22-Fadhila Za Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم): Rasuli Pekee Ambaye Allaah Ameahidi Kuhifadhi Kitabu Chake Al-Qur-aan

Fadhila Za  Nabiy  (صلى الله عليه وآله وسلم)

22-Rasuli Pekee Ambaye Allaah Ameahidi Kuhifadhi Kitabu Chake Al-Qur-aan

www.alhidaaya.com

 

 

Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ameteremshiwa Kitabu cha mwisho ambacho ni Qur-aan ambayo haibadiliki wala haiwezekani kugeuzwa wala kupotoshwa mpaka Siku ya Qiyaamah, kinyume na Vitabu vya awali ambayo vimepotoshwa kwa kubadilishwa, kupugunzwa na kuongezwa maneno yasiyokuwa ya Allaah ('Azza wa Jalla). Basi Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ameahidi Mwenyewe kuihifadhi Qur-aan kama Anavyosema: 

 

إِنَّا نَحْنُ نَزَّلْنَا الذِّكْرَ وَإِنَّا لَهُ لَحَافِظُونَ

Hakika Sisi Tumeteremsha Adh-Dhikra (Qur-aan) na hakika Sisi bila shaka ndio Wenye kuihifadhi. [Al-Hijr: 9]

 

Ama Vitabu vya awali, Allaah Aliwaachia Wanazuoni wa Ahlul-Kitaabi wahifadhi kama Anavyosema:

 

 

إِنَّا أَنزَلْنَا التَّوْرَاةَ فِيهَا هُدًى وَنُورٌ ۚ يَحْكُمُ بِهَا النَّبِيُّونَ الَّذِينَ أَسْلَمُوا لِلَّذِينَ هَادُوا وَالرَّبَّانِيُّونَ وَالْأَحْبَارُ بِمَا اسْتُحْفِظُوا مِن كِتَابِ اللَّـهِ وَكَانُوا عَلَيْهِ شُهَدَاءَ ۚ فَلَا تَخْشَوُا النَّاسَ وَاخْشَوْنِ وَلَا تَشْتَرُوا بِآيَاتِي ثَمَنًا قَلِيلًا ۚ وَمَن لَّمْ يَحْكُم بِمَا أَنزَلَ اللَّـهُ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الْكَافِرُونَ ﴿٤٤﴾

Hakika Tumeteremsha Tawraat humo mna mwongozo na nuru; ambayo kwayo, Nabiy waliojisalimisha (kwa Allaah), waliwahukumu Mayahudi. Na (kadhalika) wanachuoni waswalihina na wanachuoni mafuqahaa wa dini kwa sababu waliyokabidhiwa kuhifadhi Kitabu cha Allaah; na wakawa mashahidi juu yake. Basi msiwaogope watu, bali Niogopeni Mimi, na wala msibadilishe Aayaat Zangu kwa thamani ndogo. Na yeyote asiyehukumu kwa yale Aliyoyateremsha Allaah, basi hao ndio makafiri. [Al-Maaidah: 44]

 

Lakini haikuwezekana kuhifadhika bali vimepotoshwa kwa kupunguzwa na kugeuzwa na kuongezwa, na dalili kadhaa zimethibiti miongoni mwazo ni Kauli za Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa):

 

وَإِنَّ مِنْهُمْ لَفَرِيقًا يَلْوُونَ أَلْسِنَتَهُم بِالْكِتَابِ لِتَحْسَبُوهُ مِنَ الْكِتَابِ وَمَا هُوَ مِنَ الْكِتَابِ وَيَقُولُونَ هُوَ مِنْ عِندِ اللَّـهِ وَمَا هُوَ مِنْ عِندِ اللَّـهِ وَيَقُولُونَ عَلَى اللَّـهِ الْكَذِبَ وَهُمْ يَعْلَمُونَ ﴿٧٨﴾

Na hakika miongoni mwao kuna kundi wanaopotosha Kitabu kwa ndimi zao (wanaposoma) ili mdhanie kuwa hayo ni yanayotoka katika Kitabu, na hali hayo si yenye kutoka katika Kitabu, na wanasema: Hayo ni kutoka kwa Allaah; na hali hayo si kutoka kwa Allaah na wanamsingizia uongo Allaah na wao wanajua. [Aal-‘Imraan: 78]

 

Na,

 

فَوَيْلٌ لِّلَّذِينَ يَكْتُبُونَ الْكِتَابَ بِأَيْدِيهِمْ ثُمَّ يَقُولُونَ هَـٰذَا مِنْ عِندِ اللَّـهِ لِيَشْتَرُوا بِهِ ثَمَنًا قَلِيلًا ۖ فَوَيْلٌ لَّهُم مِّمَّا كَتَبَتْ أَيْدِيهِمْ وَوَيْلٌ لَّهُم مِّمَّا يَكْسِبُونَ ﴿٧٩﴾

Basi ole kwa wale wenye kuandika kitabu kwa mikono yao; kisha wakasema: Hiki ni kutoka kwa Allaah ili wabadilishe kwa thamani ndogo. Basi ole wao kwa yale yaliyoandikwa na mikono yao, na ole wao kwa yale wanayoyachuma. [Al-Baqarah: 79]

 

 Na,

 

وَمَا قَدَرُوا اللَّـهَ حَقَّ قَدْرِهِ إِذْ قَالُوا مَا أَنزَلَ اللَّـهُ عَلَىٰ بَشَرٍ مِّن شَيْءٍ ۗ قُلْ مَنْ أَنزَلَ الْكِتَابَ الَّذِي جَاءَ بِهِ مُوسَىٰ نُورًا وَهُدًى لِّلنَّاسِ ۖ تَجْعَلُونَهُ قَرَاطِيسَ تُبْدُونَهَا وَتُخْفُونَ كَثِيرًا ۖ وَعُلِّمْتُم مَّا لَمْ تَعْلَمُوا أَنتُمْ وَلَا آبَاؤُكُمْ ۖ قُلِ اللَّـهُ ۖ ثُمَّ ذَرْهُمْ فِي خَوْضِهِمْ يَلْعَبُونَ ﴿٩١﴾

Na hawakumkadiria Allaah kama inavyostahiki kumkadiria, pale waliposema: Allaah Hakuteremsha chochote kwa mtu. Sema: Nani aliyeteremsha Kitabu ambacho amekuja nacho Muwsaa, (chenye) nuru na mwongozo kwa watu. Mnakifanya kurasa kurasa mkizifichua na mkificha mengi. [Al-An’aam: 91]

 

Na,

 

أَفَتَطْمَعُونَ أَن يُؤْمِنُوا لَكُمْ وَقَدْ كَانَ فَرِيقٌ مِّنْهُمْ يَسْمَعُونَ كَلَامَ اللَّـهِ ثُمَّ يُحَرِّفُونَهُ مِن بَعْدِ مَا عَقَلُوهُ وَهُمْ يَعْلَمُونَ ﴿٧٥﴾

Je, mnatumai kwamba watakuaminini na hali lilikuwa kundi miongoni mwao linasikia maneno ya Allaah kisha linayageuza baada ya kuyaelewa na hali wanajua? [Al-Baqarah: 75]

 

Na,

 

فَبِمَا نَقْضِهِم مِّيثَاقَهُمْ لَعَنَّاهُمْ وَجَعَلْنَا قُلُوبَهُمْ قَاسِيَةً ۖ يُحَرِّفُونَ الْكَلِمَ عَن مَّوَاضِعِهِ ۙ وَنَسُوا حَظًّا مِّمَّا ذُكِّرُوا بِهِ ۚ  

Kwa sababu ya kuvunja kwao fungamano lao, Tuliwalaani na Tukazifanya nyoyo zao kuwa ngumu. Wanageuza maneno (ya Allaah) kutoka mahali pake, na wakasahu sehemu ya yale waliyokumbushwa.  [Al-Maaidah: 13]

 

 Na dalili mojawapo katika Hadiyth:  

 

عَنْ  إبن عَبَّاسٍ رضى الله عنهما قَالَ: كَيْفَ تَسْأَلُونَ أَهْلَ الْكِتَابِ عَنْ شَىْءٍ، وَكِتَابُكُمُ الَّذِي أُنْزِلَ عَلَى رَسُولِ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم أَحْدَثُ، تَقْرَءُونَهُ مَحْضًا لَمْ يُشَبْ وَقَدْ حَدَّثَكُمْ أَنَّ أَهْلَ الْكِتَابِ بَدَّلُوا كِتَابَ اللَّهِ وَغَيَّرُوهُ وَكَتَبُوا بِأَيْدِيهِمُ الْكِتَابَ وَقَالُوا هُوَ مِنْ عِنْدِ اللَّهِ‏ لِيَشْتَرُوا بِهِ ثَمَنًا قَلِيلاً،  

 

Ibn ‘Abbaas (رضي الله عنهما) amesema: “Kwanini mnawauliza Ahlul-Kitaab jambo lolote ilhali Kitabu chenu ambacho kimeteremshwa kwa Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) ni kipya (na cha karibuni)? Mnakisoma kikiwa ni kisafi, hakikupotoshwa wala kubadilishwa. Na mmeshajulishwa (na Allaah) kwamba Ahlul-Kitaab wamebadilisha Vitabu vya Allaah na wakavigeuza na wakaandika kwa mikono yao Kitabu wakasema “Hiki ni kutoka kwa Allaah ili wabadilishe kwa thamani ndogo.’”    [Al-Bukhaariy Kitaab Al-I’tiswaam Bil-Kitaabi Was-Sunnah]

 

Share