Mwanamke Kujipamba Mbele Ya Shemeji Au Wasiokuwa Maharimu Zake

 

Mwanamke Kujipamba Mbele Ya Shemeji Au Wasiokuwa Maharimu Zake

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Asalam alykum samahani saaaaaaana kwa usumbufu wowote utakaotokea kwa suali hili .

mimi nauliza nimeambiwa usioneshe mapambo yako mwanamke unapotoka sasa mimi niko ndani kwangu na nakaa na shemegi zangu au shemegi yangu na mume wangu ametoka sasamimi nikajipamba na kumsubiri mume wangu arudi kazini na kujipamba kwangu pengine ni kujitia manukato au rangi ya mdomo na nguo ambazo za stara kwa vile  muna watu nimevaa sasa mimi sipati dhambi wao wanapo niona na zile rangi usoni  na kunisikia harufu. na pia kaja mtu nnae mfaham ambae ni jamaa wa mume wangu  nikamfungulia mlango na hali nimejipamba kama hvo mwanzo pia sipati dhambi akiniona  na mimi niko kwangu

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

 

Ni amri kutoka kwa Allaah Subhaanahu wa Ta'aalaa kuwa mwanamke wa Kiislamu afiche mapambo yake ila kwa wale ambao hawezi kuolewa nao (Maharimu wake), nao wametajwa katika Aya ifuatayo:

 

وَقُل لِّلْمُؤْمِنَاتِ يَغْضُضْنَ مِنْ أَبْصَارِهِنَّ وَيَحْفَظْنَ فُرُوجَهُنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا ۖ وَلْيَضْرِبْنَ بِخُمُرِهِنَّ عَلَىٰ جُيُوبِهِنَّ ۖ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ أَبْنَائِهِنَّ أَوْ أَبْنَاءِ بُعُولَتِهِنَّ أَوْ إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي أَخَوَاتِهِنَّ أَوْ نِسَائِهِنَّ أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُهُنَّ أَوِ التَّابِعِينَ غَيْرِ أُولِي الْإِرْبَةِ مِنَ الرِّجَالِ أَوِ الطِّفْلِ الَّذِينَ لَمْ يَظْهَرُوا عَلَىٰ عَوْرَاتِ النِّسَاءِ ۖ وَلَا يَضْرِبْنَ بِأَرْجُلِهِنَّ لِيُعْلَمَ مَا يُخْفِينَ مِن زِينَتِهِنَّ ۚ وَتُوبُوا إِلَى اللَّـهِ جَمِيعًا أَيُّهَ الْمُؤْمِنُونَ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ ﴿٣١﴾

Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao na wahifadhi tupu zao, na wala wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa yale yanayodhihirika. Na waangushe khimaar (shungi) zao mpaka vifuani mwao, na wasidhihirishe mapambo yao isipokuwa kwa waume zao, au baba zao, au baba za waume wao, au wana wao wa kiume, au wana wa kiume wa waume zao, au kaka zao, au wana wa kiume wa kaka zao, au wana wa kiume wa dada zao, au wanawake wao (wa Kiislamu), au wale iliyowamiliki mikono yao ya kuume, au wafuasi wanaume wasio na matamanio ya jimai miongoni mwa wanaume au watoto ambao hawatambui kitu kuhusu sehemu za siri za wanawake. Na wala wasipige miguu yao yakajulikana yale wanayoyaficha katika mapambo yao. Na tubuni kwa Allaah nyote, enyi Waumini mpate kufaulu. [An-Nuwr:31]

 

 

Baadhi ya 'Ulamaa wamefasiri kuwa makusudio ya ila  yale yatakayodhihiri ni viganja vya mikono na uso. Lakini uso unapokuwa uko wazi haimaanishi kwamba mwanamke ajipambe kwani itakuwa hakuficha uzuri wake na hivyo atakuwa hakutekeleza amri katika aya hiyo wala amri ya Allaah Subhaanahu wa Ta'aalaa kwamba mwanamke asijishauwe kama ilivyo  katika aya ifuatayo.:

 

وَقَرْنَ فِي بُيُوتِكُنَّ وَلَا تَبَرَّجْنَ تَبَرُّجَ الْجَاهِلِيَّةِ الْأُولَىٰ ۖ

Na bakieni majumbani mwenu, na wala msionyeshe mapambo na uzuri kwa ajinabi kujishaua kama zama za ujahili. [Al-Ahzaab: 33]

 

 

Zama za ujaahiyyah (kabla ya Uislamu) wanawake  walikuwa wakijipamba na kutoka nje ili waonekane mapambo yao na wanaume na kujishauwa kwao.

 

 

Shemeji zako si miongoni mwa waliotajwa katika Aayah hiyo ya kwanza, kwa hiyo wao sio Mahram wako (wao wanaweza kukuoa). Hali kadhalika jamaa za mume wako unaowafahamu nao sio Mahram wako.

 

 

Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) aliulizwa kuhusu shemeji na majibu yalikuwa kwamba shemeji ndio khaswa hatari kubwa kwa mke wa ndugu yake:

 

إياكم والدخول على النساء، قالوا: يا رسول الله أرأيت الحمو؟ قال: الحمو الموت متفق عليه

((Tahadharini kuwaingilia (kuingia majumbani mwao) wanawake)) Wakasema: Ee Rasuli wa Allaah, je, vipi kuhusu shemeji? Akasema: ((Shemeji ni mauti)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

 

Hadiyth hii ya Nabiy Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam inatufahamisha kuwa shemeji ni khatari zaidi kuchanganyika naye, kwani kawaida shemeji anakuwa ana ukaribu zaidi na mke wa ndugu yake na huenda mara moja akapata huruma na mapenzi na wakaingia kwenye uharamu, kisha mwisho wake ndoa ikaharibika. Na jambo hili limeshawahi kutokea katika mujtamaa (jamii) wetu na nyinginezo.

 

 

Sasa ikiwa ni khatari kuchanganyika na shemeji kwa sababu hizo tulizozitaja, seuze tena mwanamke aongeze fitna kwa kujipamba kwa rangi za midogo, podari na manukato.

 

 

Kwanza tujue kuwa manukato ndio khatari zaidi kujipaka mwanamke mbele ya mwanamume yeyote kwani manukato haraka humfanya mwanamume avutiwe na kupata matamanio ya kumkaribia aliyepaka hayo manukato, na ndio maana Nabiy Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam amekataza mwanamke asitoke kwenda msikitini akiwa ana manukato katika Hadiyth zifuatazo: 

 

Hadiyth ya kwanza:

 

أيما امرأة استعطرت فمرّت بقوم ليجدوا ريحها فهي زانية. رواه الإمام أحمد وغير

((Mwanamke yeyote atakayejitia manukato akapita mbele ya watu wakapata harufu yake basi atakuwa amezini)) [Ahmad na wengineo]

 

 

Hadiyth ya pili:

((إذا شهدت إحداكن العشاء فلا تطيب تلك الليلة)) . رواه مسلم

((Mmoja wenu (wanawake) atakapokuja kuhudhuria Swalaah ya 'Ishaa basi asijitie manukato usiku huo)) [Muslim]

 

Hadiyth ya tatu:

 

((إذا شهدت إحداكن المسجد فلا تمسَّ طيبا))  رواه مسلم

((Anapokwenda msikitini mmoja wenu katika wanawake, basi asiguse (asipake) manukato)) [Muslim]

 

Hadiyth ya nne:

 

Abuu Huraryah Radhwiya 'anhu amesimulia Hadiyth kuwa Nabiy Swalla Allaahu alayhi wa aalihi wa sallam alimrudisha mwanamke ambaye alikuwa anakwenda msikitini kuswali akiwa amejitia manukato arudi nyumbani na aoge josho (ghuslu) la janaba. [Imaam Ahmad na Abuu Daawuwd, na Al-Albaaniy amesema kuwa ni Hadiyth Hasan] 

 

 

Kwa hiyo haifai kabisa kujitia manukato na ni dhambi kujipamba aina yoyote ya mapambo mbele ya shemeji zako au mbele ya mtu yeyote mwingine ambaye si mzazi wako, ndugu yako au mumeo hata kama ni jamaa zako, mfano; mtoto wa mjomba, shangazi, mtoto wa ammi yako (ndugu wa baba), mama mkubwa au mama mdogo, na wengineo wote ambao hawakutajwa katika aya hiyo ya Namba 31 katika Suwratun-Nuwr kwani hao wote si mahram wako.

 

 

Kwa hiyo wote hao hupasi kuonyesha uzuri wako kwao na uwe katika hijaab inayotakikana kisheria ya Kiislamu nayo ni kama ifuatavyo:

 

1. Nguo iwe ndefu ya kukufunika mwili mzima mpaka miguu, na kama ni fupi kidogo basi uvae soksi. Ukivaa nguo ambayo itaonyesha sehemu yoyote ya mwili isipokuwa uso na viganja, basi utakuwa hukuvaa hijaab sawa sawa.

 

2. Nguo hiyo iwe pana na si yenye kuonyesha umbo lako, yaani isiwe yenye kukubana popote mwilini khaswa kuanzia kifuani hadi magotini.

 

3. Nguo iwe nzito na sio iliyo nyepesi yenye kuonyesha mwili wako, yaanikitambaa cha nguo kisiwe chepesi.

 

4. Kutokuvaa nguo zinazofanana na nguo za kiume.

 

5. Kutokuvaa nguo zenye urembo na kuvutia  

 

6. Kutotia manukato.

 

 

Utakapotimiza haya utakuwa umekamilisha hijaab yako na Insha Allah utakuwa katika Ridhaa ya Rabb wako. 

 

 

Jambo jengine la kuzingatia hapa ni kwamba mwanamke hatakiwi kumfungulia mlango mwanamume yeyote asiyekua Mahram wake ikiwa mumewe hayupo nyumbani, bali amjibu tu kuwa mumewe hayupo na mwanaume naye inampasa aheshimu mafundisho haya ya Kiislamu na sio kulalamika kama wengi wanavyolalamika kuwa hakumfungulia mlango wakati ni jambo ambalo tumeamrishwa kutoka kwa Rabb wetu.

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا تَدْخُلُوا بُيُوتًا غَيْرَ بُيُوتِكُمْ حَتَّىٰ تَسْتَأْنِسُوا وَتُسَلِّمُوا عَلَىٰ أَهْلِهَا ۚ ذَٰلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ لَعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ ﴿٢٧﴾

Enyi walioamini! Msiingie nyumba zisizokuwa nyumba zenu mpaka muombe ruhusa na muwatolee salamu wenyewe. Hivyo ni bora kwenu ili mpate kukumbuka.

فَإِن لَّمْ تَجِدُوا فِيهَا أَحَدًا فَلَا تَدْخُلُوهَا حَتَّىٰ يُؤْذَنَ لَكُمْ ۖ وَإِن قِيلَ لَكُمُ ارْجِعُوا فَارْجِعُوا ۖ هُوَ أَزْكَىٰ لَكُمْ ۚ وَاللَّـهُ بِمَا تَعْمَلُونَ عَلِيمٌ ﴿٢٨﴾

Na msipokuta humo yeyote; basi msiingie mpaka mruhusiwe. Na mkiambiwa: Rejeeni! Basi rejeeni. Huo ni utakaso zaidi kwenu. Na Allaah Mjuzi wa myatendayo. [An-Nuwr: 27-28]

 

 

Tukumbuke ndugu Waislamu kuwa mafundisho hayo yote ni muhimu sana kuyatekeleza ili kuleta usalama wa kujiepusha na uharibifu wa ndoa baina zetu, na tuyapokee mafundisho hayo bila ya kuona kuwa ni mazito na kumalaumu mwenzako anapotekeleza. Mfano anapokataa mwanamke kupokea mkono wa mwanaume katika kusalimiana. Wengi huona kuwa ni kiburi cha mwanamke wakati pia ni jambo  lililokatazwa katika dini yetu. Na yote hayo ynayofanywa kimakosa na wengi wetu, ni kutokana na mafundisho yasiyo Sahihi au mazoea tuliyokulia nayo kutoka kwa wazazi wetu ambao wengi wao hawakupata mafundisho Sahihi ya dini yetu.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi. 

 

 

Share