Zingatio 5: Wakati Ni Huu Wa Ramadhwaan

 

Zingatio 5: Wakati Ni Huu Wa Ramadhwaan

 

Naaswir Hikmaany

 

 

Alhidaaya.com

 

 

Ubora wa mambo ni kujihisabu ya kwamba huna chochote ndani ya kapu lako la thawabu. Hali hiyo itakupatia hima ya kuchuma kheri zaidi na zaidi. Ramadhwaan ni wakati wa kuchuma machumo mema ili kupata salama mbele ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa). Hakuna ajuaye ya kwamba ataishi kuimaliza Ramadhwaan, wala anayeweza kunena ya kuwa ataishuhudia Ramadhwaan ya mwaka ujayo.

 

 

Ramadhwaan ni wakati wa kudhihirisha utiifu mbele ya Muumba, kwani lengo kuu la kuletwa kwetu ni kumuabudu Yeye tu bila ya mshirika:

 

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ ﴿٥٦﴾

Na Sikuumba majini na wana Aadam isipokuwa waniabudu. [Adh-Dhaariyaat: 56]

 

 

Umefika wakati wa kudhihirisha khofu kwa Rabb wetu Mtukufu. Haitokuwa na maana iwapo Ramadhwaan itamalizika hali ya kuwa nafsi haijazuilika kutenda maovu. Sio wakati wa kukaa kucheza bao, karata na mengineyo. Huu ni wakati kwa kila mtu kuirudi nafsi yake kwa mabaya aliyoyafanya.

 

 

Kutoka kwa  Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Swalaah tano, na Ijumaa mpaka Ijumaa, na Ramadhwaan mpaka Ramadhwaan, zitamfidia baina yake madamu atakua ni mwenye kujiepusha na madhambi makubwa)) [Imepokewa na Muslim]

 

 

Huu ni wakati wa kuurekebisha ulimi kuwa ni wenye kusema kweli, kuacha fitna na kuacha kusengenya katika maisha yote yaliyobaki:

 

وَالَّذِينَ هُمْ عَنِ اللَّغْوِ مُعْرِضُونَ ﴿٣﴾

Na ambao wanajiepusha na mambo ya upuuzi. [Al-Muuminuwn: 3]

 

 

Swawm ya kweli kweli ni ile ambayo ulimi pamoja na viungo vyote vinafunga na kuacha maasi kama linavyoachwa tumbo bila ya chakula. Na maovu ya kusengenya ni makubwa kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

 

 أَيُحِبُّ أَحَدُكُمْ أَن يَأْكُلَ لَحْمَ أَخِيهِ مَيْتًا فَكَرِهْتُمُوهُ ۚ وَاتَّقُوا اللَّـهَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ تَوَّابٌ رَّحِيمٌ﴿١٢﴾

Je, anapenda mmoja wenu kwamba ale nyama ya nduguye aliyekufa? Basi mmelichukia hilo! Na mcheni Allaah! Hakika Allaah ni Mwingi wa kupokea tawbah, Mwenye kurehemu. [Al-Hujuraat: 12]

 

Katu mwenye kufunga hatakiwi kupoteza wakati wake hata kidogo kwa mambo ya michezo. Huu ni wakati wa kutembelea wagonjwa ili kujionea tofauti ya uzima na ugonjwa. Ni wakati wa kulisha masikini ili kulichana chana pazia baina ya tajiri na masikini. Ramadhwaan ni wakati wa kuwa na uchu wa kukimbilia mema na pamoja na kuwa na wivu wa wakati wako namna sawa unavyoona wivu kwa ahli yako. Bila ya kusahau kusoma mno Qur-aan, kuswali kwa wingi, kukaa I’tikaaf pamoja na kuhudhuria darsa tofauti.

 

 

Basi tusikae tukawa na hiari katika amri za Rabb wetu. Kwani Analotuamrisha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) lina kheri kwetu. Hekima za Swawm Anazijua zaidi Yeye Mtunga Shariy'ah kwani hatukupewa katika elimu ila kichache mno:

 

وَمَا أُوتِيتُم مِّنَ الْعِلْمِ إِلَّا قَلِيلًا ﴿٨٥﴾

Na hamkupewa ujuzi isipokuwa kidogo tu. [Al-Israa: 85]

 

 

Bila ya kusahau kwamba fadhila za kufunga Ramadhwaan zitalipwa kikamilifu na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Siku ya Qiyaamah:

 

إِنَّ وَعْدَ اللَّـهِ حَقٌّ ۖ فَلَا تَغُرَّنَّكُمُ الْحَيَاةُ الدُّنْيَا وَلَا يَغُرَّنَّكُم بِاللَّـهِ الْغَرُورُ ﴿٣٣﴾

Hakika ahadi ya Allaah ni haki; basi usikughururini uhai wa dunia, na wala (shaytwaan) mwenye kughuri asikughururini kuhusu Allaah. [Luqmaan: 33]

 

 

Share