Niyyah Ya Swawm Ni Kwa Kila Siku Au Mara Moja Inatosha

 

 

Niyyah Ya Swawm Ni Kwa Kila Siku Au Mara Moja Inatosha?

 

 

SWALI:

 

kuna nukta chache ningependa ufafanuzi zaidi. 

 

Kuhusu nia, nimetatizika kidogo maana masheikh wetu huku wanatuambia inabidi kunuia kila siku. Na kama mfano bahati mbaya mtu akalala bila kunuia siku hiyo basi hana Swaum. Kama kasahau kunuia usiku huo haruhusiwa kula na inabidi aje kuilipa siku hiyo.

Naomba ufafanuzi, usahihi ni vipi kuhusu nia, ukitia nia siku ya kwanza yatosha kufunga mwezi mzima ama lazima kila siku unuie kama kesho wafunga?

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Hili ni suala sahali lakini kwa sababu ya kutaka kuongeza mambo katika Dini yetu tunawapatia ugumu Waislamu wa kawaida bila ya kuwa na haja aina yoyote.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anatutakia usahali hata kwa mwezi wa Ramadhwaan pale Aliposema:

 

 

شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِي أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَىٰ وَالْفُرْقَانِ ۚ فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ ۖ وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ ۗ يُرِيدُ اللَّـهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلَا يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ وَلِتُكْمِلُوا الْعِدَّةَ وَلِتُكَبِّرُوا اللَّـهَ عَلَىٰ مَا هَدَاكُمْ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ ﴿١٨٥﴾

Mwezi wa Ramadhwaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan ili iwe mwongozo kwa watu na hoja bayana za mwongozo na pambanuo (la haki na batili). Basi atakayeshuhudia miongoni mwenu mwezi na afunge. Na atakayekuwa mgonjwa au safarini, basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. Allaah Anakutakieni mepesi na wala Hakutakieni magumu; na ili mkamilishe idadi na ili mumkabbir Allaah kwa kuwa Amekuongozeni na ili mpate kushukuru. [Al-Baqarah: 185]

 

   

Na katika hali zote Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)    Anasema:

 

  وَمَا جَعَلَ عَلَيْكُمْ فِي الدِّينِ مِنْ حَرَجٍ ۚ  

Na Hakukufanyieni ugumu wowote ule katika Dini.  [Al-Hajj: 78]

 

 

Shariy'ah za Kiislamu zimekuja kuhafifisha na kuondoa uzito mwingi uliokuwepo.

 

Ya kustaajabisha ni kuwa utakuta katika mambo mengi tunarudisha ugumu usiokuwepo. Mfano ni mas-ala niyyah katika Swiyaam za faradhi, kulipa Swawm ya faradhi au kafara. Katika Swawm zote hizo ni lazima Muislamu atie niyyah na bila niyyah mfungaji hatokuwa na Swawm.

 

Lakini je, niyyah inatiwa namna gani? Utakuta katika sehemu nyingi ulimwengu watu wanatilishwa niyyah na ima Imaam au Muadhini au Shaykh ilhali jambo kama hilo ni uzushi kutoka kwa watu. Kufanya hivyo kumewapatia uzito Waislamu wengi na hivyo kuzua maswali kama haya yanayoulizwa.

 

Kuhusu swali lako la kutia Niyyah kama ni kila siku au inatosha kuiweka siku ya kwanza ya kuanza Ramadhwaan, hili hakika wametofautiana ‘Ulamaa kuna waliokwenda na kuona inatosha mwanzo wa mwezi wa Ramadhwaan kuiweka niyyah na ukatosheleza mwezi mzima. Lakini ‘Ulamaa wengi wameonelea Niyyah ni kuwekwa kila usiku wa kabla yake na hi ndio kauli yenye nguvu. Na Niyyah inaweza kuwekwa katika sehemu yoyote ya usiku hata ikiwa ni sekunde chache kabla ya Alfajiri ya kweli (yaani wakati wa adhana ya pili). Maana ya niyyah hasa ni kuazimia kwa moyo kutekeleza 'amali fulani, na kuitamka kwa ulimi ni uzushi katika Dini.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share