Mume Hataki Kuswali, Haogi Janaba, Mke Mjamzito Anataka Kuachika Aolewe Na Mume Mwengine Afanyeje Kuhusu Mimba Yake?

SWALI:

 

Assalam alaykum warahmatullah wabarakatuh, baada ya salam ya Allah, kwanza ningepeda kuwapongeza kwa kazi ambayo mnaifanya Allah awajalieni wepesi na awalipe pepo, amin; nina dadayangu ameniuliza swali nikaona niwafikishie mnisaidie kwa uwezo wake Allah, swali lenyewe linahusu ndoa yake, ana muda wa myaka sita katika ndoa yake ila imejawa na mitihani mingi moja wapo ni kwamba mme wake tangu amuoe hataki kusali japokua ni mtoto wa Kiislam na wala hakokagi janaba kwa wakati wake ila mpaka sasa wana watoto 3, tatizo analo ni kwamba alikua anataka kutoka kwenye ujumba ila ana mimba ya miezi mitatu na anategemea kuolewa na ungine mwanamme sasa mpaka sasa hajui afanye nini kuhusu iyo mimba na uyo mchumba wake mpya maana m'me wake amebaki ni m'me wa shida za ndoa tu tofauti na ilo tendo la ndoa mara nyingi hua hawaongei amejitahidi kumlingania amechoka; anauliza je afanye nini?


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu mume asiyeswali na mwenye matatizo.

 

Hakika matatizo ya ndoa yamekuwa sugu katika jamii yetu na ikiwa hatutabadilika kwa kurudi katika Uislamu basi haya matatizo yatabaki nasi kwa muda mrefu sana kutoka sasa. Mara zote wenye kupata matatizo katika unyumba ni wanawake ambao huwa ndio rahisi kuingia katika ndoa bila ya kutazama maagizo yaliyoachwa na Uislamu ambayo yangewasaidia kwa kiasi kikubwa.

 

Inashangaza sana kuona kuwa huyo dada yako kwa muda wa miaka sita ameendelea kuishi na mume asiyeswali wala kuoga janaba na akakaa naye muda wote huo na sasa ndio analalamikia tabia hizo za maasi ya mume! Isije ikawa baada ya yeye kupata mwanaume nje ya ndoa na kuwa na mahusiano naye, sasa ndio imekuwa anataja maovu ya mume wake na kutaka kuachwa, hali hii inatia wasiwasi na kama anafanya hivyo kutaka kuachika kwa sababu ya mwanaume mwengine na si kwa sababu ya matatizo ya dini ya mume wake ambayo kama ni kweli yamedumu kwa muda wa miaka yote hiyo akayanyamazia hadi leo, basi hili litakuwa ni kosa kubwa kwa huyo dada yako. Na atapata madhambi makubwa ikiwa anayosema si kweli, au ni kweli lakini hakuona ni tatizo miaka yote hiyo hadi baada ya kupata mwanaume nje ya ndoa.

 

Mwanzo inatakiwa umpatie nasaha dada yako asiingie katika madhambi hayo ya kuwa na mahusiano na mwanamme mwengine hali ya kuwa yeye bado ni mke wa mtu. Itakuwaje yeye analalamika kuhusu maasi ya mume wake ya kuacha kuswali, kisha na yeye anataka kutumbukia katika maasi mengine makubwa?

 

Kutoswali ni dhambi kubwa na pia kuzini na hasa akiwa bado ni mke wa mtu. Dada yako bado ni mke na inabidi hiyo ndoa mwanzo ivunjike kwa kupatiwa talaka au kwenda kuomba talaka kwa Qaadhi kwa kuwa mume wake haswali na hiyo ni haki yake. Pia haifai kwake kuitoa mimba kwani hilo ni dhambi jingine tena kubwa la kuua kiumbe aliye hai. Pia ni kosa kwake kuanza shughuli za kuwasiliana na mwanamme asiyemuhusu ambalo pia ni madhambi na ni njia ya zinaa.

 

Anachotakiwa kufanya dada yako ni kujaribu kujivua katika ndoa na mume wake, ima kwa kuzungumza naye ajirekebishe au amuache. Na ikiwa amekataa basi anaweza kumuona Qaadhi ili aiamulie ndoa yake. Akishapata talaka itabidi akae mpaka azae mtoto, baada ya hapo ndio anaweza kuolewa na mume mwengine. Hata hivyo, inatakiwa umpatie nasaha asiingie katika makosa aliyoyafanya kabla ya kuingia katika ndoa ya kwanza kwa kurudia kufanya kosa kama hilo la kukubali kuolewa na mwanamme bila kumchunguza au kuhakikisha uzuri wa dini yake na maadili na tabia.

 

Ama kulingania haifai kuchoka kwani hujui huenda kuwa amemuathiri kwa kiasi fulani japokuwa yeye haoni. Anatakiwa kuswali Swalah ya Istikhaarah kabla ya kuchukua uamuzi wa aina yoyote ile.

 

Tunamtakia kila la kheri katika harakati zake hizo.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

 

Share