026-Lu-ulu-un-Manthuwrun: Kulea Watoto Wa Kike Ni Kuwa Pamoja na Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) Peponi

 Lu-ulu-un-Manthuwrun

(Mkusanyiko Wa Hadiyth Mbali Mbali Na Mafunzo Yake)

Hadiyth Ya 26

Kulea Watoto Wa Kike Ni Kuwa Karibu Na Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) Peponi

www.alhidaaya.com

 

 

 

عَنْ أَنَسِ بْنِ مَالِكٍ  (رضي الله عنه)  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اللَّهِ (صلى الله عليه و آله وسلم): ((مَنْ عَالَ جَارِيَتَيْنِ حَتَّى تَبْلُغَا جَاءَ يَوْمَ الْقِيَامَةِ أَنَا وَهُوَ كَهَاتَيْنِ)) وَضَمَّ أَصَابِعَهُ. رواه مسلم  

 

 Imepokelewa kutoka kwa Anas bin Maalik (رضي الله عنه) kwamba Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Atakayewasimamia kuwalea mabinti wawili mpaka wabaleghe, atakuja Siku ya Qiyaamah mimi na yeye ni kama hivi)), Akavishikanisha vidole vyake. [Muslim]

 

  

Mafunzo Na Mwongozo:

 

 

1. Fadhila za kulea watoto wa kike ambao walikuwa wakidhalilishwa zama za ujaahiliyyah mpaka kufikia kuzikwa wangali hai. Allaah (سبحانه وتعالى) Anasema kuwa wataulizwa kuhusu kuuliwa kwao:

 

 

وَإِذَا الْمَوْءُودَةُ سُئِلَتْ ﴿٨﴾

Na mtoto wa kike aliyezikwa hali akiwa yuhai atakapoulizwa.

 

بِأَيِّ ذَنبٍ قُتِلَتْ ﴿٩﴾

Kwa dhambi gani aliuliwa? [At-Takwir: 8-9]

 

 

2. Hoja kwa makafiri wanaozusha kwamba mwanamke wa Kiislamu hana haki wala hadhi. Bali Uislamu umemnyanyua mwanamke cheo chake na kumpatia hadhi kubwa. Hadiyth ifuatayo ni dalili mojawapo ya haya:

 

Mtu mmoja alikuja kwa Nabiy Muhammad (صلى الله عليه وآله وسلم) na akasema: “Ee Rasuli wa Allaah! Ni nani miongoni mwa watu anayestahiki kwamba nimfanyie wema zaidi?” Akasema (صلى الله عليه وآله وسلم): ((Mama yako.)) Yule mtu akasema: “Kisha nani?” Aksema: ((Mama yako.)) Akauliza tena yule mtu: “Kisha nani?” Akasema: ((Mama yako)). Yule mtu akauliza kwa mara nyingine: “Kisha nani?” Akasema: ((Baba yako) [Al-Bukhaariy, Muslim]

 

Bali wanawake wamefadhilishwa mno kama ifuatavyo:

 

 

a) Allaah (سبحانه وتعالى) Ametanguliza kumtaja mwanamke kabla ya kumtaja mwanamume tokea akiwa tumboni kabla ya kuzaliwa kwao. Anasema:

 

لِّلَّـهِ مُلْكُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۚ يَخْلُقُ مَا يَشَاءُ ۚ يَهَبُ لِمَن يَشَاءُ إِنَاثًا وَيَهَبُ لِمَن يَشَاءُ الذُّكُورَ﴿٤٩﴾      

Ni wa Allaah Pekee ufalme wa mbingu na ardhi. Anaumba Atakavyo. Humtunukia Amtakaye wana wa kike, na Humtunukia Amtakaye wana wa kiume.

 

 

أَوْ يُزَوِّجُهُمْ ذُكْرَانًا وَإِنَاثًا ۖ وَيَجْعَلُ مَن يَشَاءُ عَقِيمًا ۚ إِنَّهُ عَلِيمٌ قَدِيرٌ﴿٥٠﴾

Au Huwachanganya wa  kiume na wa kike, na Humjaalia Amtakaye kuwa ni tasa, hakika Yeye ni Mjuzi wa yote, Muweza wa yote. [Ash-Shuwraa (42: 49-50)]

 

 

b) Haajar mama yake Nabiy Ismaa’iyl (عليه السلام) amefadhilishwa kuwa ni sababu ya Umati wa Kiislamu kutekeleza ‘ibaadah ya Sa’y – kutembea baina ya Swafaa na Marwah.

 

 

c) Aayah na Hadiyth kadhaa zimetaja haki za mwanamke. Rejea Hadiyth namba (29), (35), (40).

 

 

 

3. Kulea watoto wa kike malezi mema ya mafunzo ya Dini ni sababu ya mzazi kuingia Jannah. 

 

 

4. Sababu mojawapo ya kumjaalia mtu kuwa karibu na Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) huko Jannah ni kuwalea mabinti malezi mazuri.

 

 

5. Ukarimu na upole wa Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) kwa watoto na wazazi [At-Tawbah (9: 128)].

 

 

6. Muislamu anatakiwa awe mwadilifu kwa watoto wake katika malezi bila kubagua wavulana au wasichana.

 

 

7. Hii inaonyesha fadhila kubwa ya wasichana katika jamii ya Kiislamu. Ndio maana ikasemwa:  “Kumlea vyema msichana ni kutengeneza jamii.”

 

 

Share