Kutumia Dawa Za Kuzuia Hedhi Wakati Wa Hijjah

 

Kutumia Dawa Za Kuzuia Hedhi Wakati Wa Hijjah

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali:

 

Kuna uhalali gani kwa wanawake kuchelewesha au kusogeza mbele siku zao  za hedhi kwa kutumia dawa wakati wa hija? Hii inafanyika ili kutimiza ibada  nzima ya hija.

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

'Ulamaa wengi wametoa ruhusa mwanamke kutumia dawa za kuzuia hedhi ikiwa anakwenda kutimiza nguzo ya Fardhi ya Hajj, na hoja zao ni zifuatazo:

 

Inafaa kutumia dawa kuzuia hedhi ili mwanamke aweze kukamilisha nguzo yake ya tano ya Kiislamu ikiwa atakhofu  kupatwa hedhi wakati yuko katika taratibu za Hajj, kwa sababu  ya kutokana na umbali wa masafa wa kusafiri na gharama  zake nyingi ambazo pengine atashindwa tena kurudia  kuitimiza nguzo yake miaka mingine.

 

Hapa inafaa tutaje kuhusu wale wanaotaka kutumia dawa hizo kwa kuwawezesha kufunga mwezi mzima wa Ramadhaan.

 

Rai za Maulamaa kuhusu jambo hili zime ikhtilafiana, kuna wachache waliokubali na wengi  wamepinga mwanamke  kutumia dawa hizo katika mwezi wa Ramadhwaan.

 

Wale waliokubali wamesema kwamba shuruti za kutumia dawa hizo ni kwamba mwanamke apate ruhusa kwa Daktari kuwa akitumia dawa hizo hazitomfanyia madhara yoyote kwani sheria ya dini yetu haipendi madhara kwa mtu. 

 لا ضرر ولا ضرار

"Hakuna kuleta madhara wala kudhurian "

 

Wale  waliopinga kabisa kwa kusema kwamba hii na amri ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) aliyowaandikia  binaadamu, kwa hiyo sio sawa kubadilisha maumbile ya mwanamke kama alivyoambiwa Mama wa Waumini 'Aaishah (Radhwiya Allahu 'anhaa) ilipomjia hedhi wakati wa Hajj kama ilivyo katika Hadiyth hii:

 

Imetoka kwa Mama wa Waumini 'Aaishah na  Jaabir bin 'Abdillaah kuwa katika tarehe nane ya mwezi wa Dhul Hijjah siku ijulikanayo kuwa ni  ya 'Tarwiyah' walipokuwa wakielekea Minaa na Nabiy (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) wakaleta talbiya ya Hijja, kisha Nabiy akaenda kwa Bi 'Aishah (Radhwiya Allahu 'anhaa) akamkuta analia, akamuuliza: ((una nini?))  akajibu (Mama wa Waumini 'Aaishah Radhwiya Allahu 'anhaa)  ''Nimepatwa na hedhi na watu wamehirimia na wamefanya twawaaf nami sijafanya vyote hivyo! Na sasa watu wanaelekea kuhiji hivi sasa!!'' Nabiy (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia: 

 

فإن ذلك شيء كتبه الله على بنات آدم، فافعلي ما يفعل الحاج غير أن لا تطوفي بالبيت حتى تطهري

Hili ni jambo Aliloliandika Allaah kwa wanawake  (mabint Adam), basi nenda kaoge halafu kahirimie kisha Hiji na fanya yale anayofanya Mwenye kuhiji isipokuwa kutufu na kuswali)). Mama wa Waumini 'Aaishah akafanya matendo  yote ya Hajj isipokuwa kufanya Twawaaf na Swalaah.

 

Vile vile  kwa Rahma ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ametusahilishia dini yetu kwa kuturuhusu kuweza kulipa siku za Ramadhwaan ambazo mtu akishindwa kufunga ikiwa yuko safarini au ni mgonjwa na hali kama hii ya hedhi ya wanawake kwamba walipe siku zao miezi mingine baada ya kumalizika Ramadhwaan. Kwa hiyo ni bora zaidi mwanamke kukubali amri ya Allaah Aliyowaandikia kupata hedhi kwani kila majaaliwa ya Allaah juu ya binaadamu bila shaka yana hikma na manufaa makubwa kwetu. 

 

فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ ۖ وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَىٰ سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ ۗ يُرِيدُ اللَّـهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلَا يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ وَلِتُكْمِلُوا الْعِدَّةَ وَلِتُكَبِّرُوا اللَّـهَ عَلَىٰ مَا هَدَاكُمْ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ ﴿١٨٥﴾

Na atakayekuwa mgonjwa au safarini, basi (inapaswa kulipa) idadi sawa katika masiku mengineyo. Allaah Anakutakieni mepesi na wala Hakutakieni magumu; na ili mkamilishe idadi na ili mumkabbir Allaah kwa kuwa Amekuongozeni na ili mpate kushukuru. [Al-Baqarah: 185]

 

Na Allaah Anajua Zaidi

 

Share