021-Majina Ya Allaah Mazuri Na Swifa Zake أسماء الله الحسنى وصفاته: AL-MUTAKABBIR

 

أسماء الله الحسنى وصفاته

Majina Ya Allaah Mazuri Na Swifa Zake

 

Alhidaaya.com

 

 

الْمُتَكَبِّر

AL-MUTAKABBIR

 

 

 

Al-Mutakabbir:  Mkubwa, Aliye na nguvu dhidi ya kila shari, uovu na dhulma.

 

 

Al-Mutakabbir imetajwa katika Qur-aan mara moja kwenye kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

هُوَ اللَّـهُ الَّذِي لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ الْمَلِكُ الْقُدُّوسُ السَّلَامُ الْمُؤْمِنُ الْمُهَيْمِنُ الْعَزِيزُ الْجَبَّارُ الْمُتَكَبِّرُ ۚ سُبْحَانَ اللَّـهِ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٢٣﴾

Yeye Ndiye Allaah Ambaye hakuna Muabudiwa wa haki ila Yeye, Mfalme, Mtakatifu Ametakasika na sifa zote hasi, Mwenye kusalimisha, Amesalimika na kasoro zote, Mwenye kusadikisha ahadi, Mwenye kuaminisha, Mwenye kudhibiti, kushuhudia, kuchunga na kuhifadhi, Mwenye enzi ya nguvu Asiyeshindika, Jabari, Asiyeshindwa kufanya Atakalo, Mkubwa na adhama, Subhaana Allaah! Utakasifu ni wa Allaah kutokana na ambayo wanamshirikisha. [Al-Hashr: 59:23]

 

Al-Mutakabbir: Mtukufu mno, Mwenye hadhi, fakhari, shani, ukubwa, Aliye na nguvu kubwa za kuwatenza nguvu viumbe Wake waasi, Yuko juu ya viumbe.

 

Al-Mutakabbir: Mwenye kustahiki kutakabari  nayo ni utukufu, hadhi ya juu, na Al-Kibriyaa kwa maana: Ufalme, hadhi, fakhari, shani, ukubwa.

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kuhusu Fir’awn:

 

قَالُوا أَجِئْتَنَا لِتَلْفِتَنَا عَمَّا وَجَدْنَا عَلَيْهِ آبَاءَنَا وَتَكُونَ لَكُمَا الْكِبْرِيَاءُ فِي الْأَرْضِ وَمَا نَحْنُ لَكُمَا بِمُؤْمِنِينَ ﴿٧٨﴾

Wakasema: “Je, umetujia ili utugeuze kutokana na yale tuliyowakuta nayo baba zetu, na ili muwe na ukubwa na adhama katika ardhi? Na sisi hatutawaamini nyinyi.”  [Yuwnus 10: 78]

 

Yaani Ufalme. [Imethibiti kutoka kwa Mujaahid ‘At-Tafsiyr Asw-Swahiyh’ (3/30)]

 

Pia ina maana ni ukubwa na uadhama na uongozi. [Tafsiyr Ibn Kathiyr]

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

عَالِمُ الْغَيْبِ وَالشَّهَادَةِ الْكَبِيرُ الْمُتَعَالِ ﴿٩﴾

Mjuzi wa ghayb na dhahiri, Mkubwa wa dhati vitendo na sifa, Mwenye Uluwa Aliyejitukuza kabisa. [Ar-Ra’d 13: 9]

 

Allaah (Tabaaraka wa Ta’aalaa) Ana maana zote za utukufu nazo ni ukamilifu katika Jina Lake la Al-Mutakabbir Ambalo ni Lake Pekee. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَلَهُ الْكِبْرِيَاءُ فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۖ وَهُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ ﴿٣٧﴾

Na Ukubwa, Uadhama, Ujalali ni Wake Pekee mbinguni na ardhini; Naye Ndiye Mwenye enzi ya nguvu Asiyeshindika, Mwenye hikmah wa yote. [Al-Jaathiyah 45: 37]

  

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakabbir: Ndiye Mkubwa na Ametukuka katika dhati Yake na Sifa Zake, matendo Yake, ufalme Wake, na kila kitu chini Yake ni kidogo na dhalili.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakabbir: Mwenye kujiadhimisha, Ambaye Nafsi Yake iko juu ya utukuzwaji wa chochote; hana mfanowe.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakabbir: Ufalme Wake hauondoki, mwenye kudumu milele:  

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakaabir: Naye ni Mwenye kutakabari na dhulma za waja Wake, Hamdhulumu yeyote katika waja Wake, hata kama mwenye kumkufuru.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakaabir: Yeye Ndiye Mwenye kuwashinda wanaojifanya ni majabari katika Waja wake na Anaahidi kuwaadhibu kutokana na kutakabari kwao: Anasema (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَيَوْمَ يُعْرَضُ الَّذِينَ كَفَرُوا عَلَى النَّارِ أَذْهَبْتُمْ طَيِّبَاتِكُمْ فِي حَيَاتِكُمُ الدُّنْيَا وَاسْتَمْتَعْتُم بِهَا فَالْيَوْمَ تُجْزَوْنَ عَذَابَ الْهُونِ بِمَا كُنتُمْ تَسْتَكْبِرُونَ فِي الْأَرْضِ بِغَيْرِ الْحَقِّ وَبِمَا كُنتُمْ تَفْسُقُونَ ﴿٢٠﴾

Na siku watakayotandazwa wale waliokufuru kwenye moto (waambiwe): “Je, mshamaliza vizuri vyenu katika uhai wenu wa dunia na mshajistarehesha navyo? Basi leo mtalipwa adhabu ya udhalilifu kwa yale mliyokuwa mkitakabari katika ardhi bila ya haki na kwa sababu mlikuwa mnafanya ufasiki.” [Al-Ahqaaf 46: 20]

 

Na Anasema pia:

 

وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ تَرَى الَّذِينَ كَذَبُوا عَلَى اللَّـهِ وُجُوهُهُم مُّسْوَدَّةٌ ۚ أَلَيْسَ فِي جَهَنَّمَ مَثْوًى لِّلْمُتَكَبِّرِينَ﴿٦٠﴾

Na Siku ya Qiyaamah utawaona wale waliomsingizia uongo Allaah, nyuso zao zimesawajika. Je, kwani si katika Jahannam ndio makazi kwa ajili ya wanaotakabari?  [Az-Zumar 389: 60]

 

Yeye ni Al-Mutakabbir kwa kila upungufu na kila aibu, Ameepukana na kila ovu na kila kisichokuwa stahiki ya utukufu Wake.

 

Al-Mutakabbir: Ni Mtukufu Mwenye kupitisha mambo Yake kwa waja Wake, hakipiti katika ufalme Wake ila tu Anachokitaka.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakaabir kwa kila ovu hakitoki Kwake isipokuwa ni khayr tupu.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakabbir: Yuko juu ya waja Wake, kwa kila aina ya kuwa juu: Katika dhati Yake na katika Sifa Yake.

 

Al-Kibriyaa (Ukubwa, utukufu, uadhama, ujalali) wa Allaah hauna mwisho, Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

 

يَعْلَمُ مَا بَيْنَ أَيْدِيهِمْ وَمَا خَلْفَهُمْ وَلَا يُحِيطُونَ بِهِ عِلْمًا ﴿١١٠﴾

Anajua yale yaliyoko mbele yao, na yale yaliyoko nyuma yao, na wala hawawezi kufikia kuelewa chochote cha ujuzi Wake. [Twaahaa 20: 110]

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakabbir: Mwenye kutakabari katika Uola Wake (Ar-Rubuwbiyyah), Hana mshirika katika ufalme Wake, Mwenye kutakabari katika kuabudiwa Kwake (Uluwhiyyah); Hakubali Aabudiwe asiyekuwa Yeye. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

فَإِنَّهُمْ يَوْمَئِذٍ فِي الْعَذَابِ مُشْتَرِكُونَ ﴿٣٣﴾

Basi hakika wao Siku hiyo katika adhabu ni wenye kushirikiana.

 

إِنَّا كَذَٰلِكَ نَفْعَلُ بِالْمُجْرِمِينَ ﴿٣٤﴾

Hakika hivyo ndivyo Tuwafanyavo wakhalifu.

 

إِنَّهُمْ كَانُوا إِذَا قِيلَ لَهُمْ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا اللَّـهُ يَسْتَكْبِرُونَ ﴿٣٥﴾

Hakika wao walipokuwa wakiambiwa: “Laa ilaaha illa Allaah”, Hapana Muabudiwa wa haki ila Allaah, hutakabari. [Asw-Swaaffaat 37: 33-35]

 

Na pia Anasema (Subhaanahu wa Ta'aalaa) katika Hadiyth Al-Qudsiy:

 

عنْ ابي هريرة رضي الله عنه أنَّه صلَّى الله عليه وسلَّم قال: ((قال الله تعالى: أنا أغْنى الشُّركاء عن الشِّرْك، فمَن عمل عملاً أشْرَك فيه معي غيري تركتُه وشِرْكه))    

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam amesema: ((Allaah Ta’aalaa Anasema: "Mimi Ni Mwenye kujitosheleza kabisa, Sihitaji msaada wala mshirika. Kwa hiyo, yule afanyaye amali kwa kunishirikisha na mtu, Nitaikanusha pamoja na mshirika wake.”  Yaani: hatopata ujira wowote kwa amali hiyo. [Muslim (2985), Ibn Maajah (4202)]

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni Al-Mutakabbir: Yeye ni Mwenye kustahiki kiburi chote na utukufu wote kutoka kwa waja Wake.

 

 

Faida, Mafunzo Tuyapatayo Na Jinsi Ya Kufanyia Kazi Jina Hili La Allaah; Al-Mutakabbir:

 

1. Mtukuze Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa kumkabbir (Allaahu Akbar!) Muadhimishe kwa kila taadhima na ujalali. Kumbuka kwamba Yeye Ndiye Al-Mutakabbir, Mwenye ukubwa na uadhama, na Mwenye kustahiki kutakabari. Anasema katika Hadiyth Al-Qudsiy:

 

أنا الجبَّارُ أنا المُتكبِّرُ أنا الملِكُ أنا العزيزُ أنا الكريمُ

((Mimi ni Al-Jabbaar, Mimi ni Al-Mutakabbir, (Mwenye ukubwa na utukufu) Mimi ni Al-Maalik (Mfalme), Mimi ni Al-’Aziyz (Mwenye Enzi ya nguvu Asiyeshindika), Mimi ni Al-Kariym (Mkarimu, Mtukufu)) [Swahiyh Ibn Hibbaan (7327) na Taz. As-Silsilah Asw-Swahiyhah (7/596)]  

 

2. Kutakabari kulikuwa ni maasi ya kwanza yaliyotendwa na Ibliys laana ya Allaah iwe juu yake alipokataa kutii amri ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kama ilivyokuja katika Qur-aan:

وَإِذْ قُلْنَا لِلْمَلَائِكَةِ اسْجُدُوا لِآدَمَ فَسَجَدُوا إِلَّا إِبْلِيسَ أَبَىٰ وَاسْتَكْبَرَ وَكَانَ مِنَ الْكَافِرِينَ ﴿٣٤﴾

Na pale Tulipowaambia Malaika: “Msujudieni Aadam.” Wakasujudu isipokuwa Ibliys alikataa na akatakabari na akawa miongoni mwa makafiri. [Al-Baqarah 2: 34]

 

Kwa hiyo tahadhari Muislamu usije kupinga amri za Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na Rasuli Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ukawa miongoni mwa wanaotakabari.

 

3. Tahadhari pia kutokupinga haki na kujiepusha na sifa hiyo ya kutakabari kwa sababu kutakabari ni sababu mojawapo ya kupigwa chapa katika nyoyo. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

الَّذِينَ يُجَادِلُونَ فِي آيَاتِ اللَّـهِ بِغَيْرِ سُلْطَانٍ أَتَاهُمْ ۖ كَبُرَ مَقْتًا عِندَ اللَّـهِ وَعِندَ الَّذِينَ آمَنُوا ۚ كَذَٰلِكَ يَطْبَعُ اللَّـهُ عَلَىٰ كُلِّ قَلْبِ مُتَكَبِّرٍ جَبَّارٍ ﴿٣٥﴾

Wale wanaobishana kuhusu Aayaat za Allaah bila ya hoja yoyote kuwafikia, ni chukizo kubwa mno mbele ya Allaah na mbele ya wale walioamini. Hivyo ndivyo Allaah Anavyopiga chapa juu ya kila moyo wa mwenye kutakabari, jabari.  [Ghaafir 40: 35]

 

4. Ukitaka ukubwa, basi jifanye  mnyenyekevu na dhalili mbele ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na mbele ya watu kwani hivyo ndio sababu ya kupandishwa daraja:

 

((وَمَا تَوَاضَعَ أَحَدٌ لِلَّهِ إِلاَّ رَفَعَهُ اللَّهُ عَزَّ وَ جَلَّ)) مسلم

Na yeyote hanyenyekei kwa ajili ya Allaah isipokuwa, Allaah  (‘Azza wa Jalla) Atampandisha Daraja [Atamtukuza])) [Muslim]

 

5. Jiepushe na kibri hata iwe ndogo vipi kwa sababu kuwa na kibri ni kuharamika kuingia Jannah!

 

عَنْ عَبْدِ اللَّهِ بْنِ مَسْعُودٍ (رضي الله عنه) عَنْ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ: ((لاَ يَدْخُلُ الْجَنَّةَ مَنْ كَانَ فِي قَلْبِهِ مِثْقَالُ ذَرَّةٍ مِنْ كِبْر)) مسلم

Imepokelewa kutoka kwa ‘Abdullaah bin Mas’uwd (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: Hatoingia Jannah ambaye moyoni mwake mna kiburi uzito wa chembe (au sisimizi)). [Muslim]

 

6. Usidharau wenzako kwa vyovyote vile kwani wanaweza wao kuwa ni bora mbele ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kuliko wewe hata kama una sifa nzuri zaidi ya wenzako; ikiwa ni wingi wa mali, au uzuri wa sura au mwili, au ubora wa kabila au cheo kikubwa, au ‘ilmu zaidi, au umaarufu na kadhaalika. Anatahadharisha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا يَسْخَرْ قَوْمٌ مِّن قَوْمٍ عَسَىٰ أَن يَكُونُوا خَيْرًا مِّنْهُمْ وَلَا نِسَاءٌ مِّن نِّسَاءٍ عَسَىٰ أَن يَكُنَّ خَيْرًا مِّنْهُنَّ ۖ  

Enyi walioamini! Wanaume wasiwafanyie dhihaka na kudharau wanaume wengineo asaa wakawa bora kuliko wao, wala wanawake kwa wanawake wengineo, asaa wakawa bora kuliko wao.  [Al-Hujuraat 49: 11]

 

7. Muombe Al-Mutakabbir Akuondoshee sifa mbaya ya kutakabari na kuwa na kiburi. Nabiy Muwsaa ('Alayhis-Salaam) Alimuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَقَالَ مُوسَىٰ إِنِّي عُذْتُ بِرَبِّي وَرَبِّكُم مِّن كُلِّ مُتَكَبِّرٍ لَّا يُؤْمِنُ بِيَوْمِ الْحِسَابِ ﴿٢٧﴾

Na Muwsaa akasema: “Hakika mimi najikinga kwa Rabb wangu na Rabb wenu, kutokana na kila mwenye kutakabari asiyeamini Siku ya Hesabu.” [Ghaafir 40: 27]

 

 

 

Share