Kuchukua Mkopo Kutoka Benki Za Kiislamu Inajuzu?

SWALI:

 

Na swali la pili ni kuhusu mabenki ya waislam ambayo yameanziswa kenya kama ni halal kukopa.

 


 

 

JIBU:

 

 

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu kukopa kutoka kwa benki za Kiislamu ambazo zimeanzishwa Kenya.

Kweli benki hizo mbili zimeanzishwa Kenya zikiwa ni First Community Bank na Gulf African Bank. Benki hizo zinaendeshwa na maadili ya Kiislamu kama wanavyosema, hivyo ikiwa hivyo ndivyo wanavyoendesha wanatakiwa wakopeshe bila ya ribaa. Ikiwa watafanya hivyo katika mikopo yao basi mtu ataruhusiwa kukopesha na kuchukua mkopo huo. Lau kutakuwa na ribaa ndani yake hata benki hiyo ikijiita ya Kiislamu itakuwa haifai kwa Muislamu kukopesha.

 

Tunavyoelewa kuhusu benki hizo ni kuwa mpaka sasa hawajaanza kutoa mikopo hiyo. Mikopo pekee wanayotoa ni ile ya kibiashara kama wao kukununulia nyumba, gari, au kukujengea kitu unachotaka nao wakaongeza faida yao baada ya kuimiliki bidhaa hiyo. Mikopo ya masomo ambayo walikuwa waanzishe ina utata ndani yake, hivyo bado hawajaanzisha.

 

Kwa kila hali inayotakiwa kabla ya kuchukua mkopo kwa yeyote au kutoka katika benki yoyote ni kuhakikisha kwanza kama utalipishwa ribaa. Ikiwa utalipa ribaa itakuwa haifai kuchukua na ikiwa hakuna ribaa basi utaruhusiwa kishari’ah kuchukua mkopo huo.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

 

Share