011-Riyaadhw Asw-Swaalihiyn: Mlango Wa Kukatazwa Kumlaani Mtu au Mnyama

 

Riyaadhw Asw-Swaalihiyn

باب تحريم لعن إنسان بعينه أَوْ دابة

011-Mlango Wa Kukatazwa Kumlaani Mtu au Mnyama

 

Alhidaaya.com

 

Hadiyth – 1

عن أَبي زيدٍ ثابت بن الضَّحَّاك الأنصاريِّ رضي اللهُ عنه ، وَهُوَ من أهلِ بَيْعَةِ الرِّضْوَانِ ، قَالَ : قَالَ رسُولُ الله صلى الله عليه وسلم : (( مَنْ حَلَفَ عَلَى يَمِينٍ بِمِلَّةٍ غَيْرِ الإسْلاَمِ كاذِباً مُتَعَمِّداً ، فَهُوَ كَما قَالَ ، وَمَنْ قَتَلَ نَفْسَهُ بِشَيءٍ ، عُذِّبَ بِهِ يَومَ القِيَامَةِ ، وَلَيْسَ عَلَى رَجُلٍ نَذْرٌ فيما لا يَمْلِكُهُ ، وَلَعْنُ المُؤْمِنِ كَقَتْلِهِ )) . متفق عَلَيْهِ .

Imepokewa kutoka kwa Abu Zayd Thaabit bin Adh-Dhahaak Al-Answaariyy (Radhwiya Allaahu 'anhu), naye ni miongoni mwa watu walioshuhudia Bay'ah ya Rhidhwaan ambaye amesema: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Mwenye kuapa kwa makusudi yamini ya uwongo kwa dini isiyokuwa ya Uislamu, huwa ni kama alivyosema. Na mwenye kujiua kwa kitu chochote, ataadhibiwa nacho Siku ya Qiyaamah. Na hapana nadhiri kwa mtu kutoa kitu asicho miliki na kumlaani Muisalmu ni sawa na kumuua." [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Hadiyth – 2

وعن أَبي هريرة رضي اللهُ عنه : أنَّ رسُولَ الله صلى الله عليه وسلم قَالَ : (( لاَ يَنْبَغِي لِصِدِّيقٍ أنْ يَكُونَ لَعَّاناً )) . رواه مسلم .

Imepokewa kutoka kwa Abu Huraiyrah (Radhwiya Allaahu 'anhu) kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Haifai (haitakiwi) kwa mtu ambaye ni mkweli kuwa na sifa ya kulaani." [Muslim]

 

Hadiyth – 3

وعن أَبي الدرداءِ رضي اللهُ عنه قَالَ : قَالَ رسُولُ الله صلى الله عليه وسلم : (( لاَ يَكُونُ اللَّعَانُونَ شُفَعَاءَ ، وَلاَ شُهَدَاءَ يَوْمَ القِيَامَة )) . رواه مسلم .

Imepokewa kutoka kwa Abu Dardaa (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Wala wenye kulaani sana hawawezi kuwa ni mwenye kuwaombea wenziwao wala kuwa mashahidi Siku ya Qiyaamah." [Muslim]

 

Hadiyth – 4

وعن سَمُرَةَ بْنِ جُنْدُبٍ رضي اللهُ عنه ، قَالَ : قَالَ رسُولُ اللهِ صلى الله عليه وسلم : (( لاَ تَلاَعَنُوا بِلَعْنَةِ اللهِ ، وَلاَ بِغَضَبِهِ ، وَلاَ بِالنَّارِ )) رواه أَبُو داود والترمذي ، وقال : (( حديث حسن صحيح )) .

Imepokewa kutoka kwa Samurah bin Jundub (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Usimlaani yeyote kati yenu kwa laana ya Allaah wala kwa Ghadhabu Zake wala pia kwa moto." [Abu Daawuwd na At-Tirmidhiy, na akasema ni Hadiyth Hasan Swahiyh]

 

Hadiyth – 5

وعن ابن مسعود رضي اللهُ عنه ، قَالَ : قَالَ رسُولُ الله صلى الله عليه وسلم : (( لَيْسَ المُؤْمِنُ بالطَّعَّانِ ، وَلاَ اللَّعَّانِ ، وَلاَ الفَاحِشِ ، وَلاَ البَذِيِّ )) رواه الترمذي ، وقال : (( حديث حسن )) .

Imepokewa kutoka kwa Ibn Mas'uwd (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Hawi kabisa Muumini na sifa ya kusuta, wala kulaani, wala kutusi wala kutumia lugha chafu." [At-Tirmidhiy, na akasema ni Hadiyth hasan]

 

Hadiyth – 6

وعن أَبي الدرداء رضي اللهُ عنه قَالَ : قَالَ رسُولُ الله صلى الله عليه وسلم : (( إنَّ العَبْدَ إِذَا لَعَنَ شَيْئاً ، صَعدَتِ اللَّعْنَةُ إِلَى السَّماءِ ، فَتُغْلَقُ أبْوابُ السَّماءِ دُونَهَا ، ثُمَّ تَهْبِطُ إِلَى الأرْضِ ، فَتُغْلَقُ أبْوابُهَا دُونَها ، ثُمَّ تَأخُذُ يَميناً وَشِمالاً ، فَإذا لَمْ تَجِدْ مَسَاغاً رَجَعَتْ إِلَى الَّذِي لُعِنَ ، فإنْ كَانَ أهْلاً لِذلِكَ ، وإلاَّ رَجَعَتْ إِلَى قَائِلِهَا )) . رواه أَبُو داود .

Imepokewa kutoka kwa Abu Dardaa (Radhwiya Allaahu 'anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Hakika mja anapokilaani kitu chochote, laana hiyo hupanda mpaka mbinguni, na hapo milango yote ya mbinguni hufungwa mbele yake. Kwa ajili hiyo hushuka tena ardhini, na pia hufungwa milango mbele (dhidi) yake. Kisha hugeuka upande wa kuume na kushotoni na ikiwa haitapata nafasi ya kuingilia, itarudi kwa yule aliye laaniwa ikiwa atafaa kupata laana hiyo. Na ikiwa ni kinyume na hivyo basi itarudi kwa yule aliye laani." [Abu Daawuwd]

 

Hadiyth – 7

وعن عمران بن الحُصَيْنِ رضي الله عنهما ، قَالَ : بَيْنَمَا رسُولُ اللهِ صلى الله عليه وسلم في بَعْضِ أسْفَارِهِ ، وَامْرأةٌ مِنَ الأنْصَارِ عَلَى نَاقَةٍ ، فَضَجِرَتْ فَلَعَنَتْهَا ، فَسَمِعَ ذَلِكَ رسُولُ الله صلى الله عليه وسلم فقالَ : (( خُذُوا مَا عَلَيْهَا وَدَعُوهَا ؛ فَإنَّهَا مَلْعُونَةٌ )) قَالَ عمْرانُ : فَكَأنِّي أَرَاهَا الآنَ تَمْشِي في النَّاسِ مَا يَعْرِضُ لَهَا أحَدٌ . رواه مسلم .

Amesema 'Imraan bin Al-Huswayn (Radhwiya Allaahu 'anhumaa): Tulipokuwa na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika baadhi ya safari zake na wakati mmoja mwanamke mmoja wa Ki-Answaar alikuwa pamoja nasi. Alikuwa amempanda ngamia wa kike, na kwa ile shida na matatizo yaliyo kuwepo alimlaani. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alimsikia, akasema: "Chukua vitu vilivyo juu yake na umwache kwani amelaaniwa." Akasema 'Imraan: "Hakika ni kama kwamba namwangalia ngamia huyo akipita miongoni mwa watu na hakuna anayeshughulika naye kabisa." [Muslim]

 

Hadiyth – 8

وعن أَبي بَرْزَةَ نَضْلَةَ بْنِ عُبَيْدٍ الأَسْلَمِيِّ رضي اللهُ عنه قَالَ : بَيْنَمَا جَارِيَةٌ عَلَى نَاقَةٍ عَلَيْهَا بَعْضُ مَتَاعِ القَوْمِ . إِذْ بَصُرَتْ بِالنَّبيِّ صلى الله عليه وسلم ، وَتَضَايَقَ بِهِمُ الجَبَلُ فَقَالَتْ : حَلْ ، اللَّهُمَّ الْعَنْهَا. فَقَالَ النَّبِيُّ صلى الله عليه وسلم : (( لاَ تُصَاحِبْنَا نَاقَةٌ عَلَيْهَا لَعْنَةٌ )) . رواه مسلم .

Amesema Abu Barzah Nadhlah bin 'Ubayd Al-Aslamiyy (Radhwiya Allaahu 'anhu): Kijakazi mmoja alikuwa amempanda ngamia aliyekuwa amebeba samani za watu wake (kabila lake). Mara kwa ghafla akamuona Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na zile njia za majabalini zilikuwa ndogo sana, hivyo kumfanya aseme kwa hasira: "Ee Allaah! Mlaani (huyu ngamia)." Akasema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): "Asifuatane nasi ngamia ambaye ana laana juu yake." [Muslim]

 

Share