Manukato Ni Halaal?

 

SWALI:

Mimi ni mwanafunzi nipo Amerika, swali langu ninauliza kuhusu kupaka lotion au manukato je ni halal?

 


 

JIBU:

Sifa zote njema anastahiki Allah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allahu 'Alayhi wa aalihi wasallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum)  na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Kuhusu manukato hakika ni kuwa Mtume wa Allah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amehimiza Waislamu wanaume na wanawake kujipaka mafuta na manukato isipokuwa kwa wanawake wanapotoka hawafai kupaka yale yenye harufu. Lakini wakiwa nyumbani  wanaweza kupaka na hasa wakiwa wameolewa wanatakiwa wawapambie waume zao.

Ama kuhusu losheni, inaingia katika vipodozi ambavyo vinaruhusiwa kwa Muislamu ikiwa kemikali ambazo zimetumiwa kuitengeneza haitakuwa na madhara kwa mwili wa binadamu. Ikiwa madhara yake yatakuwa ni mengi zaidi kuliko manufaa, kanuni ni kuwa itakuwa imekatazwa.

Lakini kwa wale wanaoishi nchi za Kimagharibi, wanapaswa wawe na tahadhari ya kukagua viambato vinavyotumiwa humo kwani baadhi yake vina asili ya mafuta ya nguruwe. Unaweza kupiga simu  kwa shirika linalotengeneza hivyo vipodozi. Namba kawaida hupatikana nyuma ya chupa au paketi za hivyo vipodozi. Na kutokana na utafiti  na uzoefu wa kutoka kwa baadhi ya ndugu zetu wanaoishi nchi hizo, inasemekana kwamba unapopiga simu kutaka kukagua viambato vyovyote unaweza kuwatajia wazi shaka yako ya kutaka kujua kama vipodozi hivyo vina nguruwe. Nao hutoa jibu sahihi  bila ya kukhini kwa khofu ya kushitakiwa.

Vifuatavyo ni baadhi ya viambato ambavyo aghlabu huwa asili yake ni mafuta na huenda ikawa ni kutokana na nguruwe:

Glycerin

Lanolin

Beef/Pork Tallow

Lard

Magnesium stearate: (hii aghalabu hutokana na damu ya nguruwe na hutumika hasa katika dawa za kunywa kama za iron)

Pepsin

Diglyceride  

Dough Conditioners

Na Allah Anajua zaidi.

 

 

Share