Baada Ya Kumposa Binti Nimpendaye Wazazi Wake Wanakataa Kwa Vile Sio Kabila Moja Nami Nampenda Sana

 

SWALI:

 

Assalam Aleykum ndugu zangu Waislam kwanza napenda kuwapongeza kwa Kufungua Tovuti ya Dini inayoeleimisha na Kufunza mambo Mengi ambayo yako katika Fasiri ya Kiswahili. Na MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHMA AWALIPE KWA HAYA INSHAALLAH.

 

Swali langu ni napenda kuuliza kama Ifuatavyo:

 

Mimi nina Mchumba niiempenda Sana na hata niliamua Kumuoa Kabisa kwani Nilimpenda sana kwa hivyo Niliwaweka Wazazi wangu Chini na nikaongea na wao na walikubali kwenda kunitolea Posa Hivyo Basi Posa Ilitolewa na Ilikubaliwa Lakini Baadaye hawa watu walianza maneno na kusema mimi sifai, na atuko nao kabila moja na Msichana kwani Mwenzangu yeye kidogo amechanganyika na Msomali Lakini Dalili inaonyesha kwamba Hawataki na mimi Nampenda sana Msichana na Ingawa pia Posa yangu sijarudishiwa sasa nifanyeje? Kwani nimejaribu kutafuta msichana Mwingine lakini sikuweza kumuoa kutokana na Mapenzi yaliyomo juu yangu kwa huyo Msichana sasa nifanye nini na mimi mwenyewe nampenda?


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu kukataliwa posa baada ya kukubaliwa.

Hakika hili katika maeneno yetu ni jambo la kawaida, kwa mtu kukubaliwa na baadaye kukataliwa, au kukataliwa moja kwa moja baada ya wazazi kwenda kwa wenziwao wa msichana, au hata kutopokelewa. Na sababu ya kukataliwa sana inatokana na kabila kuwa tofauti kama ulivyoelezea hapo juu. Kukataliwa ni miongoni mwa mitihani ambayo ima mvulana aliyeposa au msichana aliyeposwa wanaipata.

 

Hata hivyo, kukumbana na mtihani huo haifai kumfanya Muislamu akate tamaa au aone dunia ndio imekwisha bali anatakiwa ajipatie moyo kwani wasichana wapo wengi na huenda akapata mwengine aliye bora kuliko yule wa awali. Haifai pia kumpenda msichana kuliko unavyotakiwa kumpenda Mwenyezi Mungu na Mtumewe (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Kuwa na mapenzi aina hiyo ni ishara mbaya kwa Muislamu na kuonyesha upungufu wa Imani.

 

Unapaswa ujiulize kwanza, je, huyu msichana unampenda kwa ajili ya uzuri wake, nasaba yake au Dini na maadili yake? Ikiwa unamtaka kumuoa kwa ajili ya uzuri, nasaba, au mali, ushauri wetu ni kuwa achana naye utafute mwengine kwani Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametuusia sana tutafute msichana tunapotaka kuoa mwenye Dini na sio sababu nyingine yoyote ile. Ama ikiwa umempenda kwa ajili ya uzuri, nasaba au utajiri ni afadhali uachane naye. Na ikiwa umempenda kwa ajili ya Dini yake nzuri basi endelea kufuatilia mpaka utakapofika kikomo.

 

Njia nyingine ya kufuata ni kuwatumia wazee wengine wenye ushawishi katika jamii au Mashaykh ambao wanakubalika ili wawaelezee kuhusu umuhimu ya watu kuoana, bila kujali kabila bali wajali tu Dini. Ikiwa imeshindikana njia hiyo basi itabidi mupeleke kadhiya hiyo kwa Qaadhi wa sehemu uliyopo. Qaadhi atakuita wewe, msichana na wazazi wake. Atawauliza sababu yao (wazazi) kukataa kukuozesha, ikiwa sababu hazina msingi wa kidini ataweza kwaozesha yeye. Hata hivyo, itabidi pia amuulize msichana kama anakubali kuolewa au la, ikiwa atakubali basi Qaadhi anaweza kuwaozesha bila ya tatizo. Lau atakataa basi itakuwa hakuna Nikaah baina yenu kwani mhusika mkuu amekataa kuolewa.

 

Bonyeza viungo vifuatavyo upate maelezo zaidi:

 

 

Nataka Kuolewa Na Kijana Nimpendaye Lakini Wazazi Hawatakubali Kwa Ajili ya Ukabila Na Rangi.

 

Mama Yangu Hamtaki Mume Wangu Kwa Sababu Alikuwa Mtumishi Wetu

 

 

Ndoa Ikiwa Wazazi Hawataki

 

Ndoa Bila Ya Radhi Ya Wazazi

 

Kukosa Radhi Za Mzazi Kwa Kuolewa Na Asiyetakiwa Na Mzazi Bila Sababu Za Kisheria

 

 

Hata ikiwa msichana atakubali hupatikana matatizo mengi kwani msichana huyo hukatwa na wazazi wake, hivyo, watoto wenu hawataweza kwenda kwa babu na bibi zao pamoja na jamaa zao upande wa mama. Na hilo ndilo linalopatikana sana pindi wazazi wanapokataa. Inatakiwa uzingatie sana, na huenda ikawa ni bora kutoa fikra zako juu ya huyo msichana na kufikiria kupata mwengine ambaye atakuridhisha kidini na maadili.

 

 

 

Tunakuombea uweze kusahau hayo na uangalie mengine yenye manufaa zaidi.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share