Sajdatut-Tilaawa Kwa Imaam Katika Swalah Ya Sirriyah

 

SWALI:

Pindipo Imam anasalisha sala za kimya (adhuhur & L'asir) na ikatokezea kusoma sura yenye sijdat-tilaawa, jee inamlazimu asujudu, na maamuma au??

 



 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola  wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Inatakiwa ifahamike ya kwamba Imaam amewekwa ili afuatwe na maamuma. Ikiwa atakosea kwa kuwa yeye ni mwanadamu basi anafaa akumbushwe.

Mtume صلى الله عليه وآله وسلم   amesema: “Imaam amejaaliwa kufuatwa, hivyo akirukuu nanyi nendeni katika rukuu. Na akisimama wima nanyi pia mufanye hiyo na akiswali kwa kukaa nanyi pia swalini kwa kukaa” (Muslim).

Na katika Hadithi nyingine, Mtume صلى الله عليه وآله وسلم   amesema: “Hakika amewekwa Imaam ili afuatwe basi musikhalifiane naye. Akipiga takbira nanyi pigeni takbiyra. Akirukuu nanyi nendeni katika rukuu. Na anaposema "Sami'a-Allaahu liman Hamidah", nanyi semeni: "Rabbanaa walakal-Hamd". Na anaposujudu basi nanyi sujuduni na anaposwali kwa kukaa nanyi swalini nyote kwa kukaa”  (Al-Bukhariy).

Hivyo ikiwa Imaam katika Swalah za kimya atasoma Suwrah yenye sijdah ya kisomo akasujudu inabidi maamuma wamfuate.

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share