Vipi Amuongoze Nduguye Aliye Na 'Aqiydah Potofu na Mambo ya Bid'ah?

 

 

Vipi Amuongoze Nduguye Aliye Na 'Aqiydah Potofu na Mambo ya Bid'ah?

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

 

Allaah awalipe heri kwa kazi hii.

 

Swali:

 

Mimi ni mtanzania lakini kwa sasa niko India kimasomo, chuo ninachosoma,wako waislamu wachache mno wahindi na kwa ukweli hawajui chochote katika dini. Pia nipo na mwafrika mwenzangu mmoja toka west Africa, pia ni mwislamu, lakini ni mchache mno katika dini kielimu,sina elimu kubwa ya dini lakini nilijitahidi kusoma kidogo dini na kuhudhuria madarsa mbalimbali, Tanzania,tatizo linakuja ndugu yangu kakulia kwenye nchi yenye waislam wengi lakini anazikumbatia bidaa na Akida yake kwa kweli ina mashaka sana, mf, anaamini wapo Rusuli waliopita waliokuwa wakristo, uislamu ni dini mpya na imekuja mwishoni na mengine mengi, na kila ninapojitahidi kumweka sawa, ni mbishi na hataki kubadilika, mara nyingi tumekua tukigombana kwa kutaka tu kumweka sawa.Nifanyeje?

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

 

Mwanzo tunataka kukufahamisha kuwa hizo bid‘ah huku Afrika Mashariki zilitoka katika nchi za Waislamu. Kwa mfano Mawlid yalianza mwanzo katika nchi ya Misri karne tano baada ya kuaga dunia kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Na hata Lamu, kisiwa ambacho kinajulikana kuwa ni kitovu cha Mawlid ya ngoma katika Afrika Mashariki yaliletwa kama miaka 120 tu iliyopita. Mashaykh wakubwa, na hasa Shaykh Fayswal al-Laamiy aliyapinga kabisa na hata kuna baadhi ya Misikiti mpaka sasa katika kisiwa hicho hakusomwi Mawlid. Mawlid yaliletwa na Shariyf katika ukoo wa Jamalil Layl, kwa jina Habib Swaalih kutoka Ngazija (Comoro). Kwa sasa bid‘ah zinaendelea kufanywa maradufu katika nchi za Waislamu kama Misri, Sudan, Pakistan, Bangladesh, India, Yemen na nchi nyinginezo. Hakika hilo si la kustaajabisha kabisa.

 

 

Pia utapata serikali za nchi nyingi za Waislamu zikiupinga Uislamu na Waislamu wenye msimamo mzuri dhahiri shahiri. Mfano wa nchi kama hizi ni Misr, Algeria, Morocco, Libya, Tunisia na nyinginezo. Nyingine zimekuwa za kisekula kabisa hadi kuwa wanapiga marufuku uvaaji wa hijabu kwa wanawake barabarani, katika taasisi na vyuo vya serikali kama Tunisia, Uturuki na kadhalika.

 

 

Hata hivyo katika kufanya Da ‘wah na kumlingania huyo nduguyo wa Afrika Magharibi usife moyo bali endelea kwa busara na mawaidha mazuri kama alivyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa):

ادْعُ إِلَىٰ سَبِيلِ رَبِّكَ بِالْحِكْمَةِ وَالْمَوْعِظَةِ الْحَسَنَةِ ۖوَجَادِلْهُم بِالَّتِي هِيَ أَحْسَنُ ۚ 

Lingania katika njia ya Rabb wako kwa hikmah na mawaidha mazuri. Na jadiliana nao kwa ambayo ni mazuri zaidi. [An-Nahl: 125].

 

 

Ukiona ameanza kubishana ni bora zaidi kuacha kuzozana na ungoje wakati mwengine muafaka. Sababu ni kuwa unapozozana watu hawatajua tofauti baina yenu na kufanya hivyo ni sifa ya kuwa na Imani. Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa) Anasema:

 

وَعِبَادُ الرَّحْمَـٰنِ الَّذِينَ يَمْشُونَ عَلَى الْأَرْضِ هَوْنًا وَإِذَا خَاطَبَهُمُ الْجَاهِلُونَ قَالُوا سَلَامًا ﴿٦٣﴾

Na waja wa Ar-Rahmaan ni wale wanaotembea katika ardhi kwa unyenyekevu na upole, na majahili wanapowasemesha, wao husema: Salaam! [Al-Furqaan: 63].

 

 

Tuna imani kuwa kwa juhudi zako na tawfiki ya Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa) atabadilika siku moja, In shaa Allaah.

 

 

Unachotakiwa kufanya ni wewe kumuelewesha nduguyo kuhusu maana ya Dini ambayo sio sawa na neno la Kiingereza Religion. Dini ina maana pana kuliko Religion na inajumlisha maisha yote ya mwanadamu. Yaonyesha kuwa nduguyo katekwa na kasumba ya wasio Waislamu kuwa Uislamu ni Dini aliyokuja nayo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na ni ya Waarabu peke yake. Katika hili inatakiwa umueleweshe kuwa Uislamu umeanza kuanzia kuumbwa kwa mwanaadamu wa mwanzo, Nabiy Aadam (‘alayhissSalaam). Hii ni kuwa mwanzo Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa) Ametuma Rusuli (‘alayhimus-salaam) kwa kila Ummah:

وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِي كُلِّ أُمَّةٍ رَّسُولًا أَنِ اعْبُدُوا اللَّـهَ وَاجْتَنِبُوا الطَّاغُوتَ ۖ 

Na kwa yakini Tulituma katika kila ummah Rasuli (alinganie) kwamba: Mwabuduni Allaah na jiepusheni na twaghuti.[An-Naml: 36].

 

 

Kisha mfahamishe kuwa Dini inayokubaliwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta‘aalaa) ni Uislamu tu:

إِنَّ الدِّينَ عِندَ اللَّـهِ الْإِسْلَامُ ۗ وَمَا اخْتَلَفَ الَّذِينَ أُوتُوا الْكِتَابَ إِلَّا مِن بَعْدِ مَا جَاءَهُمُ الْعِلْمُ بَغْيًا بَيْنَهُمْ ۗ

Hakika Dini mbele ya Allaah ni Uislamu. Na hawakukhitilafiana wale waliopewa Kitabu ila baada ya kuwajia elimu kwa kufanyiana baghi na uhusuda baina yao. [Al-'Imraan: 19].

 

 

Ni wazi kuwa hilo linajulikana na waliopewa Vitabu pia lakini wakavipotosha na kupotosha hayo. Tujue kuwa yeyote anayetafuta na kufuata Dini isiyokuwa ya Uislamu haitakubaliwa kwake:

وَمَن يَبْتَغِ غَيْرَ الْإِسْلَامِ دِينًا فَلَن يُقْبَلَ مِنْهُ وَهُوَ فِي الْآخِرَةِ مِنَ الْخَاسِرِينَ ﴿٨٥﴾

Na yeyote anayetaka dini isiyokuwa ya Kiislamu basi haitokubaliwa kwake; naye katika Aakhirah atakuwa miongoni mwa waliokhasirika. [Al-'Imraan: 85]. 

 

 

Mfahamishe kuwa Manabii na Rusuli wote (‘alayhimus-salaam) walikuwa Waislamu. Dalili ya kauli hiyo ni Aayah zifuatazo:

 

قُلْ آمَنَّا بِاللَّـهِ وَمَا أُنزِلَ عَلَيْنَا وَمَا أُنزِلَ عَلَىٰ إِبْرَاهِيمَ وَإِسْمَاعِيلَ وَإِسْحَاقَ وَيَعْقُوبَ وَالْأَسْبَاطِ وَمَا أُوتِيَ مُوسَىٰ وَعِيسَىٰ وَالنَّبِيُّونَ مِن رَّبِّهِمْ لَا نُفَرِّقُ بَيْنَ أَحَدٍ مِّنْهُمْ وَنَحْنُ لَهُ مُسْلِمُونَ ﴿٨٤﴾

Sema: Tumemwamini Allaah, na yaliyoteremshwa kwetu na yaliyoteremshwa kwa Ibraahiym, na Ismaa’iyl na Is-haaq, na Ya’quwb na Al-Asbaatw na yale aliyopewa Muwsaa na ‘Iysaa na Manabii kutoka kwa Rabb wao, hatutofautishi baina ya mmoja yeyote miongoni mwao, nasi ni Waislamu (tunajisalimisha) Kwake. [Al-'Imraan: 84]

 

 

Pia Allaah Subhaanahu wa Ta'aala anasema:

 

 أَمْ كُنتُمْ شُهَدَاءَ إِذْ حَضَرَ يَعْقُوبَ الْمَوْتُ إِذْ قَالَ لِبَنِيهِ مَا تَعْبُدُونَ مِن بَعْدِي قَالُوا نَعْبُدُ إِلَـٰهَكَ وَإِلَـٰهَ آبَائِكَ إِبْرَاهِيمَ وَإِسْمَاعِيلَ وَإِسْحَاقَ إِلَـٰهًا وَاحِدًا وَنَحْنُ لَهُ مُسْلِمُونَ ﴿١٣٣﴾

Je, mlikuwa mashahidi wakati mauti yalipomfikia Ya’quwb alipowaambia wanawe: Mtaabudu nini baada yangu? Wakasema: Tutamwabudu Ilaaha wako (Allaah) na Ilaaha wa baba zako, Ibraahiym na Ismaa’iyl na Is-haaq; Ilaah Mmoja, nasi ni Waislamu (tunajisalimisha) Kwake. [Al-Baqarah: 133].

 

 

Ama kuhusu Nabiy ‘Iysaa (‘alayhis-salaam) Qur-aan inatueleza kuwa alikuwa yeye pamoja na wafuasi wake ni Waislamu:

 

 إِنَّ اللَّـهَ رَبِّي وَرَبُّكُمْ فَاعْبُدُوهُ ۗ هَـٰذَا صِرَاطٌ مُّسْتَقِيمٌ ﴿٥١﴾ فَلَمَّا أَحَسَّ عِيسَىٰ مِنْهُمُ الْكُفْرَ قَالَ مَنْ أَنصَارِي إِلَى اللَّـهِ ۖ قَالَ الْحَوَارِيُّونَ نَحْنُ أَنصَارُ اللَّـهِ آمَنَّا بِاللَّـهِ وَاشْهَدْ بِأَنَّا مُسْلِمُونَ ﴿٥٢﴾

Hakika Allaah ni Rabb wangu na Rabb wenu basi mwabuduni. Hii ndio njia iliyonyooka. Basi alipohisi ‘Iysaa ukafiri kutoka kwao; alisema: Nani wanusuruji wangu kwa ajili ya Allaah? Wakasema wafuasi watiifu:  Sisi ni wasaidizi wa Allaah. Tumemwamini Allaah na shuhudia kwamba sisi ni Waislamu (tunajisalimisha Kwake). [Al-'Imraan: 51 – 52].

 

Pia,

 

وَإِذْ أَوْحَيْتُ إِلَى الْحَوَارِيِّينَ أَنْ آمِنُوا بِي وَبِرَسُولِي قَالُوا آمَنَّا وَاشْهَدْ بِأَنَّنَا مُسْلِمُونَ ﴿١١١﴾إِذْ قَالَ الْحَوَارِيُّونَ يَا عِيسَى ابْنَ مَرْيَمَ هَلْ يَسْتَطِيعُ رَبُّكَ أَن يُنَزِّلَ عَلَيْنَا مَائِدَةً مِّنَ السَّمَاءِ ۖ قَالَ اتَّقُوا اللَّـهَ إِن كُنتُم مُّؤْمِنِينَ ﴿١١٢﴾قَالُوا نُرِيدُ أَن نَّأْكُلَ مِنْهَا وَتَطْمَئِنَّ قُلُوبُنَا وَنَعْلَمَ أَن قَدْ صَدَقْتَنَا وَنَكُونَ عَلَيْهَا مِنَ الشَّاهِدِينَ ﴿١١٣﴾

Na Nilipowatia ilhamu wafuasi watiifu kwamba: Niaminini Mimi na Rasuli Wangu. Wakasema: Tumeamini na shuhudia kwamba sisi ni Waislamu. Pindi waliposema wafuasi watiifu: Ee ‘Iysaa mwana wa Maryam! Je, Anaweza Rabb wako Kututeremshia meza iliyotandazwa chakula kutoka mbinguni? Akasema: Mcheni Allaah, kama nyinyi ni Waumini. Wakasema: Tunataka kula katika hicho; na ili nyoyo zetu zitulie; na tujue kwamba kwa yakini umetuambia kweli; na tuwe juu yake miongoni mwa wanaoshuhudia. [Al-Maaidah: 111 – 113].

 

 

Pia mueleze kuwa Ukristo haukuwepo wakati wa Nabiy ‘Iysaa (‘alayhis-salaam) kwani yeye alikuwa Muislamu. Hata Biblia inatuarifu kuwa Ukristo haukuwepo wakati wa Nabiy ‘Iysaa (‘alayhis- salaam) bali ulikuja baadaye. Mpatie changa moto katika hilo akuonyeshe katika kitabu hicho sehemu ambayo Nabiy ‘Iysaa (‘alayhis-salaam) anasema kuwa amekuja na Ukristo na akatutaka sisi tumfuate. Hakika ni kuwa Biblia inatueleza: “Nao wote wawili (yaani Saulo na Barnaba) walikaa na ile jumuiya ya kanisa kwa mwaka wote mzima wakifundisha kundi kubwa la watu. Huko Antioka, ndiko kwa mara ya kwanza, wafuasi waliitwa Wakristo” (Matendo 11: 26).

 

 

Wakati huu Nabiy ‘Iysaa (‘alayhis-salaam) alikuwa hayupo tena duniani na Ukristo huo ulianzishwa nje ya Jerusalem, mji ambao alikuwa akihubiri.

 

 

Kwa sababu ya ubishi wa nduguyo, jaribu njia nyingine kama kumpatia vitabu vizuri kuhusu Uislamu vya Kiingereza kama anajua au VCD au CD au kaseti. InshaAllaah tunaamini kuwa siku moja atabadilika.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share