14-Kitaab At-Tawhiyd: Kustaghithi Na Kumwomba Asiyekuwa Allaah Ni Shirki

Mlango Wa 14

بَابٌ مِنْ اَلشِّرْكِ أَنْ يَسْتَغِيثَ بِغَيْرِ اَللَّهِ أَوْ يَدْعُوَ غَيْرَهُ

Kustaghithi[1] Na Kumwomba Asiyekuwa Allaah Ni Shirki


 

وَقَوْلُ اَللَّهِ تَعَالَى:

Na kauli ya Allaah Ta’aalaa:

 

  وَلَا تَدْعُ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُكَ وَلَا يَضُرُّكَ ۖ فَإِن فَعَلْتَ فَإِنَّكَ إِذًا مِّنَ الظَّالِمِينَ ﴿١٠٦﴾

 ((“Na wala usiombe badala ya Allaah visivyokufaa wala visivyokudhuru. Na ukifanya, basi hakika utakuwa miongoni mwa madhalimu.”))

 

وَإِن يَمْسَسْكَ اللَّـهُ بِضُرٍّ فَلَا كَاشِفَ لَهُ إِلَّا هُوَ ۖ وَإِن يُرِدْكَ بِخَيْرٍ فَلَا رَادَّ لِفَضْلِهِ ۚ يُصِيبُ بِهِ مَن يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ ۚ وَهُوَ الْغَفُورُ الرَّحِيمُ ﴿١٠٧﴾

((Na Allaah Akikugusisha dhara, basi hakuna wa kuiondosha isipokuwa Yeye. Na Akikutakia khayr, basi hakuna wa kurudisha fadhila Zake, Anasababisha kumfikia kwayo (fadhila Yake) Amtakaye katika waja Wake. Naye ni Mwingi wa kughufuria, Mwenye kurehemu))  [Yuwnus (10: 106-107)]

وَقَوْلُهُ:

Na kauli Yake: 

 

إِنَّمَا تَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ أَوْثَانًا وَتَخْلُقُونَ إِفْكًا ۚ إِنَّ الَّذِينَ تَعْبُدُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ لَا يَمْلِكُونَ لَكُمْ رِزْقًا فَابْتَغُوا عِندَ اللَّـهِ الرِّزْقَ وَاعْبُدُوهُ وَاشْكُرُوا لَهُ ۖ إِلَيْهِ تُرْجَعُونَ ﴿١٧﴾

((“Hakika mnaabudu badala ya Allaah masanamu, na mnazua uzushi. Hakika wale mnaowaabudu badala ya Allaah hawakumilikiini riziki; basi tafuteni riziki kwa Allaah, na mwabuduni Yeye na mshukuruni, Kwake mtarejeshwa)) [Al-‘Ankabuwt (29: 17)]

 

وَقَوْلُهُ:

Na kauli Yake:

 

وَمَنْ أَضَلُّ مِمَّن يَدْعُو مِن دُونِ اللَّـهِ مَن لَّا يَسْتَجِيبُ لَهُ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ وَهُمْ عَن دُعَائِهِمْ غَافِلُونَ ﴿٥﴾

((“Na nani aliyepotoka zaidi kuliko ambaye anayeomba asiyekuwa Allaah ambaye hamuitikii mpaka Siku ya Qiyaamah; nao wala hawatambui maombi yao.”)) [Al-Ahqaaf (46: 5)]

وَقَوْلُهُ:

Na kauli Yake:

 

 أَمَّن يُجِيبُ الْمُضْطَرَّ إِذَا دَعَاهُ وَيَكْشِفُ السُّوءَ وَيَجْعَلُكُمْ خُلَفَاءَ الْأَرْضِ ۗ أَإِلَـٰهٌ مَّعَ اللَّـهِ ۚ قَلِيلًا مَّا تَذَكَّرُونَ ﴿٦٢﴾

((Au nani Anayemuitika mwenye dhiki mno anapomwomba, na Akamuondoshea ouvu na Akakufanyeni makhalifa wa ardhi? Je, yuko muabudiwa wa haki pamoja na Allaah? Ni machache mno mnayokumbuka)) [An-Naml (27: 62)]

 

وروى الطَبَرانيُّ بإسناده: أنه كان في زمن النبي (صلى الله عليه وسلم) منافق يؤذِي المؤمنين، فقال بعضهم: قوموا بنا نَسْتغيثُ برسول الله (صلى الله عليه وسلم) من هذا المنافق. فقال النبي (صلى الله عليه وسلم): ((إنه لايُسْتَغَاثُ بي، وإِنمَاَ يُسْتغاث بالله))

Amesimulia At-Twabaraaniy kwa isnaad yake kwamba katika zama za Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) alikuwepo mnafiki akiwaudhi Waumini. Wakasema baadhi yao: “Simameni mtuunge tukastaghithi kwa Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) dhidi ya mnafiki huyu.” Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) akasema: ((Hakika haipasi kustaghithi kwangu, bali inapaswa kustaghithi kwa Allaah)) [Atw-Twabaraaniy fiy Mu’jamil-Kabiyr] 

 

 

Masuala Muhimu Yaliyomo:

 

1-Kuunganisha baina ya “kuomba” (du’aa) na “istighaathah’ ni kama kuunganisha baina ya jambo la ujumla na makhsusi.

 

2-Tafsiri ya Aayah:

وَلَا تَدْعُ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُكَ وَلَا يَضُرُّكَ ۖ

((“Na wala usiombe badala ya Allaah visivyokufaa wala visivyokudhuru)).

 

3-Kufanya hivyo ni shirki kubwa.

 

4-Hata mtu mwema akifanya hivyo; yaani kumwomba asiyekuwa Allaah (سبحانه وتعالى), tena kwa ajili ya kuwaridhisha wengine basi anakuwa mmojawapo katika madhalimu (washirikina).

 

5-Tafsiri inayofuatia (Yuwnus: 10:107).

 

6-Kumuomba asiyekuwa Allaah (سبحانه وتعالى), hakunufaishi duniani na juu ya hivyo ni kufuru.

 

7-Tafsiri ya Aayah ya tatu (Al-‘Ankabuwt 29:17).

 

8-Haitakiwi kuomba riziki ispokuwa kwa Allaah (سبحانه وتعالى), kama ilivyo Jannah isiombwe isipokuwa Kwake.

 

9-Tafsiri ya Aayah ya nne (Al-Ahqaaf 46: 5).

 

10-Hakuna mpotovu zaidi kuliko yule anayemwomba asiye Allaah (سبحانه وتعالى).

 

11-Anayeombwa si mwenye kumsikia muombaji, hana khabari ya lolote kati ya maombi ya muombaji.

 

12-Maombi hayo yatakuwa ni sababu ya chuki na uadui kati ya anayeomba na anayeombwa. 

 

13-Kumuomba yeyote ni aina ya ‘ibaadah basi huwa ni kumwabudu unayemuomba. 

 

14-Anayeombwa atakanusha kitendo hicho cha ‘ibaadah kinachoelekezwa kwake na mwombaji.   

 

15-Ndio maana ikawa mwombaji huyo ni mpotovu zaidi kuliko wote.

 

16-Tafsiri ya Aayah ya tano (An-Naml 27: 62).

 

17-Jambo la ajabu ni kukiri kwa washirikina kwamba hakuna anayeweza kuondoa dhiki na shida isipokuwa Allaah (سبحانه وتعالى) Pekee. Ndio maana wakawa wanaomuomba Allaah (سبحانه وتعالى) kwa ikhlaasw kabisa wanapokuwa katika janga.

 

18-Himaya ya Rasuli (صلى الله عليه وآله وسلم) katika kuihami Tawhiyd na kuwa na umakini wa kumheshimu Allaah (سبحانه وتعالى).

 

 

 

 

 

 

[1] Kuomba msaada wa uokozi katika ambayo hayamo katika uwezo wa mwana Aadam.

Share