Huswali Tahajjud Kisha Hupitwa Na Swalaah Ya Alfajiri

 

SWALI:

ASALAM ALYKUM, KWANZA NAWASHUKURU SAAAAANA KWA KUANZISHA HII WEB INSHAALLAH  M/MUNGU AWAJAALIE KHERI DUNIANI NA KESHO AKHERA AMIIIIIN.SASA MIMI NAULIZA MIMI NASALI SALA ZA USIKU NIKIMALIZA HUTAKA NISOME MPAKA SALA YA ALFAJIRI ILI NIPATE KUSALI ALFAJIRI SASA NNAKUA NASINZIA MPAKA NAKUA SIJIWEZI NA USINGIZI UMENICHUKUA SASA NIKILALA SIPATI DHAMBI KWA WAKATI ULE NA ALFAJIRI SIKU NYENGINE INAKUA INANIPITA SIKU NYENGINE NAWEZA KUAMKA PENGINE JUA LIMESHATAKA KUTOKA SASA UNANISHAURI VIPI NA HUWA NIMECHOKA SANA  KWA SABABU MIMI NNA WATOTO NA NIKO PEKE YANGU NYUMBANI KWA HIO HATA NIKILALA NAKUA NACHOKA SANA, NAOMBA JIBU INSHAALLAH.

 

 


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

  

Tunashukuru kuona kwamba dada zetu wamo katika hima ya kufanya ibada zaidi ya fardhi zao na khaswa ibada kama hiyo nzito ya kuamka usiku na kuswali Swalah ya Tahajjud kwani Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema kuwa hiyo ni Swalah bora kabisa baada ya Swalah za fardhi:

 

((أفضل الصلاة بعد الفريضة صلاة الليل))  رواه مسلم.

 

((Swalah iliyo  bora kabisa baada ya Fardh ni Swalah ya usiku)) [Muslim]

 

 Na vile vile jaza yake ibada kama hii ni pepo kama ilivyothibiti katika aya na Hadiyth nyingi mojawapo wa aya ni hii  ifuatayo:

 ((إِنَّ الْمُتَّقِينَ فِي جَنَّاتٍ وَعُيُونٍ))

 

(( آخِذِينَ مَا آتَاهُمْ رَبُّهُمْ إِنَّهُمْ كَانُوا قَبْلَ ذَلِكَ مُحْسِنِينَ))

 

 ((كَانُوا قَلِيلًا مِّنَ اللَّيْلِ مَا يَهْجَعُونَ))

((Hakika Wenye taqwa watakuwa katika Mabustani na chemchem))

((Wanapokea aliyowapa Mola wao . Kwa hakika hao walikuwa kabla ya haya wakifanya mema))

((Walikuwa wakilala kidogo tu usiku)) [Adh-Dhaariyaat: 15-17]

 

Lakini inapasa kutambua kwanza kabla ya kutekeleza ibada za Sunnah, Muislamu anatakiwa kwanza atimize zile ibada za fardhi ndio aweze kupata fadhila na thawabu za ibada hizo za Sunnah kama ilivyokuja katika Hadiythul-Qudsiy ifuatayo:.

 

عن أبي هريرة رضي الله عنه عن النبي صلى الله عليه وآله وسلم قال: (( إن الله عزوجل قال: ((مَنْ عَادَى لِي وَلِيَّاً فَقَدْ آذَنْتُهُ بِالْحَرْبِ، وَمَا تَقَرَّبَ إليَّ عَبْدِي بِشَيْءٍ أَحَبَّ إليَّ مِمَا افْتَرَضْتُ عَلَيْهِ، وَمَا يَزَالُ عَبْدِي يَتَقَرَّب إليَّ بِالنَوَافِلِ حَتَى أُحِبَّهُ، فَإِذَا أَحْبَبْتُهُ كُنْتُ سَمْعَهُ الَذِي يَسْمَعُ بِهِ، وَبَصَرَهُ الَذِي يُبْصِرُ بِهِ، وَيَدَهُ الَتِي يَبْطِشُ بِهَا، وَرِجْلَهُ الَتِي يَمْشِي بِهَا، وَإِنْ سَأَلَنِي لأُعْطِيَنَّهُ، وَلَئِنْ اسْتَعَاذَنِي لأُعِيذَنَّهُ، وَمَا تَرَدَّدْتُ عَنْ شَيْءٍ أَنَا فَاعِلُهُ تَرَدُّدِي عَنْ نَفْسِ الْمُؤْمِنِ، يَكْرَهُ الْمَوْتَ وَأَنَا أَكْرَهُ مَسَاءَتَهُ))  البخاري

Imetoka kwa Abu Hurayrah رضي الله عنه kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema ((Allaah Mtukufu Amesema:Yeyote yule afanyae uadui kwa walii Wangu Nitatangaza vita dhidi yake. Mja wangu hanikaribii na kitu chochote Ninachokipenda kama amali Nilizomuwajibisha, na mja Wangu huzidi kunikaribia kwa amali njema za Sunnah ili Nimpende. Ninapompenda, huwa (Mola) masikio yake anayosikilizia, macho yake anayoonea, mikono yake anayokamatia, miguu yake anayokwendea. Lau angeliniomba kitu bila shaka Ningelimpa, lau angeliniomba himaya bila shaka Ningelimpa. Sisiti juu ya kitu chochote kama Ninavyosita (kuichukua) roho ya mja Wangu Muumin. Anachukia mauti, Nami  Nachukia kumuumiza)) [Al-Bukhaariy]

 

Hadiyth hii ina maana ifuatayo:

 

(Yeyote yule anaemkaribia Mwenyezi-Mungu kwa yale yaliofaradhishwa na kwa amali za nawaafil (zisizo wajibu), Mola Humkaribia na Humnyanyua kiwango cha ukamilifu wa Iymaan (daraja ya Ihsaan) mpaka ile elimu kifuani mwake inaonekana na jicho la nafsi. Kujaza ujuzi wa Mwenyezi Mungu moyoni hufuta kila kitu isipokua Mwenyezi Mungu, kwa hivyo akisema, akitembea, akisikiliza, akiangalia, akikamata yote huwa kwa ajili ya Mwenyezi-Mungu)

Kwa hiyo tunaona umuhimu kwanza wa kutimiza fardhi kisha ndio ifuatilie Sunnah. Sasa kama unatekeleza Sunnah na kukaa macho sana hadi inakupita Swalah ya Alfajiri ambayo ndio fardhi itakuwa hukufanya jambo la maana. 

 

Swalah ya Tahajjud haina lazima mtu akeshe sana usiku, kwani hata ukiamka kwa Raka'a tatu inatosheleza kabisa kupata fadhila zake na Allaah سبحانه وتعالى hamkalifishi mtu jambo asiloliweza:

 

((لاَ يُكَلِّفُ اللّهُ نَفْسًا إِلاَّ وُسْعَهَا))

((Allaah Haikalifishi nafsi yoyote ila kwa kadiri ya iwezavyo)) [Al-Baqarah: 286]

 

Vile vile sio lazima usome sana kama ulivyosema, kwa Rahma ya Allaah Ametujaalia fadhila nyingi hata kwa ibada ndogo tu kama kusoma aya kumi tu zinakutosheleza kuwa hutokuwemo katika miongoni mwa walioghafilika.

 

عبدالله بن عمرو عن النبي صلى الله عليه وسلم ((من قام بعشرِ آياتٍ لم يُكتبْ من الغافلينَ ، ومن قام بمئةِ آيةٍ كُتبَ من القانتينَ ومن قام بألفِ آيةٍ كُتبَ من المُقَنْطِرينَ)) صحيح أبي داود  

 

Amesimulia ‘Abdullaah bin ‘Amr (رضي الله عنه): Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Atakayesimama usiku kuswali na akasoma Aayah kumi, hatoandikiwa kuwa miongoni mwa walioghafilika, na atakayesimama kuswali akasoma Aayah mia, ataandikiwa ni miongoni mwa watiifu, na atakayesimama kuswali akasoma Aayah elfu, ataandikwa miongoni mwa wenye mirundi (ya thawabu).’ [Abuu Daawuwd, Al-Albaaniy ameisahihisha: Swahiyh Abiy Daawuwd (1398), Swahiyh Al-Jaami’ (6439)]

 

(Maana ya mirundi ni wale walio na mrundi wa thawabu)

 

Kwa hivyo ni vizuri kuamka kuswali Tahajjud japo kwa aya kumi  kisha ukarudi kulala kama umechoka ili upate kuamka Alfajiri kuwahi Swalah ya fardhi.

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share