016-Majina Ya Allaah Mazuri Na Swifa Zake أسماء الله الحسنى وصفاته: AS-SALAAM

 

أسماء الله الحسنى وصفاته

Majina Ya Allaah Mazuri Na Swifa Zake

 

Alhidaaya.com

 

السَّلام

AS-SALAAM

 

 

 

As-Salaam:  Mwenye Amani,  Mwenye  kusalimika na kasoro zote.

 

Allaah (Tabaaraka wa Ta’aalaa) Ndiye Mwenye haki ya jina hili tukufu Pekee ambalo lina maana zote za ukamilifu, kwani yeye ni As-Salaam katika kila hali na katika kila mazingatio.

 

Yeye Ndiye As-Salaam; Aliyesalimika na kila ovu, shari, aibu, kasoro na upungufu. Yeye ni As-Salaam katika dhati Yake. Yeye ni As-Salaam katika Majina Yake na Sifa Zake.  As-Salaam katika matendo Yake Aliyesalimika na dhuluma.

 

As-Salaam; Yeye (Tabaaraka wa Ta’aalaa) Ndiye Aliyewasalimisha waja Wake na kila adhabu kwa wale ambao hawastahiki na Amewasalimisha na kila dhuluma duniani na Aakhirah.

 

As-Salaam; Yeye (Tabaaraka wa Ta’aalaa) Amewasalimisha Manabii Wake kwa amani na Akawasifia na kuwatenga na aibu na maovu. Na Akawasalimisha Mawalii Wake Aliowachagua. Amewasalimisha duniani na Aakhirah:

 

Duniani: Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

قُلِ الْحَمْدُ لِلَّـهِ وَسَلَامٌ عَلَىٰ عِبَادِهِ الَّذِينَ اصْطَفَىٰ ۗ

Sema: AlhamduliLLaah, Himidi Anastahiki Allaah na Salaamun! Amani iwe juu ya waja Wake Aliowachagua.  [An-Naml 27:59]

 

Na Anasema pia (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

سَلَامٌ عَلَىٰ نُوحٍ فِي الْعَالَمِينَ ﴿٧٩﴾

Salaamun! Amani iwe juu ya Nuwh ulimwenguni. [Asw-Swafaat 37:79]

 

سَلَامٌ عَلَىٰ إِبْرَاهِيمَ ﴿١٠٩﴾

Salaamun! Amani iwe juu ya Ibraahiym. [Asw-Swafaat 37:109]

 

 

Na pia Akamsalimisha Muwsaa na Haaruwn na Iliyaas [Asw-Swafaat 37:120,

 

Na Akawasalimisha Rusuli Wake wote Anasema (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَسَلَامٌ عَلَى الْمُرْسَلِينَ ﴿١٨١﴾

Na Salaamun! Amani iwe juu ya Rusuli.  [Asw-Swafaat 37:181]

 

 

Aakhirah: Atawasalimisha waja Wake watakapoingia Jannah. Anasema (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

إِنَّ أَصْحَابَ الْجَنَّةِ الْيَوْمَ فِي شُغُلٍ فَاكِهُونَ ﴿٥٥﴾

Hakika watu wa Jannah leo wamo katika kushughulika wakifurahi.

 

هُمْ وَأَزْوَاجُهُمْ فِي ظِلَالٍ عَلَى الْأَرَائِكِ مُتَّكِئُونَ ﴿٥٦﴾

Wao na wake zao, wakiwa katika vivuli, juu ya makochi ya fakhari wakiegemea.

 

لَهُمْ فِيهَا فَاكِهَةٌ وَلَهُم مَّا يَدَّعُونَ ﴿٥٧﴾

Watapata humo kila aina ya matunda, na watapata wanavyoomba.

 

سَلَامٌ قَوْلًا مِّن رَّبٍّ رَّحِيمٍ ﴿٥٨﴾

“Salaamun!” Kauli kutoka kwa Rabb Mwenye kurehemu. [Yaasiyn 36: 55-58]

 

Na pia:

 

تَحِيَّتُهُمْ يَوْمَ يَلْقَوْنَهُ سَلَامٌ ۚ وَأَعَدَّ لَهُمْ أَجْرًا كَرِيمًا ﴿٤٤﴾

Maamkizi yao Siku watakayokutana Naye; ni ‘Salaam’; na Amewaandalia ujira wa ukarimu. [Al-Ahzaab 33:44]

 

Ni salama na amani itokayo kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) inatosheleza kuliko salama nyingine yoyote ile, na inatosheleza kuliko maamkizi mengine yoyote yale, na inamkurubisha mtu na kila tarajio lake. “Nini dhana yako na maamkizi ya Mfalme wa wafalme, Rabb ‘Adhimu, Mpole Mwenye kurehemu, kwa waja wenye kustahiki ukarimu Wake, wale waliopata radhi Zake, basi hatowaghadhibikia kamwe.” [Tafsiyr As-Sa’adiy Suwrat Yaasiyn 36: 58].

 

As-Salaam; Yeye Ndiye chanzo cha amani na usalama, kila amani hutoka Kwake, hivyo usitake amani na usalama isipokuwa Kwake tu (Tabaaraka wa Ta’aalaa).

 

As-Salaam; Yeye (Tabaaraka wa Ta’aalaa) Ndiye Mwenye kuwasalimisha Awatakaye katika waja Wake kwa muktadha wa hekima Yake, na uadilifu Wake duniani.

 

عن أَبي هُرَيْرَةَ رضي الله عنه قَالَ: سَمِعْتُ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ يَقُولُ:  ((مَثَلُ الْمُجَاهِدِ فِي سَبِيلِ اللَّهِ - وَاللَّهُ أَعْلَمُ بِمَنْ يُجَاهِدُ فِي سَبِيلِهِ- كَمَثَلِ الصَّائِمِ الْقَائِمِ، وَتَوَكَّلَ اللَّهُ لِلْمُجَاهِدِ فِي سَبِيلِهِ بِأَنْ يَتَوَفَّاهُ أَنْ يُدْخِلَهُ الْجَنَّةَ، أَوْ يَرْجِعَهُ سَالِمًا مَعَ أَجْرٍ أَوْ غَنِيمَةٍ)) البخاري  كتاب الجهاد والسير  

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Huraryah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba: Nimemsikia Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: “Mfano wa Mujaahid katika njia ya Allaah – na Allaah Anamjua aliye Mujaahid katika njia Yake - ni kama aliyefunga Swawm   kwa kuendeleza. Allaah Amempa dhamana  kwamba Akimfisha, Atamuingiza  Jannah au arudi salama pamoja na ujira wa ghanima.” [Al-Bukhaariy katika Kitaab Al-Jihaad Was-Sayr]

 

Na Aakhirah Atawasalimisha waja Wake kama ilivyo katika Hadiyth ya Asw-Swiraatw:

 

فَأَكُونُ أَوَّلَ مَنْ يُجِيزُ، وَدُعَاءُ الرُّسُلِ يَوْمَئِذٍ: اللَّهُمَّ سَلِّمْ سَلِّمْ

“… na nitakuwa wa kwanza kuvuka, na du’aa ya Rasuli siku hiyo itakuwa: Allaahumma Sallim, Sallim!  (Ee Allaah tusalimishe, tusalimishe)” [Al-Bukhaariy Kitaab Ar-Riqaaq]

 

 

Jina hili tukufu limetajwa mara moja tu katika Qur-aan Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

هُوَ اللَّـهُ الَّذِي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ الْمَلِكُ الْقُدُّوسُ السَّلَامُ  

Yeye Ndiye Allaah Ambaye hakuna Muabudiwa wa haki ila Yeye, Mfalme, Mtakatifu Ametakasika na sifa zote hasi, Mwenye kusalimisha, Amesalimika na kasoro zote. [Al-Hashr 59: 23]

 

 

Faida, Mafunzo Tuyapatayo Na Jinsi Ya Kufanyia Kazi Jina Hili La Allaah: As-Salaam:

 

1. Kuomba du’aa kwa As-Salaam kwa unyenyekevu uombe salama duniani na Aakhirah.  

 

Ya kuomba salama duniani ni kama vile kuomba afya kutokana na maradhi, maafa na mambo yote mtu anayoyachukia.

 

Ama ya kuomba salama Aakhirah ni kuomba amani na salama katika Dini yako. Uombe salama na yakini kutokana na ukafiri, shirki, unafiki, bid’ah, maasi na kadhaalika. Na utangulize kwa Rabb wako fungamano la iymaan ya nguvu kabisa na salama katika moyo wako dhidi ya yote yanayomghadhibisha Rabb wako (Tabaaraka wa Ta’aalaa) na sifa chafu na mbaya hadi utakapokutana na Rabb wako ukiwa na moyo wa salama kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

يَوْمَ لَا يَنفَعُ مَالٌ وَلَا بَنُونَ ﴿٨٨﴾

“Siku hayatofaa mali wa watoto.

 

إِلَّا مَنْ أَتَى اللَّـهَ بِقَلْبٍ سَلِيمٍ ﴿٨٩﴾

“Isipokuwa yule atakayemfikia Allaah na moyo uliosalimika. [Ash-Shu’araa 26: 88-89]

 

 

Na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akasisitiza kuomba hayo ya salama na amani duniani na Aakhirah na akabainisha kuwa kupata salama katika Dini ndio khayr kubwa mno baada ya iymaan na ndio kufuzu. Hadiyth mbili miongoni mwazo ni:

 

قامَ أَبُو بَكْرٍ الصّدّيقُ عَلَى المِنْبَرِ ثُمّ بَكَى فقَالَ: قامَ رَسُولُ الله صلى الله عليه وسلم عَامَ الأوّلِ عَلَى المنْبَر ثُمّ بَكَى فقَالَ: ((سَلُوا اللهَ العَفْوَ والعَافِيَةَ ، فإِنّ أَحَداً لَمْ يُعْطَ بعد اليَقِين خَيْراً مِنَ الْعَافِيَة )) صحيح الترمذي (3558)،  وصحيح الترغيب والترهيب  (3387) صحيح الجامع (3632)

Abuu Bakr Asw-Swiddiyq (Radhwiya Allaahu 'anhu) alisimama juu ya minbari kisha akalia akasema: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alisimama katika minbari hiyo mwaka wa mwanzo akalia na akasema: ((Muombeni Allaah msamaha na Al-‘Aafiyah (salama, amani hifadhi ya kila baya) kwani  hakika baada ya iymaan, hakuna kilicho bora kupewa kama Al-’Aafiyah)) [Swahiyh At-Tirmidhiy (3558), Swahiyh At-Targhiyb (3387), Swahiyh Al-Jaami’ (3632)]

 

Na pia:

 

عنْ سَلَمَةَ بْنِ وَرْدَانَ الْمَدَنِيِّ، قَالَ: سَمِعْتُ أَنَسَ بْنَ مَالِكٍ قَالَ: جَاءَ رَجُلٌ إِلَى رَسُولِ اللهِ صلى الله عليه وسلم  فَقَالَ : يَا رَسُولَ اللهِ، أَيُّ الدُّعَاءِ أَفْضَلُ ؟ قَالَ: ((تَسْأَلُ رَبَّكَ الْعَفْوَ وَالْعَافِيَةَ فِي الدُّنْيَا وَالآخِرَةِ)) ثُمَّ أَتَاهُ مِنْ الْغَدِ فَقَالَ: يَا رَسُولَ اللهِ، أَيُّ الدُّعَاءِ أَفْضَلُ ؟ قَالَ: ((تَسْأَلُ رَبَّكَ الْعَفْوَ وَالْعَافِيَةَ  فِي الدُّنْيَا وَالآخِرَةِ)) ثُمَّ أَتَاهُ الْيَوْمَ الثَّالِثَ، فَقَالَ: يَا رَسُولَ اللهِ، أَيُّ الدُّعَاءِ أَفْضَلُ؟ قَالَ: ((تَسْأَلُ رَبَّكَ الْعَفْوَ وَالْعَافِيَةَ فِي الدُّنْيَا وَالآخِرَةِ، فَإِنَّكَ إِذَا أُعْطِيتَهُمَا فِي الدُّنْيَا ثُمَّ أُعْطِيتَهُمَا فِي الآخِرَةِ فَقَدْ أَفْلَحْتَ)) أحمد، 19/ 304 واللفظ له، الترمذي 3512  وابن ماجه  3848،  والأدب المفرد للبخاري، ص 222 .

 

Imepokelewa kutoka kwa Salamah bin Wardaan Al-Madaniyy (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba amemsikia Anas bin Maalik (Radhwiya Allaahu 'anhu) akisema: “Alikuja mtu kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akasema: Ee Rasuli wa Allaah! Du’aa gani ni bora kabisa? Akasema: ((Umuombe Rabb wako afya na Al-‘Aafiyah (hifadhi, amani, salama) duniani na Aakhirah)). Kisha akamjia tena siku ya pili yake akamuuliza: Ee Rasuli wa Allaah! Du’aa gani ni bora kabisa? Akasema: ((Umuombe Rabb wako afya na Al-‘Aafiyah duniani na Aakhirah)). Kisha akamjia tena siku ya tatu akamuuliza: Ee Rasuli wa Allaah! Du’aa gani ni bora kabisa? Akasema: ((Umuombe Rabb wako afya na Al-‘Aafiyah duniani na Aakhirah, kwani ukipewa hayo mawili duniani kisha ukapewa Aakhirah basi kwa yakini umefaulu)) [Ahmad (19/304) na tamshi lake, At-Tirmidhiy (3512), Ibn Maajah (3848), Al-Adab Al-Mufrad (222)]   

 

 

Na du’aa yenyewe alikuwa akiomba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika nyiradi za asubuhi na jioni kama ifuatavyo:

 

اللّهُـمَّ إِنِّـي أسْـأَلُـكَ العَـفْوَ وَالعـافِـيةَ في الدُّنْـيا وَالآخِـرَة، اللّهُـمَّ إِنِّـي أسْـأَلُـكَ العَـفْوَ وَالعـافِـيةَ في ديني وَدُنْـيايَ وَأهْـلي وَمالـي، اللّهُـمَّ اسْتُـرْ عـوْراتي وَآمِـنْ رَوْعاتـي، اللّهُـمَّ احْفَظْـني مِن بَـينِ يَدَيَّ وَمِن خَلْفـي وَعَن يَمـيني وَعَن شِمـالي، وَمِن فَوْقـي، وَأَعـوذُ بِعَظَمَـتِكَ أَن أُغْـتالَ مِن تَحْتـي

Allaahumma inniy as-alukal ‘aafiyah fid-dun-yaa wal Aakhirah. Allaahumma inni as-alukal ‘afwa wal ‘aafiyata fiy Diyniy wa dun-yaaya, wa ahliy, wa maaliy. Allaahumma-stur ‘awraatiy, wa-aamin raw’aatiy. Allaahumma-hfadhwniy min bayni yadayya, wamin khalfiy, wa ‘an yamiyniy, wa ‘an shimaaliy, wamin fawqiy, wa a’uwdhu bi’adhwamatika an ughtaala min tahtiy

 

Ee Allaah, hakika nakuomba msamaha na Al’-Aafiyah (hifadhi, amani, salama) duniani na Aakhirah. Ee Allaah, hakika nakuomba msamaha na Al’-Aafiyah katika Dini na dunia yangu, na ahli wangu, na mali yangu. Ee Allaah aibu zangu na nitulize khofu yangu. Ee Allaah, nihifadhi mbele yangu, na nyuma yangu, na kulia kwangu, na kushoto kwangu, na juu yangu, na najikinga kwa Uadhimu Wako kwa kutekwa chini yangu. [Hadiyth ya ‘Abdullaah bin ‘Umar (Radhwiya Allaahu ’anhu) Swahiyh Ibn Maajah (2/332), Swahiyh Abiy Daawuwd (5074)].    

 

2. Kuusalimisha ulimi wako na kiwiliwili chako katika kuwaudhi watu:

 

عَنْ عَبْدِ اللَّهِ بْنِ عَمْرٍو (رضي الله عنهما) قَال: قَال رَسُولُ الله صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ: ((الْمُسْلِمُ مَنْ سَلِمَ الْمُسْلِمُونَ مِنْ لِسَانِهِ وَيَدِهِ)) متفق عليه

Imepokelewa kutoka kwa ‘Abdullaah in ‘Amr (Radhwiya Allaahu 'anhumaa) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Muislamu ni yule anayeweka amani kwa watu [ambaye Waislamu wenziwe wanasalimika] kwa ulimi na mkono wake)) [Al-Bukhaariy, Muslim]  

 

3. Kutoa salaam kwa watu. Unapoamkia mtu: “Assalaamu ‘Alaykum” (Amani iwe juu yenu) inamaanisha: “Mko katika amani na hamtopata maovu yoyote kutoka Kwangu.”

 

Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesisitiza katika Hadiyth kadhaa miongoni mwazo ni:

 

عن عبدِ اللهِ بنِ مسعودٍ قال إنَّ السَّلامَ اسمٌ من أسماءِ اللهِ وضعَهُ اللهُ في الأرضِ ، فأفشُوهُ بينكم ، إنَّ الرَّجلَ إذا سلَّم على القومِ فردُّوا عليه كانت عليهم فضلُ درجةٍ ؛ لأنَّه ذكَّرَهم بالسَّلامِ ، وإن لم يردَّ عليه ردَّ عليه مَن هو خيرٌ منه وأطيبُ

Imepokelewa kutoka kwa ‘Abdullaah bin Mas’uwd (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((As-Salaam ni katika Majina ya Allaah Ameweka ardhini, basi salimianeni baina yenu. Hakika mtu anaposalimia watu wakamjibu, basi hupata daraja ya juu kabisa kuliko wao kwa sababu amewakumbusha amani. Ikiwa hatomjibu mtu, atajibiwa na ambaye ni mbora zaidi kuliko yeye na mzuri zaidi. [Swahiyh Adab Al-Mufrad  (793), Swahiyh Al-Jaami’ (3697)]

 

Mwenye sifa hiyo ya kuwatolea watu salaam atapata salama na amani ya milele katika Daarus-Salaam (Jannah), kutokana na Hadiyth ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ambayo ilikuwa ni katika mafunzo ya mwanzo kabisa kuwapa Maswahaba Madiynah:

 

((يَا أَيُّهَا النَّاسُ، أَفْشُوا السَّلَامَ، وَأَطْعِمُوا الطَّعَامَ، وَصِلُوا الْأَرْحَامَ، وَصَلُّوا بِاللَّيْلِ وَالنَّاسُ نِيَامٌ تَدْخُلُوا الْجَنَّةَ بِسَلَامٍ)) رواه الترمذي، حديث صحيح

((Enyi watu, enezeni (amkianeni) salaam, na lisheni chakula, na Swalini watu wakiwa wamelala, mtaingia  Jannahh kwa salama)) [At-Tirmidhiy – Hadiyth Swahiyh]

 

 

4. Usiache kusoma du’aa baada ya kila Swalaah:

 

أَسْـتَغْفِرُ الله، أَسْـتَغْفِرُ الله، أَسْـتَغْفِرُ الله، اللّهُـمَّ أَنْـتَ السَّلامُ، وَمِـنْكَ السَّلام، تَبارَكْتَ يا ذا الجَـلالِ وَالإِكْـرام

Astaghfiru-Allaah, Astaghfiru-Allaah, Astaghfiru-Allaah. Allaahumma Antas-Salaam, wa Minkas-salaam, Tabaarakta yaa dhal-Jalaali wal-Ikraam

 

Namuomba Allaah maghfirah, Namuomba Allaah maghfirah,  Namuomba Allaah maghfirah. Ee Allaah Wewe Ndiye As-Salaam na Kwako ndiko kutokako salama, Umebarikika Ee Mwenye Ujalali na Ukarimu. [Hadiyth ya Thawbaan Al-Haashimiy (Radhwiya Allaahu 'anhu) katika  Muslim (1/414) [591]

 

5. Kithirisha kumswalia Nabiy Muhammad  (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na kumuombea salama kama Anavyoamrisha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):  

   

إِنَّ اللَّـهَ وَمَلَائِكَتَهُ يُصَلُّونَ عَلَى النَّبِيِّ ۚ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا صَلُّوا عَلَيْهِ وَسَلِّمُوا تَسْلِيمًا ﴿٥٦﴾

Hakika Allaah na Malaika Wake wanamswalia Nabiy. Enyi walioamini mswalieni na msalimieni kwa mamkizi ya amani na kwa tasliymaa. [Al-Ahzaab 33: 56]

 

6. Unaposibiwa na maradhi, maafa, shida omba du’aa kwa kutawassal kwa Jina hili tukufu la As-Salaam. Unaweza kusema: “Allaahumma Antas-Salaam niponyeshe kadhaa.” Au “Niondoshee dhiki zangu kadhaa.“ Au “Nijaalie salama na matatizo kadhaa.” Au “Nijaalie salama na amani kutokana na adui zangu kadhaa…”

 

 

 

 

 

Share