Uthibitisho Wa Makatazo Ya Ndoa Ya Mut’ah

SWALI:

  

Ndugu zangu wa al-hidaaya naomba kujibiwa suali langu ambalo kwa kweli linanitatanisha sana na kuniumiza kichwa kuhusu ndoa hii ya MUTA'A kwa kweli kuna ninaowasikia kuwa ndoa hii haifai na ni sawa na kuzini na kuna wengine wanasema kuwa ndoa hii haina matatizo kwani ilikuwa inafanyika wakati wa Mtume wetu Muhammad (S.A.W) na pia iliendelea kufanyika wakati wa sahaba wa kwanza Abubakar (R.A) na pia katika kipindi cha sahaba Omar (R.A) pia ilifanyika lakini mwisho wa utawala wake sahaba Omar (R.A) ndipo alipoikataza. Suali langu ni hili alipokuja sahaba Omar (R.A) yeye akaikataza sasa kwa nini sahaba Omar (R.A) aliikataza kulikuwa na hekima yeyote ile hata sahaba Omar (R.A) kuikataza ndoa hii ya MUTA'A? Kuna ambao wanaosema kwa nini kama ndoa hii ilikuwa haifai Mtume wetu Muhammad (S.A.W) mpaka kafika kufa hakushushiwa aya yoyote ile na Allah (S.W) kuambiwa kuwa ndoa hii aikataze?

 


 

 

 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Shukrani kwa swali lako kuhusu ndoa ya Mut’ah.

Hakika ni kuwa Waislamu wengi leo kwa sababu ya msukumo wa Kishia na kuendekeza matamanio yao ya kimwili, tumesukumwa kuikubali ndoa ya Mut’ah na kudanganywa kwa hoja kuwa ndoa hiyo haikukatazwa na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) bali aliyeikataza kwa mujibu wa Mashia ni ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhu) kwa ujanja wao wa kuchukua baadhi ya maneno na kuacha baadhi ya maneno katika Hadiyth; au kuchukua baadhi ya Hadiyth na kuacha zingine nyingi zenye kueleza kinyume. Na alisema kweli Imaam Ash-Shaafi’iy aliposema kuwa ‘Msichukue Hadiyth kutoka kwa Mashia, kwani sijaona watu waongo kuliko wote kama wao.” Minhaajus Sunnah An-nabawiyah.

 

Hakika hilo si kweli kwani ndoa hiyo imekatazwa na Allaah Aliyetukuka pamoja na Mtumewe (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kabla ya kuaga dunia. Uhakika ni kuwa yapo mambo ambayo yalikatazwa mwanzo wakati wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kisha yakaruhusiwa. Mfano wa jambo hilo ni kuzuru makaburi ambalo lilikatazwa na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kisha likaruhusiwa.

Ama jambo lingine ni kule kukubaliwa kwa jambo fulani mwanzo kisha likaja likaharamishwa kabisa. Mfano huu ni ndoa ya Mut’ah ambayo ilikubaliwa kutegemea na ada za Kiarabu, kisha ikakatazwa baada ya Vita vya Khaybar na mara nyengine baada ya kufunguliwa Makkah.

 

Hebu tutazame baadhi ya dalili kuhusiana na hilo katika Qur-aan na Sunnah zilizo sahihi:

 

1.     Allaah Aliyetukuka Anasema: “Lakini wanaotaka kinyume ya haya, basi hao ndio wanaoruka mipaka” (al-Ma’arij 70: 31). Na Aayah hiyo ikarudiwa tena katika Suratul Mu’minuun 23: 7. Wanavyuoni wa tafsiyr kama vile Shaykh Abu Bakr Jaabir al-Jazaa’iriy anasema kuwa Aayah hizi zinakataza ndoa hiyo ya Mut’ah.

 

2.     ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alitoka nje huku akimsikia mtu (Ibn ‘Abbaas) akitaja ndoa ya Mut’ah akamwambia: “Wewe ni mtu uliyesahau, hukumbuki kuwa Mtume amekataza ndoa ya Mut’ah na kula nyama ya punda zama za Khaybar” (Muslim).

 

3.     Na Ibn ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhuma) alisikiliza maelekezo ya kutoka kwa mtoto wa ‘ami yake (yaani ‘Aliy) kwa kuacha msimamo kuwa Mut’ah ni halali kama alivyosema Imaam al-Aluusiy katika tafsiri yake ya Ruuh al-Ma’aaniy: “Ni bora kulifutu jambo hili kwa kusema kuwa baada ya hapo (Ibn ‘Abbaas) aliyarudi maneno yake kulingana na mapokezi ya at-Tirmidhiy, al-Bayhaqiy na atw-Twabaraniy kuwa alisema (Ibn ‘Abbaas): ‘Kwa hakika Mut’ah ilikuwepo mwanzo wa Uislamu, alikuwa mtu huja katika kijiji ilihali hamjui mtu basi huoa kwa muda auonao kuwa atakaa hapo, akapata kuhifadhiwa haja zake na huyo mke na kusimamiwa maslahi yake yote (na huyo mke), mpaka ikateremka Aayah isemayo: ‘Isipokuwa kwa wake zao au kwa wanawake wale iliyowamiliki mikono yao ya kuume. Basi hao ndio wasiolaumiwa’ (Suratul Mu’minuun 23: 6), kwa hiyo kila tupu isiyo mojawapo ya tupu hizi mbili ni haramu” (Juzuu 5, uk. 6 na pia Tuhfatul Ahwadhiy Sherehe ya at-Tirmidhiy, Juzuu 4, uk. 269).

 

Kwa hiyo alilofanya ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhu) wakati wake ni kuwakumbusha Maswahaba ambao wengine walikuwa kama Ibn ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhuma) kuwa Mut’ah imeharamishwa kuanza hapo wakati wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kwa hiyo wakae mbali nayo. ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhu) hakuzua lake jipya bali ni kuitwabikisha shari’ah iliyokuwepo.

 

Mwisho tnugependa kuweka jedwali kuweka wazi suala hili la Mut’ah na ndoa iliyo sahihi. Tafadhali isome kwa makini na uone tofauti za wazi.

 

Ndoa Ya Shariah

Ndoa Ya Mut’ah

Zinaa

1. Walii ni lazima katika Nikaah ya bikra (kutoa idhini).

Akiwa msichana bikra aliye na umri wa miaka kumi, walii si lazima.

Hapana haja ya walii.

2. Mashahidi waadilifu japo wawili na kutangazwa kwa ndoa.

Mashahidi si sharti wala hapana haja ya kutangazwa.

Mashahidi hawatakikani kamwe.

3. Yampasa mume kumpa mke maskani na kumlisha na mengineyo.

Haimpasi mume kumpa mke maskani wala kumlisha.

Haimpasi wala hapana maafikiano kama hayo.

4. Mume hana ruhusa ya kufunga ndoa na zaidi ya wake wanne.

Hapana kikomo cha idadi.

Hapana kikomo.

5. Lengo la ndoa ni mpaka kuachana kwa kheri. Ni daima dawama hadi kufa.

Muda una kikomo uchache wake ni dakika chache, japo baada ya ngono moja.

Muda wake ni kutosheka mume kulingana na maafikiano.

6. Baada ya kufa wote wawili hurithiana, mmoja kumrithi mwenziwe.

Mume na mke hawarithiani hata kidogo.

Hawarithiani.

7. Wakati wa eda yoyote mke hupata mahitajio yake yote, maskani, mavazi na chakula.

Mke hapati kitu baada ya kufarikiana na mume.

Mke hupata kitu walichoagana tu baada ya starehe wala hakuna eda.

8. Mtoto azaliwaye hufuata nasaba ya baba.

Mume ana haki ya kumkana mtoto wake, hivyo kuwa ni wa mama.

Baba ashamkana mtoto kabla ya kuzaliwa.

9. Haijuzu kuoa msichana wa Kimajusi au washirikina.

Hujuzu kufanya Mut’ah na yeyote hata Mmajusi.

Kwa msichana yeyote inafaa.

 

 

 

Tunatumai kuwa hayo tuliyoyaeleza yatakuwa wazi kwa kila Muislamu ili asiwe ni mwenye kudanganyika. Mut’ah ni uzinifu wa wazi kabisa. Mut’ah haimfai Muislamu mzuri mwenye Iymaan yake safi ya kisawasawa.

 

Kadhalika unaweza kusoma jibu jingine kuhusu Ndoa hiyo ya Mut’ah kwa kirefu:

 

Ndoa Ya Mut'ah

 

 

Tunamuomba Allaah Aliyetukuka Atuhidi sote katika njia nyoofu.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share