Kumpigia Kura Asiye Muislamu Au Muislamu Mlevi

 

SWALI:

Assalam alaikum, napenda kuuliza swali lenye kunikereketa moyoni mimi naishi zanzibar hivi karibuni tumepiga kura jee iwapo nnayembigia kura si muislam au ni muislam lakini mlevi nitakuwa ni mwenye makosa naomba mnisaidie inshaallah Allah atakulipeni.

 




JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Sifa zote njema Anastahiki Allah Mtukufu, Swalah na salamu zimfikie kipenzi chetu, Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam), Ahli zake na Maswahaba wake (Radhiya Allaahu 'anhum) na Watangu Wema na waliowafuata kwa kheri mpaka Siku ya Qiyaamah.

Kwa hakika mas-ala ya kura inatakiwa tuwe makini sana. Na katika kutekeleza haki yako hiyo uangalie watu ambao watakuwa na maslahi ya Uislamu na kusaidia watu baada ya kuingia bungeni. Hata hivyo masuala haya ya kupiga kura yana utata kishari'ah.

Hivyo, ikiwa amesimama Muislamu na asiyekuwa Muislamu si vyema kwako kumpigia yule asiyekuwa Muislamu hasa unapoangalia Visiwa vya Unguja na Pemba  ambako kunatakiwa wabunge wote wawe Waislamu. Wasiokuwa Waislamu wana mikakati mingi kuvibadilisha visiwa hivyo  na vinginevyo  ili Uislamu uondoke kabisa na hivyo ni muhimu  kwetu kulijua hilo.

Ikiwa waliosimama ni Waislamu wawili basi angalia yule ambaye ataleta maslahi ya dini na watu. Mfano ikiwa waliosimama mmoja ni mlevi na mwingine ni Muislamu mzuri ni lazima umchague yule ambaye ni nafuu au mzuri zaidi kuliko mwingine.

Na Allah Anajua zaidi.

 

Share