014-Hakimu Wa Kiislamu: Sura Ya Nane

 

SURA YA NANE

 

HITIMISHO

 

 

Maelezo yote haya, ingawa yamekusanywa kwa juhudi kubwa kutoka kwenye vyanzo mbali mbali, yanaonesha ukweli ya kwamba muundo na utaratibu wa Kishari’ah siku za mwanzo za Uislamu haukuwa mwepesi kama wengi wanavyofikiria. Hapana shaka, haukuwa utaratibu wenye mazonge yanayohusisha mbinu nyingi za kitaalamu zisizosaidia kitu kusuluhisha matatizo. Hata hivyo, ukosefu wa maelezo kamili na ya moja kwa moja ni miongoni mwa matatizo ya wanahistoria na wanachuoni wetu.

 

Siku za leo, kuna mawazo mengi kwamba maelezo hayo ndani ya Shari’ah, khasa mwenendo wa Mahkama, zinachukuliwa na kuazimwa kutoka sheria ya Kirama na sheria za Sasanide.[1] Pia inasemwa kwamba Hadiyth zinatungwa ili kuzifanya hizo kanuni zilizoazimwa ziwe za Kiislamu. Lakini wanachuoni wa Kiislamu wanatetea kwamba Hadiyth hizo ni sahihi, na ni maneno hasa ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) yaliyofikishwa kwa uangalifu wa hali ya juu kutoka kwa wasomi na wacha Mungu.

 

Tukiachilia mbali mgongano huu, ambao ni nje ya kazi hii, sasa tugeukia kwenye mada ambayo Uislamu ni msingi wa maisha na sio msingi wa mwenendo wa kesi. Uislamu mara zote unatoa mwangaza ili wafuasi wake wabakie ndani ya mhimili sahihi wa mafunzo ya Kiislamu. Uislamu, tokea mwanzo, pamoja na hitilafu tulizonazo, unatufunza kuwa na mwenendo maalumu wa maisha, kuweka mbele umoja.

 

Kutumia njia za kisasa na mitindo mipya ya kazi hakika ni tendo la Kiislamu. Kama Waislamu wa leo wanapigana kwa kutumia bunduki, sayansi na teknolojia, basi wasizuiliwe kwenda kinyume na waliowatangulia ambao walipigana kwa silaha na mapanga. Kupigana sehemu iliyo wazi ulikuwa ni mtindo wa Waarabu lakini pale Salmaan al-Faarisiy alipotoa wazo la kwamba handaki lichimbwe, ambalo ni mtindo wa vita vya Wafursi, Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alilikubali kwa vile ilikuwa ni njia bora ya kushinda vita hivyo. Na ni nani aliyesema kwamba yote ni makosa kwa Wakristo, Wayahudi, Waarabu, Warumi na Wafursi kutokana na uoni wa Kiislamu? Lile lililokuwa ni kosa juu yao liliwekwa, linawekwa na litaendelea kuwekwa wazi na kwa nguvu zote kupingwa na Uislamu. Ama lililokuwa zuri kwao wao linakubaliwa kwa uwazi.

 

Uislamu unahimiza kusoma yote ambayo ni mazuri na yenye manufaa kutoka kwa watu wengine. Ingawa Waislamu walishindwa kupata ridhaa ya Mola wao, lakini ilikubalika (kutokana na Shuura waliyoifanya) kwamba mateka wa vita vya Badr wawafundishe watoto wa Kiislamu namna ya kuandika. Wanachuoni kadhaa wamenukuliwa wakitoa ushauri: “Tafuta elimu hata iwe China”.[2]

 

Ndani ya kuta za mwenendo wa Kishari’ah sio dhambi kuomba muongozo kutoka sheria nyengine na kutumia vifungu vyote ambavyo haviendi kinyume wala vyenye kuchukiza dhidi ya mafundisho ya Kiislamu.



[1] Kwa mifano angalia: Goldziher, Introduction Of Islamic Theology And Law – Utangulizi Wa Dhana Ya Kiislamu Na Sheria (Tafsiri ya Kiingereza imefanywa na Andras na Ruth Hamori) uk. 44.

[2] Hii kwa wengi inajulikana kuwa ni Hadiyth ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), lakini ukweli si Hadiyth ni maneno tu ya kutungwa yanayotumika sana kwa kuhamasishia watu elimu.

Share