Ufafanuzi Wa Aayah Za Kutunza Mali Ya Yatima Na Kuhusiana Kuoa Wake Wanne

 

Ufafanuzi Wa Aayah Za Kutunza Mali Ya Yatima Na Kuhusiana Kuoa Wake Wanne

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Assalaam Alaykum
 
Naomba Nisaidie Kupata Maana Ya Kina Ya Aya Zile Za Mwanzo (aya 1- 4) Wa Suwrah An-Nisaa. Habari Za Kutunza Vema Mali Za Yatima, Allaah (Subhanahu Wa Ta'aalaa) Ameziunganisha Moja Kwa Moja Na Kuoa Wake 2, 3, Na 4. Mimi Naona Elimu Ya Aya Hii Ni Muhimu Kuielewa.
 
 
Wa Billah Taufiq.

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu ufafanuzi wa Aayah nne za mwanzo za Suwrah An-Nisaa’. Ni muhimu kufahamu tafsiri ya Aayah hizo kabla hatujaingia katika ufafanuzi wenyewe.

 

Tafsiri ni kama ifuatayo:

 

يَا أَيُّهَا النَّاسُ اتَّقُوا رَبَّكُمُ الَّذِي خَلَقَكُم مِّن نَّفْسٍ وَاحِدَةٍ وَخَلَقَ مِنْهَا زَوْجَهَا وَبَثَّ مِنْهُمَا رِجَالًا كَثِيرًا وَنِسَاءً ۚ وَاتَّقُوا اللَّـهَ الَّذِي تَسَاءَلُونَ بِهِ وَالْأَرْحَامَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلَيْكُمْ رَقِيبًا ﴿١﴾وَآتُوا الْيَتَامَىٰ أَمْوَالَهُمْ ۖ وَلَا تَتَبَدَّلُوا الْخَبِيثَ بِالطَّيِّبِ ۖ وَلَا تَأْكُلُوا أَمْوَالَهُمْ إِلَىٰ أَمْوَالِكُمْ ۚ إِنَّهُ كَانَ حُوبًا كَبِيرًا ﴿٢﴾ وَإِنْ خِفْتُمْ أَلَّا تُقْسِطُوا فِي الْيَتَامَىٰ فَانكِحُوا مَا طَابَ لَكُم مِّنَ النِّسَاءِ مَثْنَىٰ وَثُلَاثَ وَرُبَاعَ ۖ فَإِنْ خِفْتُمْ أَلَّا تَعْدِلُوا فَوَاحِدَةً أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُكُمْ ۚ ذَٰلِكَ أَدْنَىٰ أَلَّا تَعُولُوا ﴿٣﴾وَآتُوا النِّسَاءَ صَدُقَاتِهِنَّ نِحْلَةً ۚ فَإِن طِبْنَ لَكُمْ عَن شَيْءٍ مِّنْهُ نَفْسًا فَكُلُوهُ هَنِيئًا مَّرِيئًا ﴿٤﴾

Enyi watu! Mcheni Rabb wenu Ambaye Amekuumbeni kutokana na nafsi moja (Aadam) na Akaumba kutoka humo mke wake (Hawwaa) na Akaeneza kutoka hao wawili wanaume na wanawake wengi. Na mcheni Allaah Ambaye Kwake mnaombana (haki zenu kwa kuunga) undugu. Hakika Allaah ni Mwenye kuwachunga daima. Na wapeni mayatima mali zao, na wala msibadilishe kibaya (chenu) kwa kizuri (chao). Na wala msile mali zao pamoja na mali zenu. Hakika hilo limekuwa ni dhambi kubwa. Na mkikhofu kuwa hamtoweza kufanya uadilifu kwa mayatima; basi oeni waliokupendezeni katika wanawake wengine; wawili au watatu au wanne. Lakini mkikhofu kuwa hamtoweza kufanya uadilifu, basi mmoja tu au ambao mikono yenu ya kulia imewamiliki. Hivyo ni karibu zaidi kwamba hamtoelemea kudhulumu. Na wapeni wanawake mahari zao kwa maridhawa. Lakini wakitoa chochote wenyewe katika mahari yao kwa khiari zao, basi kuleni kwa kufurahia na kunufaika. [An-Nisaa: 1-4]

 

Tukitazama kwa makini Aayah ya kwanza utaona kuwa inatuelezea kuhusu amri ya kuwa na Taqwa (uchaji wa Allaah), tanbihi kuhusu kuumbwa kwa mwanaadamu na kuwatendea wema jamaa.

 

Ama Aayah ya pili hadi ya nne inatuelezea kuhusu ulinzi wa mali ya mayatima. Katika hayo ni kule kuamriwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kuwa mayatima wakabidhiwe mali zao zote wanapofikia baleghe. Hapo hapo Ameharamisha kuitumia au kupora sehemu yake. Hivyo Amesema: “Wala msibadilishe kibaya (Chenu) kwa kizuri (Chao)”. As-Suddiy amesema: “Mmoja wao (mdhamini wa mayatima) angechukua kondoo mnono kutoka kwa mali ya yatima na badala yake akamweka kondoo mkondefu, huku akisema: ‘Kondoo kwa kondoo’. Aidha akachukua dirham halisi na kuibadili kwa dirham bandia, akisema: ‘Dirham kwa dirham’”.

Na kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala): “Na wala msile mali zao pamoja na mali zenu.”. Hiyo ina maana msichanganye ili msile na mali zao, kama Mujaahid, Sa‘iyd bin Jubayr, Muqaatil bin Hayyaan, as-Suddiy na Sufyaan Husayn walivyoelezea, yaani msichanganye mkala wote. Na Allaah Amesema: “Hakika hilo limekuwa ni dhambi kubwa.”, kufanya hivyo ni dhambi kubwa kulingana na Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhuma). Haya yamepokewa pia kutoka kwa Mujaahid, ‘Ikrimah, Sa‘iyd bin Jubayr, al-Hasan, Ibn Siriyn, Qataadah, Muqaatil bin Hayyaan, adhw-Dhwahhaak, Abu Maalik, Zayd bin Aslam na Abu Sinaan. Maana iliyotajwa hapo juu ni kuwa kuchanganya mali yako na yao ni dhambi kubwa na kosa kubwa, hivyo jiepushe nayo.

 

Aayah ya tatu hasa inaharamisha kuwaoa mayatima bila ya kuwapa mahari, kwani kufanya hivyo ni kujitoa katika nidhamu ya Kiislamu iliyo njema kuwa kila mmoja apewe haki yake kwa wakati wake. Ama sehemu ya Aayah: “Na mkikhofu kuwa hamtoweza kufanya uadilifu kwa mayatima; basi oeni waliokupendezeni katika wanawake wengine; wawili..”. Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Anaamuru hapa kuwa mmoja wenu anayemlea yatima wa kike na anachelea kuwa asingeweza kumpa mahari yenye hadhi yake, basi analazimika kumuoa mwanamke mwengine – ambao hao wanawake - wako wengi na Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) hakumkwaza kwa hilo. Imaam al-Bukhaariy alipokea kutoka kwa ‘Urwah bin az-Zubayr (Radhwiya Allaahu ‘anhuma), alisema kuwa alimuuliza Mama wa Waumini ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anha) kuhusu maana ya kauli ya Allaah isemayo: “Na mkikhofu kuwa hamtoweza kufanya uadilifu kwa mayatima;’. Akasema: ‘Ee mpwa wangu! Kauli hii inamhusu yatima wa kike anayesihi na mlezi anayetumia mali yake. Mali yake na uzuri vinaweza kumshawishi kumuoa bila ya kumpa mahari ya kutosha ambayo angepewa na mchumba mwengine. Hivyo, walezi wa aina hiyo wamezuiwa kuwaoa mayatima wa aina hiyo mpaka wawafanyie uadilifu na kuwapa mahari iliyostahili yao; vinginevyo wameamrishwa kuoa wanawake wengine”. Mama wa Waumini ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) aliongeza kusema: “Baada ya kushuka Aayah hiyo, watu waliendelea kumuuliza Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) juu ya kuoa mayatima. Allaah Alishusha Aayah ifuatayo:Na wanatafuta fatwa kwako (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلمkuhusu wanawake.’ (an-Nisaa: 127). Akasema, kauli ya Allaah katika Aayah hii.Na mnapenda kuwaoa’. Inamhusu mlezi ambaye hakusudii kumuoa yatima anayemlea kwa sababu ama hana mali au si mzuri. Walezi walizuiwa kuwaoa mayatima jamali na wenye mali bila kuwatendea uadilifu kama walivyo jiwekea baidi kuwaoa (waliokuwa na mali na jamali)”.

 

Kisha Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Ametoa rukhsa kwa wanaume kuoa wanawake wengi mpaka wanne: “wawili au watatu au wanne. ”, yaani oeni wanawake wengi kama mtakavyo minghairi ya msichana yatima, wawili, watatu au wanne. Na iwapo mmoja wenu anachelea kutofanya uadilifu basi aoe mke mmoja peke yake: “Lakini mkikhofu kuwa hamtoweza kufanya uadilifu, basi mmoja tu au ambao mikono yenu ya kulia imewamiliki.”. Kwa hiyo, kuoa wake wengi kumewekewa sharti na shari’ah ya kuwafanyia insafu na uadilifu na kushindwa kufanya uadilifu inabidi utosheke na mke mmoja tu. Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Amesema: “Hivyo ni karibu zaidi kwamba hamtoelemea kudhulumu.”. Muradi wake ni kutofanya udhalimu. Na wanachuoni wengine wengi wanasema maana yake ni kukengeuka (kwenye haki) kwa mahali ni lazima.

 

Ama Aayah ya nne inatuonyesha sisi uwajibu wa kutoa mahari kuwapa wanawake wanaoolewa. Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhuma) amesema, Nihlah katika kauli ya Allaah (Aayah ya 4) inakusudiwa mahari. Na Mama wa Waumini ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) akasema maana yake imeshurutishwa, na Ibn Zayd akasema: “Katika lugha ya Kiarabu, Nihlah ina maana kitu kilicho lazima”. Hivyo Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Anatuamrisha msioe mpaka muwape wake zenu haki zao. Baada ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hapana mtu mwengine aliyeruhusiwa kuoa mwanamke mpaka kwa kutoa mahari wala si kwa kutoa ahadi za uongo kuhusu mahari iliyokusudiwa. Kwa hiyo, mwanamme anafaa kumpa mahari mkewe kwa moyo safi kama ampavyo zawadi. Hata hivyo, endao mke atampa sehemu au mahari yote kwa hiyari yake bila kulazimishwa, mume anaruhusiwa kuipokea na ni halali kwake katika mazingira haya kuitumia kwa kuifanyia lolote kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa): "Lakini wakitoa chochote wenyewe katika mahari yao kwa khiari zao, basi kuleni kwa kufurahia na kunufaika."

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share