Anaweza Kufuta Picha Za Ngono Katika Kompyuta Ya Mwenziwe Bila ya Ruhusa?

   

Anaweza Kufuta Picha Za Ngono Katika Kompyuta Ya Mwenziwe Bila ya Ruhusa?

 

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali:

Hongereni kwa program hii nimeikubali Allaah awazidishie mtoe bora zaidi ya hivi KEEP IN TOUCH MY FELLOW MUSLIMS je kuna tatizo lolote kufuta ie delete mambo ya kipuuzi like phonographs kwenye computer ya mtu bila ya kumtaarifu muhusika ie mwenye computer au bila yeye mwenyewe kukuruhusu sorry for this question if not good for you.

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Hakika ni kuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na Nabiy Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) wametuhimiza sana mas-ala ya kuamrisha mema na kukataza mabaya. Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

ادْعُ إِلَىٰ سَبِيلِ رَبِّكَ بِالْحِكْمَةِ وَالْمَوْعِظَةِ الْحَسَنَةِ ۖ وَجَادِلْهُم بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ ۚ

Lingania katika njia ya Rabb wako kwa hikmah na mawaidha mazuri. Na jadiliana nao kwa ambayo ni mazuri zaidi. [An-Nahl: 125].

 

Na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

"Yeyote katika nyinyi atakayeona munkari naubadilishe kwa mkono wake; na akiwa hawezi basi afanye hivyo kwa ulimi wake; na akiwa hawezi basi afanye kwa moyo wake na huo ni udhaifu wa Imani" (Muslim).

 

Nguvu zinatumika kwa yule aliye chini yako kama mtoto wako au watoto unaowalea na wengineo kama mtu ambaye yupo chini ya usimamizi wako au unamlea n.k., lakini ikiwa ni rafiki yako ni lazima ubadilishe munkari kwa busara na kumkinaisha. Kuifuta pekee haitoshi kwani akiona haipo atairudisha nawe pia utakuwa umeingia makosani kidini. Na pia huenda ikamfanya mwenzio azidi kurudia hayo maovu  badala ya kukubali nasaha kwa kuchukia kuingiliwa katika mambo yake ya kibinafsi  Pia ufahamu kuwa hairuhusiwi kuingia katika nyumba au vitu vya watu bila idhini yao. Jambo la busara ni wewe uzungumze naye huku ukimueleza na kumfahamisha makosa hayo katika Dini. Akikinaika na hilo nawe utapata ujira na kama hakukubali kuhusu hilo wewe jukumu lako litakuwa limekwisha isipokuwa utahitajika kumnasihi tena na tena na tawfiki inatoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa). Hata kama hatakubali unayomwambia wewe utakuwa na ujira wako kwa ukamilifu.

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

وَذَكِّرْ فَإِنَّ الذِّكْرَىٰ تَنفَعُ الْمُؤْمِنِينَ ﴿٥٥﴾

Na kumbusha, kwani ukumbusho huwafaa Waumini. [Adh-Dhaariyaat: 56].  Na anasema Allaah Subhaanahu wa Ta'aalaa:

 

وَمَا أُرْسِلُوا عَلَيْهِمْ حَافِظِينَ ﴿٣٣﴾

Na wao hawakutumwa kuwa ni walinzi juu yao. [Al-Mutwaffifyn: 33].

 

Na Anasema tena:

فَذَكِّرْ إِنَّمَا أَنتَ مُذَكِّرٌ ﴿٢١﴾لَّسْتَ عَلَيْهِم بِمُصَيْطِرٍ ﴿٢٢﴾

Basi kumbusha! Hakika wewe ni Mkumbushaji. Wewe si mwenye kuwadhibiti. [Al-Ghaashiyah: 21 – 22].

 

Tukumbuke pia kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa salaam) amesema:

 

"Miongoni mwa uzuri wa Uislamu wa mtu ni kuacha lisilomkhusu" [at-Tirmidhiy, nayo ni Hadiyth Hasan].

 

Nia yako na malengo ni mazuri sana, lakini ni vyema ufuate utaratibu wa sawa ili kupatikane natija nzuri inshaAllaah. Hata hivyo, ikiwa unahisi ukifuta hatoweka tena au kupata tena na kuweka, na hakutoleta matatizo, basi ni bora kufanya hivyo 

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share