024-Kutoa Zakaah: Zakaah Ya Wanyama Wa Kufugwa

 

 

Zakaah Ya Wanyama Wa Kufugwa

 

Alhidaaya.com

 

 

Wanyama wanaofugwa wanalazimika kutolewa Zakaah kwa masharti yafuatayo:

1.  Lazima watimie Niswaab

2.  Wakamilishe mwaka

3.  Wawe wanyama wa kufugwa.

 

Wanyama wasiokuwa wa kufugwa kama vile wa kupandwa au wanaotumiwa kwa kubeba mizigo au kwa kilimo n.k. Hawa hawatolewi Zakaah.

Wanyama wanaotolewa Zakaah ni Ngamia, Ng'ombe, Mbuzi na Kondoo.

 

Zakaah Ya Ngamia

 

Ngamia hawatolewi Zakaah mpaka watimie watano. Wakitimia watano wa kufugwa hadi tisa na kutimiza mwaka chini ya milki ya mtu, basi atawatolea mbuzi mmoja.

 

Wakitimia ngamia 10 mpaka 14 atawatolea mbuzi wawili.

 

Na hivyo hivyo kila wakizidi ngamia watano ataongeza mbuzi mmoja.

Wakitimia ngamia 25 mpaka 35 atatoa mtoto wa ngamia jike aliyekamilisha mwaka na kuingia mwaka wa pili au mtoto wa ngamia dume aliyekamilisha mwaka wa 2 na anaingia wa 3.

 

Kuanzia ngamia 36 mpaka 45 atatoa mtoto wa ngamia jike aliyekamilisha miaka 2 na keshaingia wa 3.

 

Kuanzia ngamia 46 mpaka 60 atatoa mtoto wa ngamia jike aliyekamilisha miaka 3 na kuingia wa 4.

 

Kuanzia ngamia 61 mpaka 75 atatoa mtoto wa ngamia jike aliyekamilisha miaka 4 na kuingia mwaka wa 5.

 

Kuanzia ngamia 76 mpaka 90 atatoa watoto wa ngamia wawili jike waliokamilisha miaka miwili na kuingia wa tatu.

 

Kuanzia ngamia 91 mpaka 120 atatoa watoto wa ngamia wa kike wawili waliotimia miaka 3 na kuingia mwaka wa 4.

 

Wakizidi kuliko hapo, basi katika kila ngamia 40 atatoa mtoto wa ngamia wa kike aliyekamilisha miaka 2 na kuingia wa 3. Na katika kila ngamia 50 waliozidi kuliko hapo atatoa mtoto wa ngami wa kike aliyekamilisha miaka 3 na kuingia wa nne.

 

Anasema Sayyid Saabiq katika Fiqhis Sunnah:

"Hawatolewi Zakaah ngamia dume ikiwa wapo wa kike, lakini anatolewa mtoto wa ngamia wa kiume aliyetimia miaka miwili na kuingia wa tatu ikiwa hajapatikana wa kike aliyekamilisha mwaka na kuingia wa pili.

 

 

Zakaah Ya Ng’ombe

 

Ng'ombe hawatolewi Zakaah mpaka watimie 30 wa kufugwa. Wanapotimia 30 mpaka 39 wa kufugwa na kukamilisha mwaka, atatolewa ndama aliyekamilisha mwaka mmoja.

 

Wakitimia ng'ombe 40 mpaka 59 atatolewa ndama asiyepungua umri wa miaka miwili.

 

Wakitimia ng'ombe 60 mpaka 79 atatolewa ndama wawili wa mwaka mmoja.

 

Kutoka hapo, kila wakizidi ng'ombe 30, ataongeza kutoa ndama wa mwaka mmoja.

 

Na kila wakizidi ng'ombe 40 atawatolea ndama wa miaka miwili.

 

 

Zakaah Ya Mbuzi

 

Mbuzi hawatolewi Zakaah mpaka watimie 40, na wakitimia arubaini mpaka 120 wa kufugwa na kukamilisha mwaka kwa mwenye kuwamiliki, atawatolea mtoto wa mbuzi wa mwaka mmoja.

 

Hatowatolea tena mpaka wafikie idadi yao mbuzi 121.

 

Wakiongezeka na kutimia 121 mpaka 200, atawatolea mtoto wa miaka miwili.

 

Kuanzia mbuzi 201 mpaka 300 atawatolea kondoo watatu.

 

Wakizidi kuliko mbuzi 300, basi atawatolea kondoo mmoja katika kila mbuzi mia waliozidi.

 

Inaruhusiwa pia kutoa mbuzi badala ya kondoo.

 

Wanyama Wengine

 

Wanyama wengine wasiokuwa hawa kama vile farasi, nyumbu, punda na wengineo, hawatolewi Zakaah isipokuwa kama ni kwa ajili ya biashara.

  

 

Share