Kuomba Du'aa Pamoja Baada Ya Swalaah Na Kunyanyua Mikono Ni Sunnah Au Bid-ah?

 

Kuomba Du’aa Pamoja Baada Ya Swalaah Na Kunyanyua Mikono Je, Ni Sunnah Au Bid-ah?

 

www.alhidaayacom

 

 

 

SWALI:

 

assalam alaykum warahmatullah wabaraqatuh,

katika misikiti mingi tunasoma dua kwa pamoja (imam au mtu mwengine anasoma na wengine tunaitikia) jee hii ni sunna,faradhi au bidaa na kama haifai tuombe vipi baada ya swala.

Allah atuzidishie iman na mapenzi ya dini yetu wasalam

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Du'aa ni ‘ibaadah kama alivyosema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

 عن النعمان بن بشير رضي الله عنه عن النبي صلى الله عليه وسلم (( الدعاء هو العبادة (( ثم قرأ: ((وَقَالَ  رَبُّكُمُ  ادْعُونِي  أَسْتَجِبْ  لَكُمْ  إِنَّ  الَّذِينَ  يَسْتَكْبِرُونَ  عَنْ  عِبَادَتِي  سَيَدْخُلُونَ  جَهَنَّمَ  دَاخِرِينَ)) رواه الترمذي

 

Imetoka kwa An-Nu'maan bin Bashiyr (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Du'aa ni ‘ibaadah)) Kisha Akasoma: ((Na Rabb wenu Amesema: “Niombeni, Nitakuitikieni. Hakika wale wanaotakabari katika kuniabudu wataingika Jahanam wadhalilike)) [Ghaafir:60] [At-Tirmidhiy, na Shaykh Al-Albaaniy kasema kuwa ni Hasan Swahiyh katika Sunan At-Tirmidhiy]

 

Kwa hivyo inatupasa tuombe kwa kufuata njia iliyo sahihi kama tulivyopata mafunzo kutoka Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Haikuthibitika kutoka kwa Maswahaba zake kuwa alikuwa akisoma Du'aa pamoja kwa sauti na wao wakiitikia baada ya Swalaah au hata nje ya Swalaah. Kwa hiyo kufanya hivyo itakuwa ni bid'ah (uzushi), jambo ambalo linampasa Muislamu ajiepushe nalo ili abakie katika mafunzo Sahihi.

Itambulike kwamba kutenda ‘amali ambayo haimo katika mafunzo sahihi ya Dini yetu itakuwa ni amali isiyo  na thamani yoyote kwa dalili ya kauli ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

((من أحدث في أمرنا هذا ما ليس منه فهو رد))  متفق  عليه .

((Yeyote atakayezusha katika mambo yetu haya (ya Dini) ambayo hayamo kwetu basi hakitapokelewa)) [Al-Bukhaariy na Muslim]  

 

Kuomba Du'aa katika Swalaah au baada ya Swalaah tumeamrishwa katika Qur-aan na Sunnah, lakini kila mtu anatakiwa aombe pekee na sio kwa ujumla kwani hahitaji mtu kuwasiliana na Allaah (‘Azza wa Jalla) kumuomba jambo lake kupitia kwa mtu yeyote, kwa sababu Yeye  Anaitikia maombi ya muombaj na  Yuko karibu na sisi kama Anavyosema:

 

وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ ۖ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ ۖ فَلْيَسْتَجِيبُوا لِي وَلْيُؤْمِنُوا بِي لَعَلَّهُمْ يَرْشُدُونَ ﴿١٨٦﴾

186. Na watakapokuuliza waja Wangu kuhusu Mimi, basi Mimi ni Niko karibu (kwa ujuzi); Naitikia du’aa ya muombaji anaponiomba. Basi waniitikie Mimi na waniamini Mimi, wapate kuongoka.  [Al-Baqarah:186] 

 

 

Vile vile Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema kwamba Du'aa huombwa wakati mtu anaposujudu, kama ifuatavyo:

 

عن ابْنِ عَبَّاسٍ رضي الله عنهما قَالَ : قال رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ : ( أَلا وَإِنِّي نُهِيتُ أَنْ أَقْرَأَ الْقُرْآنَ رَاكِعًا أَوْ سَاجِدًا ، فَأَمَّا الرُّكُوعُ فَعَظِّمُوا فِيهِ الرَّبَّ عَزَّ وَجَلَّ ، وَأَمَّا السُّجُودُ فَاجْتَهِدُوا فِي الدُّعَاءِ فَقَمِنٌ – أي جدير وحقيق - أَنْ يُسْتَجَابَ لَكُمْ   .  مسلم

Imetoka kwa ibn 'Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) amesema: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Hakika mimi nimekatazwa kusoma Qur-aan katika kurukuu au kusujudu. Ama katika kurukuu mtukuzeni Rabb Mwenye Utukufu na Ujalali. Na Ama katika kusujudu jitahidini katika Du'aa kwani ni yakini kuwa Atakutakabalieni)) [Muslim]

 

Na aliposema tuombe du'aa katika kila baada ya Swalaah ni kuomba kila mtu pekee yake na bila ya kuinua mikono.

 

Pia baadhi ya ‘Ulamaa wameona kwamba ni baada ya tashahhud na kabla ya kutoa salaam.

 

 

Kunyanyuka mikono katika du’aa inakubalika katika hali fulani ya kuomba du’aa kama vile katika Swalaah ya Istisqaa (Swalaah ya kuomba mvua), pia sehemu  kama Swafaa na Marwah, ‘Arafah, Muzdalifah, Jamaraat (baada ya  kurusha vijiwe kwenye nguzo) n.k.  Na Hadiyth ifuatayo inathibitisha kunyanyua mikono katika du’aa:

 

عن سَلْمَانَ رضي الله عنه قَالَ : قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ : ( إِنَّ رَبَّكُمْ تَبَارَكَ وَتَعَالَى حَيِيٌّ كَرِيمٌ يَسْتَحْيِي مِنْ عَبْدِهِ إِذَا رَفَعَ يَدَيْهِ إِلَيْهِ أَنْ يَرُدَّهُمَا صِفْرًا  ((  أبي داود"، وصححه الشيخ الألباني   

Kutoka kwa Radhwiys ambaye amesema: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Hakika Rabb wenu Tabaaraka wa Ta’aalaa Yuhai na Mkarimu Anasitahi kwa mja Wake anapoinua mikono yake (kumuomba) Airudishe sifuri)) (bila ya kumjibu) [Abuu Daawuwd na ameipa daraja ya Swahiyh Shaykh Al-Albaani ]  

 

 

‘Ulamaa wameona kwamba pale panapo dalili kwamba inaruhusiwa kunyanyua mikono katika kuomba du’aa basi hakuna kosa.

 

 

Na hivyo katika shida zake mtu anazotaka kumuomba Rabb wake, anaweza kunyanyua mikono kutokana na Hadiyth iliyotangulia kutajwa juu.

 

Kisha vile kutokana na Hadiyth iliyopokelewa na Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu 'anhu):

 

 

((Mtu aliyekwenda safarini akachoka na kujaa vumbi, kisha akanyanyua mikono juu na kuomba "Ee Rabb, Ee Rabb” lakini chakula chake ni haramu, kinywaji chake ni haramu na mavazi yake ni haramu, amerutubishwa kwa haramu, vipi atatakabliwa?)) [Muslim]

 

 

Hadiyth hii inaonyesha kwamba mtu huyo alikuwa akiomba kwa Allaah ('Azza wa Jalla) shida zake na huku amenyanyua mikono.   

 

Bonyeza viungo vifuatavyo upate manufaa zaidi:

 

 

Hadiyth Kuhusu Kuomba Du’aa Pamoja Baada Ya Swalaah Ni Swahiyh Au Dhaifu?

 

 

Kusoma Du’aa Pamoja Baada Ya Swalaah na Kuomba Du’aa Baada ya Mihadhara

 

 

025-Hiswnul-Muslim: Nyiradi Baada Ya Kutoa Salaam Ya Kumaliza Swalaah

 

 

Na Allaah Anajua zaidi  

 

 

Share