Inafaa Kufanya Biashara Ya Condom?

SWALI:

 

Mimi ni muislamu na nimejiajiri hapa Dar. Ninakibiashara cha kusafirisha mizigo nchini. Imetokea tenda ya kusafirisha Condom kwenda Lubumbashi Congo. Inalipa vizuri yaani $1000. Tafadhali nipeni maoni kabla ya Ijumaa. Sasa waislamu wenzangu nisaidieni kama nimkabidhi Trucks mbili huyu mtu apakie au la? Kuna container mbili za 40ft tena nyepesi kwaiyo faida juu ya faida maana mafuta yatatumika kidogo. Au niingize Condom kwenye list yangu ya vitu kama POMBE, SIGARA, e.t.c vitu ambavyo sigusi kabisa?

 


JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu biashara ya condom. Kwanza tutazame condom ni nini? Hiki ni kifaa ambacho kinafahamika sana na watu wanaoishi katika zama hizi za utandawazi. Huu ni mpira ambao unatumiwa na wanaume na wanawake nao wana aina zao. Lengo kubwa la utengenezaji wa condom ni kueneza uasherati na zinaa katika mataifa hasa ya Waislamu na ya ulimwengu wa tatu.

 

Wanayotuambia watengenezaji ni kuwa condom ni kifaa cha kudhibiti ukimwi kikiwa kitatumiwa wakati wa jimai. Na hivyo matangazo ambayo twatangaziwa ni kuwa ikiwa huna budi utembee nje basi tumia mpira. Au matangazo mengine yasema, kuwa na mpenzi mmoja. Haya yote yanatupatia maelezo gani hasa sisi Waislamu.

 

Hebu tutazame Uislamu unatuambia nini kuhusu mas-ala tofauti na utambuzi wetu wa halali na haramu. Tufahamu kuwa Uislamu umekuja kutengeneza maadili na tabia za wanadamu na kuwaepusha wao na chochote ambacho kinaweza kuwaharibu na kuwaweka mahali pabaya. Msingi wa Kiislamu ni kuwa, ikiwa kitendo kimekatazwa na kufanywa kuwa haramu basi lolote ambalo linaweza kukusahilisha kufanya la haramu nalo ni haramu. Kwa ajili hiyo, Uislamu unatatua matatizo kutoka kwenye mizizi na sio kwenye matawi.

 

Kwa ajili hiyo, Allaah Aliyetukuka Hakusema msizini bali alisema msikaribie zinaa. Na Mtume naye (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akatuelezea kuwa viungo vyote vinazini; jicho, mdomo, miguu, mikono, na utupu unayakinisha hayo. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hakusema tu kuwa pombe ni haramu bali mwenye kutengeneza, mwenye kubeba, mwenye kunywa, mwenye kuuza, mwenye kumsindikiza mwenziwe, na kadhalika.

 

Tukija katika condom ni kuwa katika nchi ambazo zinauzwa hazitumiwi na wanandoa bali zinatumika katika uzinzi. Kwa minajili hiyo Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametupatia muongozo pale alipotuambia:

"Acha lenye kukutia shaka kwa lisilokutia shaka" (Ahmad, at-Tirmidhiy, an-Nasaa'iy, na imesahihishwa na Ibn Hibbaan na al-Bayhaqiy).

Kule kuwepo na shaka kuhusu hilo ni afadhali Muislamu ajiepushe na biashara aina hiyo.

 

Na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anazidi kutupatia muongozo pale aliposema:

"Hakika halali iko wazi na haramu iko wazi; na baina ya vitu viwili hivi kuna mambo yenye shaka, watu wengi hawayajui. Basi mwenye kuepuka mambo yenye shaka, hakika amehifadhi Dini yake na heshima yake. Na mwenye kuingia katika mambo ya shaka ameingia katika haramu…" (Al-Bukhaariy, Muslim, Abu Daawuud, at-Tirmidhiy na Ibn Maajah).

 

Hivyo nasaha kwako kutoka kwetu kuwa uiache kazi na biashara hiyo mbali na kuwa ina pato na kishawishi kizuri. Na fahamu kuwa Muislamu hataacha la haramu au lenye shaka kwa ajili ya Dini yake isipokuwa Allaah Aliyetukuka Humtolea njia nyingine yenye kheri zaidi.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share