Fadhila Za Siku Ya ‘Arafah, Sababu Zake Na Tofauti Ya Nyakati Baina Ya Nchi

 

Fadhila Za Siku Ya ‘Arafah, Sababu Zake Na Tofauti Ya Nyakati Baina Ya Nchi

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali La Kwanza:

 

 

Assalam Alaykum,

 

Alhamdulillah leo nimemtumia msg swahiba wang kuhusu Arafah kwamba afunge siku ya Alhamis sawa na mwezi9 wa saudia,akanjib kua Nabiy amefunga mwez 9 wala si siku ya Arafah nkamuliza nini lengo la kufunga si kuungana na mahujaji? akanjib Nabiy amefunga Arafah kwa lengo la kukutana Adam na Hawaa na kuchinja mwezi 10 kwa lengo la Nabiy Ibrahim kabla ya kufaradhishwa Hijjah, akasema amemskia shekh maneno ayo huku shekh amestadil hadiyth ya bi Aisha swahiba wng akaniuliza je kama lengo la Arafah ni kungana na waislam makkah kuna mchi kama marekan hadi linazama jua la mchana wa Arafah wao markan ni usiku au Australia ni sa5 za usiku je enyi mashekh zang wana Alhidaaya haya nikweli?mm nkafanya bahthi kwenye alhidaaya sjaona sehem inayosema kua Nabiy amesema watu wafunge mwez9 au siku ya Arafah?nime search kwenye Arafah nkaona fadhila za siku ya arafah sio lini wafunge arafah je ni siku au kisimamo? nimeonelea ntumie email hii ili npate majibu haraka kwan siku ya alhamis haiko mbali ningetumia email ya masuala nngechelewa kujibiwa labda kwa kutoliona hili mapema. Rabb awazidishien kwa kuwaelimisha Ummah

 

 

Swali La Pili:

 

Katika hii dunia tumetofautiana kimasaa utakuta nchi moja hadi nyingine wametofautiana masaa 8 hadi 12. Je inakuwaje pale watu wanakuwa kwenye viwanja vya arafa na wao unakuta wapo nyuma kimasaa?

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Maana ya ‘Arafah ni jina la Jabali lilioko mji wa Makkah ambalo alisimama Nabiy Swalla Allaahu 'alayhi wa  aalihi wa sallam) kuwahutubia Maswahaba alipotekeleza Hajj yake ya mwisho. Na hiyo ndio nguzo mojawapo kuu ya Hijjah bila ya kuweko hapo mwenye kuhiji atakuwa hakutimiza hijja yake kama tunavyopata dalili katika Hadiyth ifuatayo:

 

عن عبد الرحمن بن يعمر قال: قال رسول الله صلى الله عليه وسلم:  ((الحج عرفة ، من جاء قبل طلوع الفجر من ليلة جمع فقد أدرك الحج))  صحيح الجامع   

Kutoka kwa ‘Abdur-Rahmaan bin Ya’mur ambaye amesema Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam: ((Al-Hajj ni ‘Arafah, atakayekuja kabla kutoka Alfajiri usiku wa kujumuika atakuwa ameipata Hajj)) [Swahiyh Al-Jaami’]

 

Mwezi wa tisa katika kalenda ya Kiislamu ni mwezi wa Ramadhwaan ambao umefaridhiswa Swawm kama tunavyojua sote. Sasa hatuelewi muulizaji amekusudia nini.  Ama ikiwa  ni tarehe 9 ya Dhul-Hijjah, basi hiyo ndiyo siku ya ‘Arafah  na ni siku ambayo mahujaji wanakusanyika wote hapo kutimiza nguzo hii kuu ya Hijjah. Na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) hakufunga Swawm siku hiyo kwa dalili iliyo wazi kabisa.

 

عن ميمونة بنت الحارث: أن الناس شكوا في صيام النبي صلى الله عليه وسلم يوم عرفة ، فأرسلت إليه بحلاب ، وهو واقف في الموقف ، فشرب منه والناس ينظرون" البخاري

Kutoka kwa Maymuunah bint Al-Haarith (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba watu walitia shaka na Swawm ya Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)   [kama alifunga] Siku ya ‘Arafah, nikampelekea maziwa, naye akiwa amesimama akayanywa na huku watu wanamtazama”  [Al-Bukhaariy]

 

 

Kwa hiyo hakuna hukmu ya Swawm siku ya ‘Arafah kwa mahujaji. Bali Swawm ya siku hiyo ni kwa Waislamu wasiojaaliwa kuweko siku hiyo ‘Arafah kwa ajili nao wapate fadhila za siku hiyo tukufutu ambayo Swawm yake ni kufutiwa madhambi ya miaka miwili kama tunavyopata dalili katika Hadiyth ifuatayo:

 

عَنْ أَبِي قَتَادَةَ رضي الله عنه أن النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ :  ((صِيَامُ يَوْمِ عَرَفَةَ أَحْتَسِبُ عَلَى اللَّهِ أَنْ يُكَفِّرَ السَّنَةَ الَّتِي قَبْلَهُ وَالسَّنَةَ الَّتِي بَعْدَهُ )) أخرجه مسلم

Imetoka kwa Abu Qataadah (Radhwiya Allaahu 'anhu) ambaye amesema: Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kasema: "Swawm ya 'Arafah nataraji (kwa Allaah) kufuta madhambi ya mwaka uliopita na wa baada yake." [Muslim]

 

 

Fadhila nyinginezo zinapatikana katika kiungo kifuatacho:

 

 

 Fadhila Za Siku Ya 'Arafah Na Yawmun-Nahr (Siku Ya Kuchinja)

 

Ama kuhusu tofauti ya masaa baina ya nchi na nchi, inampasa Muislamu aamini Aayah na Hadiyth zinazoeleza mas-alah haya bila ya kutilia shaka au kujaribu kuzipinda. Hii ndio ‘Aqiydah sahihi ya Ahlus-Sunnah wal-Jamaa’ah.  

 

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa):

 

إِنَّ فِي خَلْقِ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ وَاخْتِلَافِ اللَّيْلِ وَالنَّهَارِ لَآيَاتٍ لِّأُولِي الْأَلْبَابِ ﴿١٩٠﴾ 

Hakika katika kuumbwa mbingu na ardhi, na mabadiliko ya mfuatano wa usiku na mchana; bila shaka ni Aayaat (ishara, zingatio) kwa wenye akil [Aal-‘Imraan: 190]

 

Bila shaka kuna hikma yake ya kuwa nchi zote ulimwenguni zikhitilafiane kwa wakati. Ikiwa Kusini au Magharibi mwa dunia ni asubuhi, Kaskazini au Mashariki ya dunia kuwe ni usiku. Hii inaonyesha pia Rehma za Allaah kwa waja Wake kutokuwatia katika mashaka, Naye Ndiye Aliyeumba mbingu na ardhi kwa namna yake ya mzunguko wa ardhi, jua na mwezi. Na Ndiye Mwenye kudhibiti mizunguko hiyo. Hivyo Aliyoyaumba yote ni kwa ajili ya manufaa ya binaadamu wote ulimwenguni. Na Anapotoa hukmu fulani basi tutambue kwamba ina hikma yake na tuwe wenye kusikia na kutii bila ya kutilia shaka.

 

Na kuamini huku ni sawa na kuamini kuteremka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) thuluthi ya mwisho ya usiku katika mbingu ya kwanza:

 

 

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُ أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ: ((يَنْزِلُ رَبُّنَا تَبَارَكَ وَتَعَالَى كُلَّ لَيْلَةٍ إِلَى السَّمَاءِ الدُّنْيَا حِينَ يَبْقَى ثُلُثُ اللَّيْلِ الْآخِرُ يَقُولُ: مَنْ يَدْعُونِي فَأَسْتَجِيبَ لَهُ مَنْ يَسْأَلُنِي فَأُعْطِيَهُ مَنْ يَسْتَغْفِرُنِي فَأَغْفِرَ لَهُ)) البخاري و مسلم  

Imetoka kwa Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Allaah Tabaaraka wa Ta’aalaa Huteremka (kwa namna inavyolingana na utukufu Wake) kila siku katika mbingu ya dunia (mbingu ya kwanza) inapobakia thuluthi ya mwisho ya usiku na Husema: Nani ananiomba Nimtakabalie? Nani Ana shida Nimtekelezee? Nani ananiomba maghfirah Nimghufurie?” [Al-Bukhaariy, Muslim]

 

Na hivyo kila Muislamu popote alipo ulimwenguni anaweza kupata fadhila zilotajwa katika Hadiyth hiyo ya kuamka thuluthi ya mwisho ya usiku kwa wakati wa nchi aliyoko. Haiingii akilini kwamba Mahujaji wasimame ‘Arafah Makkah wakati ni machana, na watu walioko nchi za mbali ambako kwao ni wakati wa usiku huko, nao wafunge Swawm zao usiku na hali kufunga Swawm ni kuanzia Alfajiri hadi jua kuzama kwa jua.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share