Mume Kaahidi Kutoa Talaka (Tatu) Ikiwa Mke Alifanya Zinaa Kabla Au Baada Ya Kumuoa Naye Mke Amefanya Zinaa Lakini Ameficha

 

SWALI:

Ikiwa mtu kamwambia mkewe ikiwa umefanya zinaa kabla au baada ya kukuoa basi nimekupa talaka tatu, na huyo mwanamke amefanya lakini anaficha vipi na mume anashaka nae vipi hukumu yake?


JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu mume kutoa talaka ya sharti.

Hii inaitwa katika sheria Atw-Twalaaq al-Mu‘allaq (yaani talaka inayo ningi’nia). Inaning’inia kwa ajili ya sharti ambayo mume ameiweka. Jambo hilo likitokea basi talaka itakuwa imepita. Na kwa hali yako hii ni mfano wa hilo, kwani mumeo amesema ikiwa umefanya zinaa kabla au baada ya kukuoa basi wewe utakuwa umeachwa.

Ikiwa kweli utakuwa umefanya zinaa kabla au baada ya kukuoa basi moja kwa moja utakuwa umeachika. Na kwa kuwa wewe ndio unajua hali yako kama ulizini au umezini sasa utakuwa umeachika na kumficha mumeo hilo utakuwa unapata dhambi kwani mtakuwa mnazini na wewe ndiye mwenye kujua hilo.

Inatakiwa usifiche tena hilo bali mkae na mumeo na umwambie uhakika wa hilo suala na umuombe msamaha kuwa umefanya hilo kwa sababu moja au nyingine lakini umejirekebisha sasa.

Talaka tatu zinazotolewa wakati mmoja huhesabiwa kuwa ni talaka moja tu kwa kauli sahihi zaidi, hivyo mna nafasi ya kurudiana tena. Na lau mume ataona kuwa hataki kuwa na wewe tena basi Mwenyezi Mungu Yupo na unaweza kupata mume mwengine mzuri zaidi kuliko huyo aliyekuachana.

Ingia katika viungo vifuatavyo upate maelezo zaidi

Mas-ala Ya Talaka Mbali Mbali

Talaka Tatu Pamoja Inakubalika? Mume Hatimizi Zamu Kisha Ametoa Talaka Mara Tatu Kwa Pamoja

Talaka Ziko Aina Ngapi Na Wakati Gani Zinasihi?

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share