Kufanya Zinaa Na Kumuoa Mwanamke Aliyeshika Mimba

SWALI:

Assalaam aleikum,

Baada ya salam na kumshukuru Mwenyezimungu kwa rehma zake na Mtume wetu mohammad ninapenda kutowa shukran zangu za dhati kwa waendeshaji wa tovuti hii ya AL HIDAAYA,kwa kazi hii tukufu munayoifanya kuelemisha ummah. Allah wataala ndiye ataokulipeni ujira wenu.

Halafu tafadhali napenda kuuliza ikiwa mwanamme na mwanamke wamefanya zinaa na wanataka kuowana. Huyo mwanamke anahitajika kushufu kipindi cha kusubiri kusafisha tumbo lake la uzazi kabla ya huyo mwanamme kumuowa? Jee ikiwa ana mimba? Anaweza kumuowa wakati yupo katika mimba na kumwita huyo mtoto wake mwenyewe?

Ndugi zangu suali hili ni muhimu sana kwangu kwa hiyo Inshallah nategemeya majibu karibu kutoka kwenu.

Shukran


JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)  Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allahu 'anhum jamiy'an) na watangu wema mpaka Siku ya Qiyaamah.

 

Kwanza tunapenda na sisi kutoa shukurani kwa du'aa zenu nzuri mnazotuombea nyote mnaotuma maswali yenu pamoja na wengineo wanaoingia ALHIDAAYA  kutafuta faida mbali mbali. Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)  Atutakabalie hizo du'aa na Atuzidishie uwezo wa kuelimishana kwa kadiri Anavyotujaalia. Aamiyn

Shukran kwa muulizaji swali hili. Na inaonyesha kuwa mas-ala haya ya uasherati au mafungamano ya kimwili baina ya mume na mke yamekithiri. Inatakiwa tuwe ni wenye kumcha Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) popote tulipo na kila wakati. Na kama ilivyo kawaida, sisi wanaadamu huwa tunakosea, hivyo tunapokosea au kufanya dhambi basi hapo hapo turudi kwa Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) kwa kumuomba msamaha na kutubia toba ya kweli kweli. Na pia tufanye mambo mema ili yafute hayo mabaya ya madhambi.

Mwanzo inatakiwa tufahamu kuwa zinaa ni kitendo kibaya sana kilichokatazwa na Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) na Mtume Wake (Swalla Llaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Na yeyote mwenye kufanya amali hiyo basi angefaa apatiwe adhabu ya kisheria hapa. Adhabu yenyewe ni kama ifuatavyo:

Ikiwa ni mwanamume au mwanamke waliokuwa hawakuoa/kuolewa bado, na ni watu huru, wenye akili timamu, basi ni kupigwa mijeledi (bakora) mia na ishuhudiwe hiyo adhabu hadharani na kundi la watu. Kisha ni kuhamishwa mbali mwanamume ahame huo mji aliokuwa akiishi kwa muda wa mwaka mmoja.

Ikiwa mwanamume na mwanamke waliozini au mmoja wao ni mtu huru (sio mtumwa), mwenye akili timamu, na amefanya zinaa wakati tayari yumo katika fungamano la ndoa, basi adhabu yake ni kupigwa mawe hadi mauti yawafike.

Dalili ya hayo ni Hadiyth ifuatayo:

فِي الصَّحِيحَيْنِ مِنْ رِوَايَة الزُّهْرِيّ عَنْ عُبَيْد اللَّه بْن عَبْد اللَّه بْن عُتْبَة بْن مَسْعُود عَنْ أَبِي هُرَيْرَة وَزَيْد بْن خَالِد الْجُهَنِيّ فِي الْأَعْرَابِيَّيْنِ اللَّذَيْنِ أَتَيَا رَسُول اللَّه صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ فَقَالَ أَحَدهمَا : يَا رَسُول اللَّه إِنَّ اِبْنِي هَذَا كَانَ عَسِيفًا - يَعْنِي أَجِيرًا - عَلَى هَذَا فَزَنَى بِامْرَأَتِهِ فَافْتَدَيْت اِبْنِي مِنْهُ بِمِائَةِ شَاة وَوَلِيدَة فَسَأَلْت أَهْل الْعِلْم فَأَخْبَرُونِي أَنَّ عَلَى اِبْنِي جَلْد مِائَة وَتَغْرِيب عَام وَأَنَّ عَلَى اِمْرَأَة هَذَا : الرَّجْم فَقَالَ رَسُول اللَّه صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ: ((وَاَلَّذِي نَفْسِي بِيَدِهِ لَأَقْضِيَنَّ بَيْنكُمَا بِكِتَابِ اللَّه تَعَالَى الْوَلِيدَة وَالْغَنَم رَدّ عَلَيْك وَعَلَى اِبْنك مِائَة جَلْدَة وَتَغْرِيب عَام . وَاغْدُ يَا أُنَيْس - لِرَجُلٍ مِنْ أَسْلَم - إِلَى اِمْرَأَة هَذَا فَإِنْ اِعْتَرَفَتْ فَارْجُمْهَا))  فَغَدَا عَلَيْهَا فَاعْتَرَفَتْ فَرَجَمَهَا      البخاري  و مسلم

 

Katika Swahihayn kutoka kwa Abu Hurayrah na Zayd bin Khaalid Al-Juhani (Radhiya Allahu 'anhum) katika kisa cha Mabedui wawili waliokuja kwa Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).  Mmoja alisema: "Ewe Mjume wa Allaah, mwanangu (wa kiume) aliajiriwa na bwana huyu kisha akafanya zinaa na mke wake. Nimemlipa fidia kwa ajili ya mwanangu kwa kumpa kondoo mia moja na mtumwa mwanamke. Lakini nilipowauliza watu wenye elimu, wamesema kwamba mwanangu apigwe mijeledi mia na ahamishwe mji kwa muda wa mwaka na mke wa huyu bwana apigwe mawe hadi afariki".  Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akasema: ((Naapa kwa Yule Ambaye nafsi yangu imo Mikononi Mwake, nitahukumu baina yenu wawili kutokana na kitabu cha Allaah. Rudisha mtumwa mwanamke na kondoo  na mwanao apigwe bakora mia kisha mwanao ahamishwe mbali kwa muda wa mwaka. Nenda Ewe Unays! )) Alimwambia mtu katika kabila la Aslam, ((Nenda kwa mke wa huyu bwana na akikiri makosa yake, basi mpige mawe hadi mauti [yamfike])) Unays akamuendea na akakiri makosa yake, kwa hiyo akampiga mawe hadi mauti. [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

قال الإمام مالك أن عمر، رضي الله عنه، قام فحمد الله وأثنى عليه، ثم قال: أما بعد، أيها الناس، فإن الله بعث محمدًا بالحق، وأنـزل عليه الكتاب، فكان فيما أنـزل عليه آية الرجم، فقرأناها وَوَعَيْناها، وَرَجمَ رسول الله صلى الله عليه وسلم وَرَجمْنا بعده، فأخشى أن يطول بالناس زمان أن يقول قائل: لا نجد آية الرجم في كتاب الله، فيضلوا بترك فريضة قد أنـزلها الله، فالرجم في كتاب الله حق على من زنى، إذا أحصن، من الرجال والنساء، إذا قامت البينة، أو الحبل، أو الاعتراف. (  الموطأ و البخاري و مسلم   )

Imaam Maalik amerikodi kwamba 'Umar (Radhiya Allahu 'anhu) alisimama na kumsifu na kumtukuza Allah, kisha akasema: "Enyi watu! Allah Amemtuma Muhammad (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kwa haki na Amemfunulia Kitabu Chake. Jambo moja alilofunuliwa ni Aayah ya kupigwa mawe hadi mauti ambayo tumeisoma na kuifahamu. Mjumbe wa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) ameitimiza adhabu hii ya kupigwa mawe na baada yake pia sisi tumeitimiza. Lakini nakhofu kuwa muda (miaka) utakapopita wengine watakuja kusema kuwa hawakuiona hii Aayah ya kupigwa mawe katika Kitabu cha Allah, na watapotoka kwa sababu ya kuacha moja ya wajibu wa kisheria iliyofunuliwa katika Kitabu cha Allah kwa mwanamume au mwanamke watakaofanya zinaa, ikiwa mmojawapo ameoa au ameolewa, na ushahidi ukipatikana au mimba ikidhihirika kutokana   na kitendo hicho, au akikiri mmojawao. [Al-Muwattwaa, Al-Bukhaariy na Muslim] 

Hivyo tunaona jinsi gani adhabu kali ilivyoweka hukumu yake katika jambo hili ovu la zinaa, na lau ingelikuwa hukumu hii inatekelezwa katika dola za Kiislamu au kwa kila Muislamu anayetenda kitendo hiki, basi hakika hakuna mtu yeyote angelithubutu kutenda kitendo hiki kiovu kabisa. Ni jambo la kusitisha sana kuona kitendo hiki hakichukuliwi kuwa ni dhambi kubwa ambayo adhabu yake ni kali kama hiyo. Mara kwa mara tunapata maswali kama haya, na mara kwa mara tunasikia kitendo hiki kutendekea katika Jamii yetu na Jamii nyingine pia hadi tumefika kuwa kama makafiri wanaoishi kama wanyama na kuingiliana bila ya khofu yoyote.

Lakini kwa kuwa hakuna dola ya Kiislamu kwa wakati huu na nchi nyingi tunazoishi si za Kiislamu wala Waislamu wengi, anatakiwa mkosa afanye toba ya sawasawa pamoja na kufanya mema mengi kadri ya uwezo wake.

Jambo hili Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Amelikanya na kutuonya hata tusilikaribie kabisa: 

((وَلاَ تَقْرَبُواْ الزِّنَى إِنَّهُ كَانَ فَاحِشَةً وَسَاء سَبِيلاً))

((Wala msikaribie uzinzi. Hakika huo ni uchafu na njia mbaya)) [Al-Israa:32]

Ikiwa watu hao wawili wamefanya zinaa wanaweza kuoana kisheria baada ya kutenganishwa kwa muda. Muda huu ni wa kuhakikisha kuwa yule mwanamke hana mimba. Muda unaweza kuanzia miezi mitatu au kutegemea uamuzi wa Qadhi ikiwa katika sehemu hiyo yupo mmoja. Na ikiwa mwanamke ana mimba basi hawatafaa kuoana mpaka yule mwanamke azae kwa sababu Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amekataza kumwaga mbegu za uzazi juu ya mbegu nyingine kama ilivyo katika Hadiyth ifuatayo:

 

 ((لا يحل لامرئ يؤمن بالله واليوم الآخر أن يسقي ماءه زرع غيره)) ابن حبان  

((Haimpasi mtu mwenye kumuamini Allah na Siku ya Mwisho amwage maji (ya uzazi) juu ya mbegu aliyootesha mwingine)) [Ibn Hibbaan]

Kwa hiyo baada ya kuzaa ndio wanaweza kuoana baada ya wote kufanya toba ya kweli kabisa. Na huu ndio msimamo sahihi (Wa Allahu A'alam) kulinganisha na ule wa wale wanaokataza wasioane hata baada ya toba. Matokeo yake watu wanaendelea kufanya zinaa maadam wamependana na hawawezi kuwa mbali.

Ifahamike kuwa yule mtoto hatokuwa wa baba yule na hawatariathiana kisheria baina yao. Baba hatarithi anachoacha mtoto, wala mtoto kutoka kwa baba.  

Na Allah Anajua zaidi

 

 

Share