Zingatio 2: Kuukaribisha Mwezi Mtukufu Wa Ramadhwaan Na Kukhofia Kikata Ladha

 

Zingatio 2: Kuukaribisha Mwezi Mtukufu Wa

 

Ramadhwaan Na Kukhofia Kikata Ladha

 

Naaswir Haamid

 

 

 Alhidaaya.com

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  Ameiumba dunia ikiwa ni mchezo na hakuna ndani yake ila pumbao. Kuna kila aina ya starehe duniani, bila ya kusahau kwamba Jannah ndio kiboko cha starehe. Kwani huko kuna maisha ya milele, starehe zisizokuwa na mpaka, hakuna maneno ya bughudha na mengineyo. Basi kusanya vingi utakavyoweza, nenda mbali utakavyoweza, fanya ovu unaloliweza ila usisahau ile siku utakayotenganishwa na hii dunia.

 

 

Mkumbuke Malakul-Mawt ambaye atayakatisha maisha ghafla moja, bila ya mtu kutaraji, bila ya wakati maalum na bila ya kuletewa barua. Huyo si mwengine, ila mwenye kumpatia jina jipya mtu kuwa ni Aliyefariki, anayeligeuza jina la mke kuwa Kizuka na kumfanya kuwa Mjane. Anayempatia jina jipya mtoto kuwa ni Yatima. Anayegeuza mali iliyoachwa kuwa ni mirathi. Hiyo ni amri ya Rabb wetu kuzichukua roho za wana Aadam, mmoja baada ya mmoja. Na ujira wa matendo yote yatalipwa kamili Siku ya Qiyaama. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):  

 

كُلُّ نَفْسٍ ذَائِقَةُ الْمَوْتِ ۗ وَإِنَّمَا تُوَفَّوْنَ أُجُورَكُمْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ ۖ فَمَن زُحْزِحَ عَنِ النَّارِ وَأُدْخِلَ الْجَنَّةَ فَقَدْ فَازَ ۗ وَمَا الْحَيَاةُ الدُّنْيَا إِلَّا مَتَاعُ الْغُرُورِ ﴿١٨٥﴾

Kila nafsi itaonja mauti. Na hakika mtalipwa kikamilifu ujira wenu Siku ya Qiyaamah. Basi atakayewekwa mbali na moto na akaingizwa Jannah kwa yakini amefuzu. Na uhai wa dunia si lolote ila ni starehe ya udanganyifu. [Aal-‘Imraan: 185]

 

Wakati ni huu wa kujitayarisha kutenda mema, kuachana na maovu. Wakati umefika wa kujikurubisha kwa Rabb bila ya kurudi nyuma. Sio wakati tena wa kuandaa ratiba za Vunja Jungu wala kupanga mikakati ya kuimaliza Ramadhwaan kwa haraka ukitegemea kufanya maovu siku ya ‘Iyd.  Usiwe sawa na Fir-‘awn ambaye hadi roho yake inatolewa ndio anashuhudia kuwa Risaala ya Muwsaa ‘('alayhis-salaam)  kuwa ni haki. Wala usisubirie hadi roho inatolewa ndio uombe tawbah. Hapo toba katu haikubaliwi kwani sio sehemu yake kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa): 

 

وَلَيْسَتِ التَّوْبَةُ لِلَّذِينَ يَعْمَلُونَ السَّيِّئَاتِ حَتَّىٰ إِذَا حَضَرَ أَحَدَهُمُ الْمَوْتُ قَالَ إِنِّي تُبْتُ الْآنَ وَلَا الَّذِينَ يَمُوتُونَ وَهُمْ كُفَّارٌ ۚ أُولَـٰئِكَ أَعْتَدْنَا لَهُمْ عَذَابًا أَلِيمًا ﴿١٨﴾ 

Lakini tawbah si kwa wale wanaofanya maovu mpaka mauti yanapohudhuria kwa mmoja wao husema: “Hakika mimi sasa nimetubu.” Na wala wale wanaokufa na hali wao ni makafiri. Hao Tumewaandalia adhabu iumizayo. [An-Nisaa: 18]

 

Kifo ndugu yangu hakikimbiliki katu. Eeh hasara yetu kwa kughafilika na dunia hii! Kama umekuja duniani basi ipo siku utaondoka. Hizo zote ni haki zake mwana Aadam, Allaah lazima Amtimizie, Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَجَاءَتْ سَكْرَةُ الْمَوْتِ بِالْحَقِّ ۖ ذَٰلِكَ مَا كُنتَ مِنْهُ تَحِيدُ﴿١٩﴾

Na sakarati ya mauti itakapomjia kwa haki. (Itasemwa): Hayo ndiyo yale uliyokuwa ukiyakimbilia mbali. [Qaaf: 19]

 

 

Hivyo tujihimize katika miezi hii mitukufu na kumkaribisha mgeni mwema Ramadhwaan pamoja na miezi iliyobaki kwa kuchuma yale ambayo yatatuingiza Jannah na kuyaepuka yale ambayo yatatuingiza Motoni. Kwani Moto ni matokeo ya matendo maovu, wakati Jannah ni natija ya amali njema.

 

 

Share