Zingatio: Kizazi Kinapotea Kwa Maisha Ya Ulaya Na Marekani

Zingatio: Kizazi Kinapotea Kwa Maisha Ya Ulaya Na Marekani

 

 Naaswir Haamid

 

Alhidaaya.com

 

 

Shaykh Ibn Al-'Uthaymiyn anasema: ‘Hakuna ruhusa ya kuhama kuelekea nchi za Kikafiri isipokuwa kwa masharti matatu: Awe na elimu ya diyn itakayomzuia kupotoka, awe na msimamo wa diyn utakaomzuia kuhadaika na awe ni mwenye kulazimika kwa hilo analoendea.’

 

Hakuna shaka yoyote kwamba, makundi mengi ya Waislamu yanayokimbilia Ulaya na Marekani hayajatimiza masharti hayo yaliyotajwa hapo juu.

 

Kinachotafutwa huko nacho kimegawika kwenye makundi matatu: rizki, elimu na maisha. Kwa bahati mbaya, pongezi hutolewa kwa yule aliyehamia Magharibi na kudharauliwa aliyeacha nafasi ya kwenda huko.

 

Waungwana wanasema: ‘Kawia ufike kuliko kulala njiani’ haraka hizo za nini kuelekea Majuu hali ya kuwa baadhi yao wana maisha mazuri ndani ya nchi zao walizozaliwa? Basi iwapo Muislamu anashikilia msimamo wake wa kuparamia huko Majuu kwa hoja zisizo na maana, ni vyema tumkumbushe maneno ya Wahenga: "Mwenye pupa hadiriki kula tamu’.

 

Kwa hakika athari mbaya nyingi tumezishuhudia kwa vijana wetu kuondoka mijini wakaenda huko Magharibi. Wapo mashababu ambao walikuja matembezini katika nchi zao za asili wakiwa wamevaa vidani na wasichana wamevaa nguo zilizochupa juu ya magoti na wengine hadi kuonyesha vitovu vyao. Hali sio hiyo tu, wale baadhi ya mashekhe na maustadhi wetu waliohamia huko, nao kwa masikitiko makubwa wameelemewa na dunia wakaigawa diyn yao bure!

 

Mzee naye kwa upande wake anamuhimiza mwanawe kwenda nchi za Kimagharibi, mara nyengine mzee anadiriki kumdhamini na kumpatia kila anachokihitajia kwa lengo la kumfikisha mwanawe Ulaya au Marekani. Uhuru anaopatiwa huko unamfanya awe kama mwehu wa kutimiza shahwa zake, kila kinachotendwa katika ardhi hizo za Magharibi anakiona ndio ustaarabu. Ndio sababu hata kina mama kushindwa kutembea na mabinti zao pale wanapozuru miji yao ya asili. Maana afadhali mama mtu atajiheshimu, lakini kwa binti zake, ni kinyago.

 

Uhamiaji wa nchi za Kimagharibi bila ya dharura nzito ni dhulma ya nafsi. Kwani Muislamu hatakuwa huru kutekeleza masharti ya diyn yake vile inavyotakiwa. Qur-aan inatupatia mjadala wa kuhama (hijrah) baina ya Malaika na watu wa motoni baada ya kutolewa roho zao:

 

إِنَّ الَّذِينَ تَوَفَّاهُمُ الْمَلَائِكَةُ ظَالِمِي أَنفُسِهِمْ قَالُوا فِيمَ كُنتُمْ ۖ قَالُوا كُنَّا مُسْتَضْعَفِينَ فِي الْأَرْضِ ۚ قَالُوا أَلَمْ تَكُنْ أَرْضُ اللَّـهِ وَاسِعَةً فَتُهَاجِرُوا فِيهَا ۚ فَأُولَـٰئِكَ مَأْوَاهُمْ جَهَنَّمُ ۖ وَسَاءَتْ مَصِيرًا ﴿٩٧﴾

97. Hakika wale ambao Malaika wamewafisha, hali wamejidhulumu nafsi zao; (Malaika) watawaambia: Mlikuwa katika hali gani?  Watasema: Tulikuwa tukikandamizwa katika ardhi.  (Malaika) Watasema: Je, kwani ardhi ya Allaah haikuwa ya wasaa mkahajiri? Basi hao makazi yao yatakuwa ni Jahannam, na uovu ulioje mahali pa kuishia. [An-Nisaa: 97]

 

Waislamu tufunuke macho na tuelekee kule kilipo Qiblah chetu, nacho kipo Makkah hakipo Marekani. Leo Waislamu wanakimbia jivu wanatumbukia kwenye moto. Akili zimeruka kwa Ulaya badala ya kufikiria kwenda Hijjah na kutenda ya maana.

 

Tukumbuke kwamba kila hatua na maamuzi tunayofanya tunatakiwa tuegemeze kwenye Uislamu wetu. Awali ya yote, ni Uislamu wetu. Hivyo, sio vyema kwa Muislamu kuacha mji wake ambao unampatia nafasi ya kumuabudu Rabb wake kwa wasaa na akaelekea miji ambayo fitna imejaa na  utekelezaji wa ‘Ibaadah zake si kwa wepesi na wasaa. 

 

Share