Zingatio: Toa Swadaqah Kwa Ajili Ya Allaah

 

Zingatio: Toa Swadaqah Kwa Ajili Ya Allaah

 

Naaswir Haamid

 

 

Alhidaaya.com

 

 

Ihsaan ni kinyume cha ufisadi, na miongoni mwa Ihsaan ni kufanya wema bila ya kujali mipaka ya Kaskazi wala Kusi, na kutoa kwa ajili ya Allaah ni wema na Ihsaan kwa mwanaadamu.

 

Hakuna shaka yoyote kwamba Swadaqah ni katika tabia njema, na iwapo tutafungua kurasa za Siyrah za wema waliotangulia, tutaona kwamba walikuwa wakikithiri mno kwenye kutoa Swadaqah. Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Anasema:

خُذْ مِنْ أَمْوَالِهِمْ صَدَقَةً تُطَهِّرُهُمْ وَتُزَكِّيهِم بِهَا

Chukua (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم) katika mali zao Swadaqah, uwatakase na ziwazidishie kwazo.. [At-Tawbah: 103]

 

Kupitia Tamko hilo hapo juu, tunafahamu kwamba kumbe kuisafisha nafsi kutokana na takataka za upungufu na kuiinua jamii mpaka kuifikisha kwenye daraja tukufu kabisa, ndio hekima ya juu. Ni kwa ajili hii ndio Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipanua wigo katika kuelezea maana ya neno “Swadaqah” ambayo Muislamu anatakiwa kuitoa, akasema:

 

"Tabasamu lako usoni kwa nduguyo (Muislamu mwenzio) ni Swadaqah, kuamrisha kwako mema na kukataza kwako maovu ni Swadaqah. Na kumuongoza kwako njia mtu katika ardhi (nchi) ya upotevu, hilo kwako ni Swadaqah. Na kuondosha kwako njiani udhia, mwiba na mfupa, hilo kwako (nalo) ni Swadaqah. Na kumtekea kwako maji nduguyo, kwako ni Swadaqah na kumsaidia kwako mtu dhaifu wa uoni kuongoza njia, (hilo nalo) kwako ni Swadaqah". [Al-Bukhaariy]

 

Swadaqah huanza kwa kuuzoesha mkono kutoa kila mara bila ya kinyongo wala manuuniko. Mkono una dhima kuu ya kukulingania kutoa Swadaqah katika vile ulivyoruzukiwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) kama Alivyosema:

 

فَأَمَّا مَنْ أَعْطَىٰ وَاتَّقَىٰ ﴿٥﴾ وَصَدَّقَ بِالْحُسْنَىٰ ﴿٦﴾ فَسَنُيَسِّرُهُ لِلْيُسْرَىٰ ﴿٧﴾

 Basi yule anayetoa (mali) na akamcha Allaah. Na akasadikisha Al-Husnaa (Jazaa na Kalimah ya laa ilaaha illa Allaah).  Basi Tutamuwepesishia kwa yaliyo mepesi. [Al-Layl: 5-7]

 

Hiyo ndio faida na jazaa ya aliyeutumia vyema mkono wake katika kutoa Swadaqah. Akautumia mkono wake katika kutoa vile Alivyoruzukiwa na Allaah Ar-Razzaaq, katika kuisadia jamii na kuupeleka mbele Uislamu.

 

Ni vyema ukakumbuka kwamba kutoa katika mambo ya khayr ni katika kuishukuru neema ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa). Ambako hakumaanishi ila kuzidishiwa neema, tusome kwa mazingatio:  

وَإِذْ تَأَذَّنَ رَبُّكُمْ لَئِن شَكَرْتُمْ لَأَزِيدَنَّكُمْ ۖ وَلَئِن كَفَرْتُمْ إِنَّ عَذَابِي لَشَدِيدٌ﴿٧﴾

 Na pindi Alipotangaza Rabb wenu: Ikiwa mtashukuru, bila shaka Nitakuzidishieni (neema Zangu); na mkikufuru, basi hakika adhabu Yangu ni kali. [Ibraahiym: 7]

 

"Mtenda wema hutendea nafsi yake na mtenda ovu humrejea mwenyewe". Hivyo elewa kamba kuishukuru neema kikweli kweli na kuitumia vile inavyostahiki sio tu kusema au kuandika kwenye milango kwa mbwembwe: ‘AlhamduliLlaah’ au ‘Hadha Min Fadhli Rabiy! Na ni ubaya ulioje kuzitumia neema hizi kinyume na vile Alivyoamrisha Ar-Razzaaq.

 

 

Share