Tashahhud Au Tahiyyaatu Nne Kwenye Swalaah Moja

SWALI:

Je, kuna uwezekano wa kuwa na tahiyatu nne kwenye salah moja?


 

JIBU:

AlhamduliLLaah - Himdi Na Sifa Zote Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Mola wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

Hali hii itatokea pale ambapo Masbuwq (aliyetanguliwa au aliyechelewa Rak'ah na Imaam) amechelewa Swalaah ya Maghrib na kukuta Imaam yuko kwenye Tashahhud ya kwanza (ya Rak'ah ya pili), yeye atajiunga na Imaam na kukaa Tashahhud hiyo, kisha Imaam atasimama kumalizia Rak'ah ya tatu, wakati huo kwa Masbuwq hiyo kwake ni Rak'ah ya kwanza, hivyo atasoma Suwratul-Faatihah na Suwrah ndogo. Kisha Imaam atakaa Tashahhud ya pili (ambayo ni Rak'ah ya tatu na ya mwisho ya Swalaah ya Maghrib) na akimaliza Imaam kutoa Salaam zote mbili, Masbuwq atasimama na kwake itakuwa ni Rak'ah ya pili ambapo ataendelea kwenye Rak'ah hiyo kisha atakaa Tashahhud itakayohesabika kwake ni ya kwanza lakini kiujumla itakuwa ni ya tatu tangu alipojiunga na Imaam. Kisha atanyanyuka na kukamilisha Rak'ah ya tatu na kukaa kikao cha Tashahhud itakayohesabika kwake ni ya pili na ya mwisho, ingawa kiujumla atakuwa amekaa vikao vinne vya Tashahhud.

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share