 (1).

[4] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 10 – 11.

[5] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 12.

[6] Sheria ya Mwenendo wa Madai, S. 13

[7] (a) al-Mawardi; Adaab Al-Qaadhi, II, uk. 330-355 (b) Ibn Qudamah, Akhbaar Al-Qudhaat, IX, uk. 84.

[8] Al-Marghinani; Al-Hidayah, II, uk. 201.

[9] Ibn Farhuun, Tasbirah, I. uk. 86-88.

[10] Al-Murghinani; Al-Hidayah; II, uk. 201-202.

[11] (a) Ibn Qudamah; Akhbaar Al-Qudat, IX, uk. 85-86 (b) Al-Mawardi; Adab Al-Qaadhi, II, uk. 330.

[12] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. IV, r. 1.

[13] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VI, r. 2.

[14] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VI, r. 4.

[15] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VI, r. 7.

[16] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VII, r. 16.

[17] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VII, r. 1.

[18] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VII, r. 2.

[19] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VII, r. 3.

[20] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. VII, r. 4.

[21] Al-Majallah, uk. 277-278.

[22] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. I, r. 1

[23] Stroud V. Lawson, (1898) W Q. B. 44, uk. 52.

[24] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. 1, R. 3 na 5.

[25] Angalia kesi ya The Bank of India V. Shah, (1965) E. A. 18.

[26] Al-Hidayah, Juzuu ya VI, uk. 381-390.

[27] Sheria ya Mwenendo wa Madai, O. V, r. 21-22

 

Share