Ameugua Muda Mrefu Akatii Majini Kutekeleza ‘Ibaadah Zake, Je, ‘Ibaadah Zake Zinakubalika?

 

Ameugua Muda Mrefu Akatii Majini Kutekeleza

‘Ibaadah Zake,  Je, ‘Ibaadah Zake Zinakubalika?

 

Alhidaaya.com

 

SWALI:

 

Asalam Alaykum,

Kwa uwezo wake Allaah Karim natumai mnaendelea vizuri na shughuli za kuwaelimisha waislam.

swali langu ni kwamba Mumewangu alikuwa si mtu wa kufanya ibada bali alikuwa ni mtu wa kupenda/kutenda maovu tu. Baada ya  miaka kadhaa kupita akaugua maradhi kiasi kwamba alikuwa kama chizi hatimaye majini wakajitokeza na wakadai afanye ibada pamoja na kutibu. kutokana na kuugua kwa muda mrefu akakubali, hivi sasa anafanya ibada na anatibu Je ibada yake inaswii?

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amtuambi kuwa Allaah Hakuteremsha ugonjwa ila Ameteremsha na dawa, hivyo fanyeni dawa enyi waja wa Allaah. Na katika kauli yake nyengine akatuusia tusiwe ni wenye kufanya dawa kwa zilizo haramu.

 

Tunafahamu kuwa majini wapo na wanaweza kumdhuru mwanaadamu kwa idhini ya Allaah Aliyetukuka si kwa uwezo wao majini kabisa.

 

Hivyo, ikiwa Muislamu amekumbwa kweli na majini zipo dawa za yeye kutibiwa kwa mpango wa Sunnah ambao hautaingizwa shirki ndani.

 

Sasa kwa kuwatii hao majini mmeingia katika shirki kwani wa kuabudiwa ni Allaah Aliyetukuka peke Yake. Tufahamu sisi huwa tunamuahidi Allaah Aliyetukuka kwa kukariri mara 17 kila siku:

إِيَّاكَ نَعْبُدُ وَإِيَّاكَ نَسْتَعِينُ ﴿٥﴾

Wewe Pekee tunakuabudu na Wewe Pekee tunakuomba msaada. [Al-Faatihah: 5].

 

Na tufahamu kuwa mwenye kumshirikisha Allaah Aliyetukuka basi amali yake yote huwa ni bure.

 

Kwa hivyo, hapa mlipofika mnatakiwa mjiondoe katika dhambi hiyo kubwa -ambayo haisamehewi na Allaah Aliyetukuka- kwa kumuomba kidhati na kikweli ili Awasamehe, mjute kwa mliyofanya, mtie Niyah ya kutorudia na mfanye ‘amali nzuri. Baada ya hapo mnaweza kwenda kusomewa kisomo cha Qur-aan na Insha Allaah ugonjwa wa mumeo utaondoka.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share